Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira Dkt. Selemani Jafo, Naibu Waziri na wataalamu wa Wizara na wadau wa maendeleo kwa mchango mkubwa sana kwenye kuhifadhi mazingira.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia kwenye suala la umuhimu wa kubadilisha sheria na kurudisha eneo la Half Mile kwa wakazi wa vijiji vilivyomo katika mipaka ya Mlima Kilimanjaro ili washiriki kikamilifu kutunza mazingira ya Mlima Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, Half Mile ni eneo lenye upana wa kati ya 0.5-0.8 ya mile. Eneo hili lilikuwa linatenganisha Mlima Kilimanjaro na makazi ya watu. Eneo hili kwa upande wa majimbo ya Moshi Vijijini na Vunjo linajumuisha vijiji 40.

Mheshimiwa Spika, wakoloni wa Tanganyika walitumia sheria kandamizi kujimilikisha ardhi ya wana Kilimanjaro na rasilimali za msitu wa Mlima Kilimanjaro na kuwapora wana Kilimanjaro haki yao ya kufaidi rasilimali zao za asili.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa 1941 wakoloni walianzisha Sheria ya Half Mile Strip kwa lengo la kuwapatia majirani wa msitu Kilimanjaro huduma za mazao ya misitu kama vile dawa za asili (ngesi), mboga za majani (mnafu) miti ya kujenga nyumba, kuni na majani ya ng’ombe.

Mheshimiwa Spika, tofauti na malengo ya kuanzishwa kwa eneo la Half Mile, kazi za kibinadamu zilisababisha uharibifu wa mazingira katika Half Mile na yale maeneo ya hifadhi kwa kukata miti, kupasua mbao, kuchoma misitu, kuchunga mifugo na kuendesha shughuli za kilimo ndani ya hifadhi. Hii ilitokana na kukosekana kwa usimamizi mahiri kutoka katika mamlaka husika Serikalini.Mheshimiwa Spika, baada ya uharibifu huu, Serikali ilisimamisha vijiji vyote 40 kutokutumia Half Mile Strip toka mwaka 2004, kwa sheria iliyoanza kutumika mwaka 2005. Hii ilitokana na kusainiwa kwa sheria ya kuziingiza Half Mile Strip za maeneo ya Moshi Vijijini na Rombo iliyotiwa sahihi na Marehemu Rais Mkapa tarehe 18/7/2005 na kutangazwa katika Gazeti la Serikali tarehe 16.9.2005.

Mheshimiwa Spika, baada ya zuio hili, Serikali yetu iliondoa ile huruma ya wakoloni kwa Wana Kilimanjaro ya kutumia ile buffer zone ya Half Mile. Siku hizi hakuna cha Half Mile tena na ukikamatwa na maaskari wa KINAPA utakuwa na bahati mbaya sana.

Mheshimiwa Spika, wapiga kura wangu wamenituma niiombe Serikali ibadilishe sheria hii kwani baada ya kunyima watu wasitumie Half Mile, hii imesababisha matatizo makubwa ikiwa ni pamoja na uharibifu mkubwa wa mazingira ya msituni Kilimanjaro kwa kupanuka kwa shughuli za kukata miti ndani ya msitu ikifanywa na maharamia; kuongezeka kwa wanyama waharibifu wa mazao kwenye mashamba ya wakulima kama nyani, ngedere na kima kuingia kwenye mashamba ya wanakijiji na kuharibu mazao.

Mheshimiwa Spika, kabla ya mwaka 2005 shughuli za wananchi kwenye Half Mile zilizuia wanyama kuingia vijiji vya mpakani na ilikuwa hakuna uharibifu wa mazao.

Mheshimiwa Spika, Makamu wa Rais Mstaafu Dkt. Ali Mohamed Shein alipotembelea Mkoa wa Kilimanjaro mwaka 2008 akiambatana na Waziri wa Maliasili Profesa Jumanne Maghembe wananchi walimweleza matatizo yaliyojitokeza baada ya Serikali kuunganisha eneo la Hifadhi la KINAPA na misitu ya hifadhi za asili.

Mheshimiwa Spika, baada ya ziara hiyo, Wizara ilikaa na kuiagiza TANAPA (kwa barua yenye Kumb Na. CAB. 315/ 484/01/A ya tarehe 22.1.2008 ya Waziri Profesa Maghembe kwenda kwa Mwenyekiti wa Bodi ya TANAPA, na barua Kumb Na. CJA.246/374/01/42 ya tarehe 27.2.2009 ya Katibu Mkuu Dkt. Ladislaus Komba kwenda kwa Mkurugenzi wa TANAPA) wachore ramani upya na kutenga eneo la Half Mile liwe nje ya Hifadhi ya KINAPA kama ilivyokuwa awali.

Mheshimiwa Spika, pamoja na maelekezo hayo hapo juu na kukumbushwa mara kwa mara na wadau wa maendeleo wa Mlima Kilimanjaro hadi leo ramani hiyo haijatoka na sheria hii kandamizi kwa wananchi wa vijiji 40 vya mpaka na Mlima Kilimanjaro bado inawanyanyasa.

Mheshimiwa Spika, sheria kandamizi kama hii si nzuri na zinasababisha migogoro isiyo ya lazima baina ya wananchi na Serikali yao na uhifadhi wa mlima unawatenga wananchi wa vijiji jirani.

Mheshimiwa Spika, kama mwakilishi wa wananchi, hata mimi naikataa kabisa sheria kandamizi kwa wapiga kura wangu na ninamwomba Waziri Jafo amshauri Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan aliangalie jambo hili kwa jicho la huruma kama alivyoelekeza Makamu wa Rais mwaka 2008 ili wananchi wawe sehemu ya kutunza mlima na kuzuia majangili wasiingie mlimani kukata miti na kuharibu mazingira ya Mlima Kilimanjaro. Wananchi wanaoishi vijiji vya mpakani wakielekezwa na kukabidhiwa maeneo ya kulinda, wanaweza wakawa walinzi bora bila hata kutumia bunduki.

Mheshimiwa Spika, sheria ikibadilishwa, Half Mile Strip inaweza kutumika kwa mafanikio makubwa chini ya usimamizi wa Serikali Kuu, Serikali ya Mkoa, Wilaya, Kata na Vijiji na kusaidia wananchi wa vijiji husika kuutunza mlima na kuboresha mazingira yake; kuwapatia wananchi huduma na kuinua uchumi wa wananchi, Wilaya, Mkoa na Taifa.

Mheshimiwa Spika, sheria ikibadilishwa, wananchi washauriwe kupanda miti ya muda mfupi kama cyprus, pine na mikaratusi na aina nyinginezo zinazokua haraka kwa ajili ya nguzo za umeme, nguzo za ujenzi wa nyumba zikiwemo ghorofa, miradi kama hii iko Iringa. Rais akiruhusu hili, nchi nzima itanufaika kwani Kilimanjaro ina miundombinu bora ya kusafirisha hizi bidhaa na kuzisambaza zinakohitajika.

Mheshimiwa Spika, kama hatua stahiki hazitachukuliwa mapema, hali itakuwa tete sana miaka michache ijayo, na mazingira ya Mlima Kilimanjaro huenda yakaharibika zaidi.

Mheshimiwa Spika, KINAPA hawana watumishi wa kutosha wa kuulinda mlima na kupanda miti mingi ya kutosheleza kulinda mazingira ya mlima Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo yangu hapo juu, naunga mkono hoja.