Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kutoa mchango wangu kuhusu taarifa ya Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1972, aliyekuwa Mfalme wa Dubai wakati huo, Sheikh Rashid Bin Maktoum, alikuwa na ndoto ya kujenga bandari kubwa sana katika ukanda ule wa Ghuba ya Uajemi na Mashariki ya Kati kwa ujumla lakini kwa bahati mbaya washauri wake kutoka Uingereza walimwambia hapana mradi huu hautakuwa na manufaa makubwa ya kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa bahati mbaya washauri wake kutoka Uingereza walimwambia hapana mradi huu hautakuwa na manufaa makubwa ya kiuchumi. Sheikh Maktoum alikataa alisema hapana sikubaliani na ushauri huu. Hata kama mradi huu hautakuwa maslahi ya kiuchumi nitautekeleza kwa sababu ninaamini wajukuu na watoto wangu hawataweza kuutekeleza mradi huu miaka mingi ijayo kwa sababu gharama zake zitakuwa zimepanda sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajifunza nini? Tunachojifunza ni kwamba, tukitaka kupiga hatua ya maendeleo ya haraka kama Taifa tunapaswa kuwa na viongozi, na ninaposema viongozi sina maana ya viongozi wa kitaifa nina maana ya Waheshimiwa Mawaziri, Wabunge, Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa; tunahitaji kuwa na viongozi wa aina gani? tunahitaji mambo mawili. Kwanza tunahitaji viongozi wenye maono makubwa, wanaozingatia maslahi ya kizazi kinachokuja kuliko kizazi cha sasa. Pili tunahitaji viongozi wenye ujasiri wa kufanya maamuzi magumu kwa sababu kutakuwa na watu maamuzi hayo wanayatilia shaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nayasema haya; kwa zaidi ya miaka 15 tumekuwa tukizungumza utekelezaji wa mipango ya utekelezaji wa miradi mikuu miwili, mradi wa makaa ya mawe na chuma kule Liganga na Mchuchuma pamoja na mradi wa kusindika gesi asilia kule Lindi. Kwa bahati mbaya katika kipindi cha miaka 15 mpaka leo miradi hii haijatekelezwa

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maoni yangu, nadhani kama miradi hii ingetekelezwa miaka 15 iliyopita, Taifa letu lingepata maslahi makubwa sana ya kiuchumi, na nitayataja. Kwanza gharama za miradi hii zingekuwa chini sana kuliko ilivyo leo, pili tungetekeleza mradi wa gesi asilia miaka 15 iliyopita leo tungenufaika na soko kuu sana linalotokana na uhaba wa gesi asilia duniani unaotokana na vita vya Ukraine na Urusi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika tungetekeleza mradi wa gesi asilia miaka 15 iliyopita leo tungepata gesi nyingi sana inayotumika katika kuendesha mitambo na magari na hatimaye kupunguza uagiziaji wa mafuta kutoka nje. Lakini kwa upande wa chuma leo tungekuwa na chuma cha kutosha kwa ajili ya kutekeleza mradi wa reli ya kati. Hivi sasa Taifa letu linatumia kiasi kikubwa sana za fedha za kigeni kwa ajili ya kuagiza chuma kinachohitajika katika ujenzi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, tungetekeleza miradi miaka 15 iliyopita ingetusaidia sana kwa sababu naamini miaka mitano mpaka 10 inayokuja mahitaji ya gesi asilia duniani yatakuwa yamepungua sana, kwa maana hiyo gesi asilia haitakuwa na faida kubwa kwa Taifa letu. Kwa nini nasema hivyo? Hivi sasa mjasiriamali mkuu sana duniani anayeitwa Elon Musk ameshaanza uzalishaji wa magari yanayotumia umeme. Jambo hilo likifanyika kwa kiwango kikubwa gesi haitakuwa na matumizi makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mataifa mbalimbali tayari yameshaanza utafiti hivi sasa wa namna ya kutumia gesi ya hydrogen kama chanzo kikuu cha nishati. Jambo hilo likifanyika gesi asilia ya Tanzania haitakuwa na maslahi makubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa ushauri wa mwanadamu anayeaminika kuwa mtu mwenye busara kubwa sana kupata kutokea hapa duniani Mfalme Suleiman. Mfalme Suleiman aliwahi kusema maneno haya, na sisi kama viongozi tunapaswa kuyazingatia; akasema hakuna wakati mzuri wa kutekeleza mambo makubwa na muhimu kwa wanadamu kuliko sasa hivi. Tusisubiri muda unaokuja kwa sababu huo muda utakaokuja hatuna uhakika kwamba kila kitu kitakuwa sawa. Lakini, mwisho hatujui Mwenyezi Mungu amepanga lini na nini, kesho na kesho kutwa, kwa hiyo tunapaswa kutekeleza leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali tunapaswa kufanya kila linalowezekana sisi kama Taifa tuitekeleze miradi hii sasa kwa sababu hatujui kitakachotokea baada ya miaka mitano au kumi ijayo, linalowezekana leo lisingoje kesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)