Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kuhusu mchango huu ambao ni maoni ya Mpango wa Bajeti ya Serikali. Kwanza niseme jambo mmoja, tangu juzi Wabunge wamejadili humu ndani mambo mbali mbali lakini mmoja kubwa ambalo Wabunge wengi tumejiuliza ndani ya Bunge lako Tukufu ni kwamba tunayo maji ya kutosha, tunayo ardhi ya kutosha, tunao watu, Wabunge wanasema, kwanini mambo hayaendi mbele? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, aliwahi kusema wakati fulani, na pengine hilo huwenda likawa ndilo jibu. Alisema kuna msemo Wakwere wanasema ‘zilongwa mbali zitendwa mbali’; yaani yanayosemwa na yanayokwenda kutekelezwa ni tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu wa Mheshimiwa Waziri wa Fedha ukiusoma ni mpango mzuri sana, na hata ukisoma takwimu ni takwimu nzuri sana; lakini utajiuliza ni kwa nini kila mwaka tukija hapa ndani tunarudia mambo yale yale ndiyo maana jibu lake likawa zilongwa mbali zitendwa mbali. Ukitazama michango ya Wabunge, wamechangia maeneo mazuri sana kwenye kuboresha mpango huu. Wametoa maoni mengi sana kwenye Bunge lako Tukufu, lakini unaweza kuja kushangaa tukija mwakani hapa, kwenye mpango wenyewe ukaona hakuna hata moja ambalo wenzetu wa Wizara wameyaweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe wenzangu Waheshimiwa Wabunge na Mheshimiwa Spika utuongoze Bunge lako, tulioyasema humu ndani ya Bunge, tunatamani kuyaona kwenye mpango wenyewe. Tunaolala na wagonjwa ni sisi, ndio tunaojua wanapoumwa. Sisi ni Wabunge tunajua shida za wananchi wetu, tuwaombe sana wataalam watusikilize, watusikilize na waamini kwamba tunayoyasema ndiyo matatizo ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hasa nianze kwenye kilimo, jambo la kilimo tangu wakati wa Mwalimu Nyerere, tumesema kilimo ni siasa, kilimo cha kufa na kupona na kadhalika, lakini miaka yote hii kilimo kimekuwa kinasuasua. Nitumie nafasi hii kwa mara ya kwanza kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ambaye yeye ameamua kuondoka kwenye kauli ya zilongwa mbali zitendwa mbali ameamua kufanya kwa vitendo kwa kuongeza bajeti ya kilimo kuanzia bilioni 294 hadi bilioni 959, zaidi ya zaidi ya mara tatu. Rais ana dhamira njema ameamua kufanya kwa vitendo, lakini nimwombe sana Waziri wa Kilimo na hili nasema na Bunge liweke Kumbukumbu. Tumemuongezea Waziri wa Kilimo fedha kwa ajili ya mbolea, mbegu, ujuzi na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, nataka kuamini tutakuja mwakani hapa, tutakuwa na wakulima wengi ambao wamelima mazao yao lakini hakuna soko. Mwaka jana kabla ya kuongeza bajeti tulikuja hapa, tukaiomba Serikali itafute fedha za dharura kwenda kununua mahindi kwa wakulima. Namuomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, wameshauri Waheshimiwa Wabunge humu ndani, mpango mzuri unaokwenda nao, tusaidie kuweka mkakati wa kutafuta masoko kwa ajili ya mazao haya ya wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kule Lupembe wananchi wangu wamehamishwa sana kulima parachichi, tunavyozungumza wamelima parachichi wameuza zaidi ya miezi sita hawalipwi kwenye mazao yao, soko hakuna. Kwa hiyo naomba kabla hatujatengeneza crisis ya soko tujipange mapema, tuandae soko, wananchi wakilima mahindi au mazao watakwenda kuuza wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pili, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, nakuomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo Tusaidie kutuondolea watu wababishaji na wafanyabiashara uchwara kwenye kilimo. Sisi Lupembe kwa mfano tunalo zao la chai, zao ambalo ni kubwa sana kwenye nchi hii. Linaingiza fedha za kigeni na lina uwezo wa kutoa ajira nyingi sana kwa wananchi wetu. Linaweza kutoa ajira kwa mkulima mwenyewe kwa mzalishaji, watu wenye magari, wasafirishaji na kadhalika. Lakini zaidi ya miaka 20 wananchi wa zao la chai Lupembe wamezidi kuwa maskini, wanalia na Serikali kila siku wanaomba kiwanda chao kirudi kifanye kazi sababu hakifanyi kazi. Tunaongea habari ya ajira hapa, mtapataje ajira?

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, wananchi wa Lupembe wamelia kilio kama mamba majini machozi yao yanakwenda na maji. Naomba wapatie matumaini wananchi wangu wa Lupembe, kile kiwanda cha Lupembe Tea factory Kirudishwe kifanye kazi na mwekezaji aliopo pale tuondolee kama ni mzigo, atoke pale, wananchi wangu wapate ajira na Serikali ipate fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni kuhusu…

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Edwin Ennoy Swalle kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa Kilimo.

T A A R I F A

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa tu taarifa Mheshimiwa Mbunge wa Lupembe na wananchi wake, kwamba Serikali imeshachukua hatua dhidi ya muwekezaji wa kiwanda cha Lupembe Tea Company Dhow Merchantile, na sasa Bodi ya Chai imeshamuandikia notice ya kumfutia leseni kwa sababu makubaliano yote aliyoingia na Serikali ameamua kutokuyafuata. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Swalle, unaipokea taarifa hiyo.

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili kwa niaba ya Wananchi wa Lupembe. Ninachoomba kauli hii ya Mheshimiwa Waziri isiwe zilongwa mbali zitendwa mbali. Nakushukuru sana Mheshimiwa Bashe kwa jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ni kuhusu jambo la mazingira. Nimesoma kwenye mpango wa Serikali, jambo la mazingira limesemwa kama jambo la mzaha hivi. Jambo la mazingira; naishauri Serikali tusitegemee fedha za wahisani tu, tuanzishe mpango maalum angalau kwenye halmashauri zetu waanze kutenga fedha kwa ajili ya kutunza vyanzo vya maji. Hata hapa Dodoma hali ya hewa imekuwa ikibadilika siku hadi siku, na wananchi yetu wanaendelea kuongezeka, tusipoweka mkakati wa muda mrefu wa kutunza mazingira, wakutunza maji, suluhu ya muda mfupi ya kuhamisha wananchi kwenye mabonde haiwezi kusaidia. Suluhu ya kudumu ni kutunza mazingira, tuwashirikishe wananchi wapande miti, watunze vyanzo vya maji wawe sehemu ya kuhifadhi mazingira yetu. Tukifanya hivyo, tutakuwa tumesaidia nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajenga Bwawa la Mwalimu Nyerere pale leo, linategemea maji, Mikoa ya Kusini ndio mwanzo wa maji haya. Tumeingiza trilioni sita pale lakini mpango wa Serikali wa kuhifadhi vyanzo vya maji kwa kutumia fedha za ndani kwenye halmashauri upo wapi? Juzi pale kwangu Mtwango wananchi wangu wamelima kwenye maeneo ya mabonde, wamefyekewa mazao yote pale, lakini kufyeka mazao haiwezi kuwa suluhu ya kuhifadhi maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kuwa na mpango wa Serikali wa kukwamua utunzaji wa mazingira na vyanzo vya maji. Napendekeza kama itakuwa jambo jema, Serikali ikiona inafaa, waziagize halmashauri, kwa kuwa mmeagiza kutoa asilimia kumi kwa ajili ya wanawake, vijana na wenye ulemavu, agizeni halmashauri watenge hata asilimia mbili kwa ajili ya fedha za kuhifadhi mazingira na kutunza vyanzo vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.