Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Jerry William Silaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja iliyoko mezani ya Ofisi ya Rais TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kuipongeza sana Wizara ya Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa kazi nzuri sana wanayoifanya. Nampongeza kaka yangu Mheshimiwa Innocent Bashungwa, Mbunge kwa kuaminiwa na kuteuliwa kuiongoza Wizara hii na Naibu Mawaziri wake Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange na Mheshimiwa David Silinde kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa kuwa karibu na Wabunge kwa kutusikiliza na kuwa wanyenyekevu katika kutumikia Taifa letu. Binafsi niwaahidi ushirikiano, vijana wenzetu tupo tutawalinda, tutawatetea katika kutekeleza majukumu yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nimpongeze Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha nyingi za maendeleo kupitia kwenye Wizara hii. Tumesikia kwenye Hotuba ya Waziri, fedha zilizokuja za barabara kupitia TARURA kila Jimbo tumepata fedha hizi, tunaishukuru na kumpongeza sana Rais. Tumepata pesa za tozo kujenga vituo vya afya, Jimbo la Ukonga tumepata bilioni 1.5, Kituo cha Afya Kipunguni kinajengwa, Kituo cha Afya Majohe na Kituo cha Afya cha Zingiziwa tunaishukuru na kuipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuleta fedha za elimu bila malipo, shilingi bilioni 1.2 kwenye elimu ya msingi na shilingi bilioni 3.84 kwenye elimu ya sekondari kwenye Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam zimepokelewa, tunaishukuru na kuipongeza Serikali. Ujenzi wa zile shule za kimkakati kwenye Mradi wa SEQUIP fedha zimeanza kupokelewa na kule Jimbo la Ukonga shule itajengwa kwenye Kata ya Mbondole na kuna mpango mwingine wa shule nyingine kwenye Kata ya Kitunda, tunaishukuru sana Serikali.

Naomba Serikali, niiombe sana tuendelee kutenga fedha hasa za barabara kwenye majimbo yote lakini kwenye Jimbo la Ukonga tunaomba sana Serikali, uendelezaji wa mradi wa DMDP awamu ya pili ambacho ndiyo kilio kikubwa cha wananchi wengi wa Jimbo la Ukonga na Mkoa wa Dar es Salaam kama wenzetu tulivyosikia hapa kwenye hotuba ya Waziri, mradi wa TACTIC ambao ni uendelezaji wa mradi wa Tanzania Strategic City Project ambao umeanza, tunaiombe Serikali ijitahidi kuongeza kasi ya mazungumzo na Benki ya Dunia ili Mradi wa DMDP awamu ya pili na wenyewe uweze kuanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Dar es Salaam na kule Jimbo la Ukonga pamoja na fedha hizi za TARURA zilizoletwa na Mheshimiwa Rais, Wabunge wengi hapa alivyotambulishwa Engineer Seif wamepiga makofi kutokana na fedha zile kupokelewa kwenye majimbo karibia yote nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuiombe sana Serikali barabara nyingi za Dar es Salaam kile kigezo cha traffic density, cha wingi wa magari yanayotumia barabara kimezidi yale magari 400 ya kujenga barabara kwa kiwango cha changarawe na kiukubwa ni kujenga barabara kwa kiwango cha lami. Barabara za Pugu - Majohe, barabara za Banana - Kitunda - Kivule tunategemea kwenye mradi huu wa DMDP tukipata fedha zitajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la barabara niombe mambo mawili; jambo la kwanza niiombe sana Serikali inapogawa fedha hizi basi vigezo vya kitaalam vya wenzetu vya TARURA vizingatiwe. Majimbo mengi yanatofautiana urefu wa kilometa za barabara, majimbo mengi yanatofautiana changamoto za ujenzi wa vivuko na madaraja. Nikuombe radhi hata humu Bungeni kwako ikitokea unagawa huduma yoyote ya mpango ya uzazi salama hauwezi Bi. Asha Mshua ukamuweka kundi moja na Ng’wasi Kamani, lazima utaweka kwa vigezo vyao na umri wao kutokana na hali halisi ya mazingira ya uzazi salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana kwenye mgao wa fedha hizi ombi la pili na wenzetu wa Zanzibar kwa mahusiano mazuri ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mnapogawa fedha hizi za barabara, basi kama tulivyofanya kwenye fedha za UVIKO na wenzetu wa majimbo ya Zanzibar nao muangalie jinsi ya kuweza kuwafikishia fedha za barabara ili kuwe na usawa wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba nizungumzie system za structures za Serikali za Mitaa, leo hapa tumeombwa zaidi ya trilioni 4.6 kama mishahara kwenye Serikali za Mitaa kwa jumla ya watumishi zaidi 319,000, tumeombwa fedha za maendeleo zaidi ya shilingi trilioni 3.26 ambazo zinaenda kutekelezwa kwenye Serikali za Mitaa. Lakini Serikali za Mitaa zimeundwa kwa mujibu wa Katiba, zinapata mamlaka yake kwenye Ibara ya sita, Ibara ya nane, Ibara ya 145 na Ibara ya 146 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wananchi wa Tanzania wenyewe ndiyo wameamua kwenda kutengeneza Serikali za kusimamia maendeleo yao. Fedha hizi zinaenda kule chini kuna Wenyeviti wa Vijiji, kuna Wenyeviti wa Mitaa, kuna Waheshimiwa Madiwani, tujiulize swali moja la msingi je, mifumo na miundo ya Halmashauri hizi inawapa mamlaka ya kutosha ya kusimamia uwezo wa miradi hii ya maendeleo? Halmashauri hizi zinawezeshwa na watendaji hawa kwenda kusimamia watumishi hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi kubwa inapaswa kufanyika, kazi ya kwanza kwenye miundo. Muundo wa Halmashauri zetu tukitoka hapo nje getini ukamtafuta Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa kama ana ufahamu wa bajeti hii inayosomwa na Waziri, nadhani majibu yake utayapata. Kuna kazi kubwa ya kurekebisha muundo wa Halmashauri, ili Waheshimiwa Madiwani wapate fursa ya kujadili bajeti hizi kwa kina kabla hazijafika hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwenye Halmashauri imekuwa ni desturi ya bajeti hizi kupita kwa kasi na kuwa na haraka ya kupita yale malengo ya Regional Secretariat na kuleta Bungeni.

Mhshimiwa Naibu Spika, lakini la pili; je, Wenyeviti wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji; je, Waheshimiwa Madiwani wanapata mafunzo ya kutosha ya kuweza kusimamia rasilimali fedha na rasilimali watu kule kwenye Halmashauri zetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la tatu niipongeze Serikali toka mwaka fedha uliopita imeanza kulipa posho za Madiwani. Lakini je, posho hizi zinatosha? Je, posho za Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji zinatosha? Hivi kweli Mwenyekiti wa Mtaa analipwa posho ya shilingi 100,000 kwa mwezi, ataacha kuwa- charge wananchi gharama za kuandika barua ofisini? Ataweza kweli kusimamia maendeleo kwenye eneo lake?

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme ifike wakati Serikali itengeneze muundo mzuri wa kuwawezesha kimuundo, kimafunzo, lakini kimaslahi viongozi wetu hawa wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji na Waheshimiwa Madiwani waweze kusimamia majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni Halmshauri zenyewe Serikali kuzitendea haki. Mwaka 2019/2020 kodi ya majengo (property tax) ilikuwa inakusanywa na Halmashauri zetu; na pale Halmashauri nyingi za Dar es Salaam tulikusanya shilingi bilioni tisa, lakini mwaka 2021zilipelekwa TRA. Fedha hizi hazikukusanywa wala hazikuletwa kwenye Halmashauri kuja kutekeleza majukumu yetu. Mwaka 2021/2022 zimepelekwa kwenye LUKU, sijui hii mwaka 2022/2023 mtazileta wapi? Niiombe sana Serikali tuziwezeshe Halmashauri zetu, tuzipe mamlaka ya kukusanya mapato yake, zitengenezewe malengo na zisimamiwe kuweza kutekeleza majukumu kwa wananchi wake. Hata hao Wenyeviti wa Mitaa, Wenyeviti wa Vijiji, Waheshimiwa Madiwani, wawekewe malengo ya kukusanya mapato, kuwe na sera ya retention ili waweze kuendesha shughuli zao kwenye ofisi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Mtaa inapokuwa na retention ya kodi ya majengo haitam-charge mwananchi barua ya dhamana kulipia kwenda kumtoa ndugu yake aliyekuwa na matatizo mahakamani. Watakuwa na uwezo wa kujiendesha, kutoa mafunzo kwa wananchi wao, hata kusimamia vikundi vya kina mama na vijana na walemavu wanaopata mikopo ya Halmashauri hata kuwaandikia katiba, kuwasajilia vikundi; na huu uwezeshaji wa wananchi utafika kwenye maeneo ya mitaa, vijiji na vitongoji na Waheshimiwa Madiwani leo watakuwa na uwezo wa kusimamia halmashauri zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuheshimi muda na kwa wachangiaji waliopo leo, naomba niseme naunga mkono hoja iliyowekwa mezani na Waziri wa Nchi, naomba kuwasilisha. (Makofi)