Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na kuhudhuria katika Bunge hili la Bajeti. Pia, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, jinsi anavyosimamia shughuli za maendeleo ya nchi hii hususani Wizara hii ya TAMISEMI kwa sababu iko katika Ofisi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichukue nafasi hii nimpongeze Waziri Innocent Bashungwa na wasaidizi wake Mheshimiwa Silinde na Mheshimiwa Dugange, Katibu Mkuu Profesa Shemdoe na Manaibu wake wawili; kwa jinsi wanavyochapa kazi kuhakikisha kwamba shughuli za maendeleo katika nchi hii zinaendelea. Vile vile niwapongeze sana kwa kuandaa taarifa ya bajeti ya mwaka 2022/2023. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla niipongeze Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, jinsi ilivyotoa fedha nyingi kwa miradi mbalimbali ya maendeleo katika Majimbo yetu na katika nchi yetu kwa ujumla. Naomba nianze kuchangia upande wa TARURA. Kwa upande wa TARURA kwanza niishukuru Serikali kwa kutoa fedha za nyongeza shilingi bilioni moja kwa miradi ya utengenezaji wa barabara katika Jimbo langu la Mbinga Mjini. Pia nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali kupitia Mkurugenzi Mkuu wa TARURA kwa kutoa gari aina ya Landcruiser mpya hivi karibuni, ambayo imesaidia sana wahandasi kuzunguka katika maeneo ya Jimbo la Mbinga Mjini na kufuatilia maeneo mbalimbali ambayo barabara zina shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hotuba ya Waziri imeeleza kwamba TARURA inasimamia mtandao wa barabara wenye kilomita 144,229. Katika kilomita hizo kilomita 2,473 ni kiwango cha lami, kilomita 30,756 ni kiwango cha changarawe, lakini kilomita 111,199 ni udongo. Mimi binafsi nataka nichangie hasa kwenye barabara zinazotengenezwa kwa kutumia udongo. Katika Jimbo langu kuna Barabara ya Mbinga – Kitanda – Masimeli – Miembeni, lakini kuna Barabara nyingine ya Mbinga – Kikolo – Kiungu na Barabara nyingine ya Mbinga – Magamao – Mpepai – Mto Lumeme. Barabara hizi zote zinatengenezwa kwa kutumia udongo. Maeneo ya Jimbo la Mbinga haya maeneo niliyoyatamka ni maeneo ambayo yapo kwenye miteremko, kiasi kwamba kama barabara inatengenezwa kwa kutumia udongo ina maana kwamba kipindi cha mvua barabara ile yote inaharibika; na wananchi hawawezi kupita katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyojua kwamba Serikali inapeleka miradi mbalimbali katika maeneo ya Kata hizo ni kwamba hasa kipindi kile cha mvua ujenzi wa miradi mbalimbali pamoja na kutengeneza barabara hizo, inakuwa ni ngumu kwa sababu tayari mvua zinakuwa zimeharibu miundombinu, kwa hiyo inakuwa ni shida. Ushauri wangu hapa naiomba Serikali kwa maeneo hayo ambayo yana hali ya kijiografia tofauti, barabara zake zingekuwa zinatengenezwa angalau kwa kutumia changarawe na kwa barabara hizo zinazotengenezwa, Serikali izingatie kujenga mifereji katika maeneo hayo ili kulinda uharibifu wa barabara hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya pili ni kwenye suala la afya. Kwenye upande wa afya naipongeza Serikali kwa kutoa fedha kwa ajili ya kujenga zahanati kwenye vijiji mbalimbali pamoja na vituo vya afya. Lakini changamoto iliyopo katika Jimbo la Mbinga kuna changamoto ya uchakavu wa majengo ya hospitali ya wilaya. Hospitali ya Wilaya ya Jimbo la Mbinga Mjini inahudumia takribani Kata 13 mpaka Kata 14, lakini hospitali hiyo ilijengwa mwaka 1970 mpaka sasa hivi majengo yale yamechakaa na ipo katika hali mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kabisa Waziri atakapohitimisha aniambie kwamba ni lini atasimamia kuhakikisha kwamba majengo ya hospitali ile yanajengwa upya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)