Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hizi Kamati mbili, Kamati ya Miundombinu pamoja na Kamati ya Mifugo, Kilimo na Maji.

Mheshimiwa Spika, nikianzia na Kamati ya Kilimo, usimamizi wa rasilimali za uvuvi. Nimepokea kwa masikitiko makubwa sana juu ya taarifa ya kupungua kwa samaki katika maziwa, mabwawa na mito yetu. Maelezo ya kamati ni kwamba upungufu huu unatokana na usimamizi hafifu wa rasilimali, lakini wakaenda mbali wakasema samaki aina ya sangara kwenye Ziwa Victoria wamepungua kwa 50% na wakaenda mbali zaidi wakasema sasa hivi samaki wazazi wamebaki 0.4%. Sasa kama Ziwa Victoria samaki wazazi wamebaki 0.4%, maana yake ni kwamba ziwa letu hilo linaenda kuwa sawa tu na swimming pool kwa sababu huwezi ukawa na Samaki wazazi 0.4% na ukawezesha kuwepo kwa samaki majini.

Mheshimiwa Spika, kwa takwimu zinazoishia Desemba, 2020 samaki wazazi kwenye Ziwa Victoria walifikia 5.2% na kima cha chini kinatakiwa walau wasiwe chini ya 3%. Kwa hiyo hili ni jambo ambalo linahitaji kuchukuliwa hatua haraka sana na wameeleza mpaka madhara yake kwamba kwa vyovyote vile maana yake viwanda vyetu haviwezi kuzalisha tena inavyotakiwa, viwanda vingi vitafungwa, ajira zitakosekana katika hilo eneo, chakula kitakosekana hapa nchini, bei ya chakula cha samaki itakuwa ni kubwa, madhara ni mengi yanayoweza kupatikana.

Mheshimiwa Spika, sasa tufanye nini? Tatizo kubwa hapa na ninachojiuliza nini chanzo cha usimamizi hafifu, kwa sababu kamati inatueleza hapa inasema inaitaka Serikali idhibiti uvuvi haramu kwa kutumia njia sahihi ambazo hazitwezi utu. Nakubaliana nao lakini chanzo cha usimamizi hafifu ni nini mpaka maji yetu yamefikia hiyo hatua.

Mheshimiwa Spika, nina mapendekezo yafuatayo kuongeza kwenye pendekezo la Kkamati kwamba Bunge liitake Serikali kuwasilisha Bungeni chanzo cha usimamizi hafifu katika rasilimali za uvuvi ili Bunge liweze kuchukua nafasi yake. Pendekezo la pili, Bunge liitake Serikali kudhibiti uvuvi haramu na biashara haramu ya mazao ya uvuvi katika maeneo yote kwa mujibu wa sheria zilizopo.

Mheshimiwa Spika, hii Wizara ukiiangalia mapato yanayotokana na uvuvi yameanguka vibaya sana, mapato yatokanayo na mifugo yameanguka vibaya sana. Sasa hili tatizo ni kubwa na moja ya mambo mengine nitaeleza huko kwenye mfumko wa bei kwamba huwezi ukau-control mfumko wa bei kama nchi haina chakula. Kama samaki wanauzwa kwa bei kubwa na hawapatikani, huwezi ku-control mfumko wa bei. Sasa suala hili ni lazima tulichukulie kwa ukubwa kama lilivyo kwa ukubwa kama Wawakilishi wa wananchi.

Mheshimiwa Spika, suala la pili limezungumzwa na Kamati ya Miundombinu, Kamati hii imelalamika sana juu ya uingiaji kwenye mikataba na Wakandarasi wasiokuwa na uwezo, juu ya miradi mingi ya maendeleo kutelekezwa na kukaa kwa muda mrefu bila kumalizika na juu ya miradi mingi kutekelezwa chini ya viwango.

Mheshimiwa Spika, ni lini Bunge lako linaanza usimamizi wa Serikali? Hapa tulilalamika, Wabunge walilalamika, Mkataba wa TRC na Kampuni ya China Civil Engineering Construction Corporation tukasema kwamba baada ya kupatikana kwamba tender yao kwenye mfumo wa TANePS tukasema unawezaje mradi mkubwa kama huu ukaupata kwa njia ya single source? Wabunge wakahoji hapa, mradi mkubwa wa trilioni 6.34 unatumiaje mfumo wa single source? Mfumo ambao hauruhusu competition, hauruhusu ushindani na ni mfumo ambao mtu anaweza akapendelea kampuni anayoitaka yeye, anaweza akaingia kwenye rushwa, huwezi kumkwamua katika mfumo wa single source, tukalalamika Wabunge hapa.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu kampuni hii iliyokuwa inaingia mkataba CCECC iliingia mkataba lot six, Tabora-Kigoma kilomita 506 kwa trilioni 6.34, lakini wakati huohuo imeshapewa Tenda ya Isaka-Mwanza kilomita 341 kwa trilioni 3.12, unawezaje kuipa mkataba mwingine wakati ina mkataba mbichi kabisa huo wa Isaka-Mwanza? La pili, kampuni haijawahi kujenga hata kilomita moja na mbaya zaidi kipande cha Kigoma-Tabora ndio sasa hivi ni kipande ambacho kina gharama kuliko vipande vyote.

Mheshimiwa Spika, average ya mradi huohuo ambao Kampuni ya CCECC ndio inautekeleza wa Isaka- Mwanza, wastani wa kilomita moja ya SGR ni bilioni 9.1, lakini wastani wa kilomita moja katika kipande cha Tabora - Kigoma bilioni 12.5, tafauti ya bilioni 3.4 kwa kilomita. Mbaya zaidi wakati huo wataalam wetu wanafanya usanifu wa kina wa kujenga barabara kipande cha Tabora - Kigoma walisema kipande hicho kingeweza kujengwa kwa trilioni 4.89, average ya shilingi bilioni 9.5 kwa kilomita, lakini tenda imekuja kutoka ya trilioni 6.4 tofauti ya trilioni 1.5. Sasa mkataba wa aina hii unakubaliwaje? Hivi juzi Serikali imesaini huo mkataba licha ya Bunge lako kutoa tahadhari zote lakini Serikali imesaini huo mkataba.

Mheshimiwa Spika, naomba kupendekeza mambo yafuatayo kuhusu mkataba huu: -

Mheshimiwa Spika, moja, Bunge liitake Serikali kuwasilisha taarifa ya mchakato wa manunuzi Bungeni kuanzia kutangaza zabuni ya tathmini ya utoaji wa zabuni ya SGR kipande cha Tabora - Kigoma kilomita 506. Mkataba huu uwasilishwe Bungeni na kazi hii inaweza ikafanywa vizuri sana na Kamati ya Miundombinu, lakini Kamati ya Katiba na Sheria wakawasilisha mchakato wote. Mkataba huu unaenda kuwa gharama zaidi ya ile inayotakiwa kwa trilioni 1.7, Taifa linakwenda kuingia na wataalam wetu wamesaini, Wabunge wamelalamika hapa viwango na nini na nini, mambo yote yanafanyika huko miundombinu, lakini hawakusikilizwa.

Mheshimiwa Spika, pili, ufanyike Ukaguzi Maalum, CAG na PPRA waunde timu ya pamoja na PCCB waukague mradi huu na kutoa taarifa za kiukaguzi juu ya kile kilichofanyika katika Mradi wa SGR kipande cha Tabora - Kigoma. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)