Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika Bunge lako hili Tukufu. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kuwa hai na kuiona siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii pia kuipongeza Kamati ya Sheria Ndogo; kiukweli wamefanya kazi kubwa na ninawapongeza sana. Pia ninampongeza Mwenyekiti wetu kwa namna alivyowasilisha vizuri taarifa ya kamati yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitajielekeza kwenye mambo machache ya upande wa sheria ndogo. Tumebahatika kuchambua sheria nyingi, na ni ukweli usiofichika bado sisi kama Bunge hili tuna kazi ya kufanya. Tumekasimu madaraka haya kwa baadhi ya taasisi zenye uwezo wa kutunga hizi kanuni lakini tunaona bado changamoto ya hizi sheria ndogo ni nyingi mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria ndogo nyingi zinakosa uhalisia, hazitekelezeki na zinaleta changamoto sana kwa maisha ya wananchi. Ukiangalia sheria ndogo ya usafi wa mazingira ya Wilaya ya Misungwi ya mwaka 2022 inatoa katazo la watu kufanya shughuli yoyote ya maendeleo kuanzia saa 12 asubuhi mpaka saa nne asubuhi kwa lengo la kufanya usafi wa mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo linaweza likawa zuri la kufanya usafi lakini kutoa katazo la kufanya shughuli yoyote ya maendeleo, hili si sawa. Sisi tunadhani kama taifa tulitakiwa tufikirie kwenda mbele na si kufikiria kurudi nyuma. Kama lengo likiwa ni kufanya usafi tuondoe hili zuio la kusema shughuli za maendeleo zozote zisifanyike kwa masaa haya matano. Sheria hii inaleta usumbufu sana kwa wananchi. Jiulize, wewe eneo la biashara kila siku uko hapo unafanya biashara, ni usafi gani huo utakaohitaji kuufanya kwa masaa matano?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo watu ambao wanaweza wakafanya usafi kwa nusu saa, waruhusiwe kuendelea na shughuli zao za maendeleo. Wapo watu ambao wanaweza wakafanya usafi kwa muda wa saa moja, waruhusiwe kuendelea na shughuli zao za maendeleo. Kuna mama zetu hawa ambao wanafanya biashara ndogo ndogo. Mama anapika vitumbua, biashara yake anatakiwa afanye asubuhi. Unapomwambia kuanzia saa 12 mpaka saa nne asifanye shughuli yoyote tunarudisha uchumi nyuma wa Watanzania hawa masikini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii haiko tu Misungwi, sheria hii iko maeneo mengi; na moja ya maeneo ambayo sheria hii inatumika, hata hapa Dodoma sheria hii inatumika. Sheria hii inatumika Ikungi, Nsimbo na maeneo mengi ya nchi yetu. Sisi kama Kamati tunaona sheria hii imepitwa na wakati, tunarudisha nyuma maendeleo ya wananchi wetu kwa kuweka sheria hii ambayo ina usumbufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiitazama sheria ndogo hii kwenye utekelezaji wake, haiwezekani. Hata kwenye practice huko mitaani watu hawaendi kufanya usafi kama tulivyotarajia; wanachokifanya ni kufunga biashara zao ifike saa nne waweze kufungua ili wasikamatwe na kupigwa faini. Sasa tujiulilze, sisi kama taifa tunataka nini? Tunataka usafi au tunataka watu wafunge biashara kusubiri saa nne ndipo wafungue?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe, kama kamati ilivyoshauri jambo hili kamati imekataa na haikubaliani nalo. Ukija sheria Ndogo ya Usafi wa Mazingira ya Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi inazungumzia ni kosa kwa abiria kutupa takataka nje ya chombo cha usafiri. Kweli kila mtu anakubaliana na jambo hilo; lakini kusema tukio hilo au kosa hilo litachukuliwa kama limefanywa na mmiliki wa chombo hicho, hiyo siyo sawa. Kwanza ni kinyume cha sheria, ni kinyume cha misingi ya sheria lakini pia kinapingana na sheria mama. Ukisoma kifungu cha 40 cha Sheria ya Mazingira kinazungumzia principle ya mtu aliyefanya kosa ndiye awajibike. Haiwezekani leo abiria atupe takataka, faini alipe mwenye basi, haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sisi kama kamati tumeshauri, kama kosa litafanywa na abiria, basi awajibishwe abiria, kama kosa litafnywa na kondakta, basi awajibishwe kondakta na kama kosa litafanywa na mwenye chombo, basi awajibishwe mwenye chombo; huo ndio uliokuwa usahuri wa Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hizi ndogo sisi kama Bunge tunazipitisha hapa; na tumetoa mamlaka, ukisoma Cap 1 kifungu kile cha 37 kinatoa mamlaka ya sheria hizi kuanza kutumika kabla hazijapitishwa na Bunge. Shida kubwa ya changamoto hii inaanzia hapo. Kwa kuwa tumeruhusu sheria hizi zianze kutumika kabla hazijapitishwa na Bunge, hicho ndicho kimekuwa kichaka cha wananchi wetu kuteswa na sheria hizi mbovu, kukandamizwa na kanuni hizi mbovu na mwisho wa siku zinaletwa tayari wananchi wameshaumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa nina ombi kwa Bunge hili. Kama itakupendeza kuna haja sisi kama Bunge kufanyia marekebisho Kifungu cha 37 cha Sheria ya Tafsiri. Kifungu cha 37 kiondoe ile hali ya kuiruhusu sheria hizi kuanza kutumika kabla hazijapitiwa na Bunge. Kwa sababu unaona changamoto hizi, unapozungumzia Misungwi wana sheria hii.

Pia Halmashauri ya Nsimbo ime-copy sheria hizi nao wana sheria hizi hizi. Kwa hiyo ukifanya tathmini utagundua kuna sheria nyingi ndogo mbovu zinazoumiza wananchi na bado zinaendelea kutumika zikisubiri mpaka Bunge lije liziite, lizichambue na lizipitishe. Kwa hiyo mimi niombe Waheshimiwa Wabunge, kama itawapendeza kuna haja ya Serikali kuleta sheria ili sisi tuifanyie marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimalizie kwa kusema yafuatayo. Mwaka 2019, sisi kama Bunge tulipitisha sheria ndogo, na sheria hiyo ilikuwa ni kanuni ya kukataza mifuko ya plastic. Leo ni takribani miaka mitatu tu tangu zuio hilo litokee lakini naomba nikupe taarifa, mifuko ya plastic sasa iko mitaani na inatumika, na Serikali iko kimya haitoi tamko lolote kuhusu kitendo hicho kinachoendelea. Sasa hii inashangaza. Sisi kama Bunge tunakaa hapa, tunapitisha sheria, tunatoa maazimio yetu lakini utekelezaji wake ndio unakuwa na changamoto hizo. Mimi niombe, niiombe Serikali. Kwanza inajukumu la kufanya kujua kwamba taarifa ya mifuko inayo au haina.

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi? Mheshimiwa Ramadhan.

T A A R I F A

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji dada yangu Sylvia na mwanakamati mwenzangu kwamba Zanzibar ilipitisha kanuni kama hiyo anayoisema ya kuzuia mifuko ya plastic, leo Zanzibar mifuko ya plastic ni historia. Kama wenzetu wanataka kwenda kujifunza waende Zanzibara wakajifunze, wao wamewezaje, huku tushindwe tuna nini?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sylvia unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea hiyo taarifa kwa mikono miwili, si jambo baya kujifunza kwa waliofanikiwa. Kwa hiyo hata sisi kama tumeona changamoto ya utekelezaji wa mifuko hii ya plastic bado tuna nafasi ya kwenda kujifunza kwa wenzetu, kwa hiyo siyo jambo baya kujifunza kwa waliofanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimalizie kwa kusema, ninaipongeza Kamati; lakini nilikuwa na ombi maalum kama Kamati itaona inafaa kuongeza azimio kwenye Maazimio ya Kamati tuitake Serikali ilete sheria cap 1, interpretation of laws act, ije hapa tuifanyie marekebisho hicho kifungu cha 37. Kwa sababu kifungu hicho ndicho kinacholeta changamoto zote hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na ninaunga mkono hoja za Kamati zote mbili.