Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Bupe Nelson Mwakang'ata

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru sana kwa kunipa nafasi iliniweze kuchangia katika hoja hii muhimu ya Waziri Mkuu. Kwanza kabisa nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na kutupa kibali cha kuweza kusimama katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri Mkuu kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya, lakini kipekee nimpongeze sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Samia Suluhu kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya. Kwa kweli Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya na kibali ili kuwatumikia Watanzania vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuipongeza nakuishukuru Serikali kwa mambo mazuri ambayo wameendelea kufanya. Sisi wanawake tunashukuru sana kwa kitendo cha kutujali kwa kutupa asilimia 10 ya wanawake, watu wenye ulemavu na vijana, kwa kweli tunashukuru sana, hiyo asilimia 10 imefaidisha sana, ikiwemo na sisi wanawake wa Mkoa wa Rukwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuipongeza Serikali tumeona madarasa mazuri kabisa ya kisasa, watoto wetu wanasoma bure, tunaishukuru sana Serikali. Haikuishia hapo tu tumezunguka kukagua miradi ya maendeleo miradi, inakwenda vizuri, miradi mikubwa na midogo inaendelea, kwa kweli kazi ni nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuipongeza Serikali na kuishukuru kwa suala zima la hotuba ya Rais aliyohutubia siku ya tarehe 4 Aprili, ambayo iligusa moja kwa moja kwenye suala zima la kilimo. Tunajua kilimo ndio ilikuwa ndio kilio kikubwa sana kwa wananchi wa Tanzania, lakini ile hotuba inakwenda kuwafungua wakulima kuwapa ahueni, inakwenda kuwafanya walime kilimo cha kisasa, lakini chini ya Mheshimiwa Waziri wa Kilimo ambaye kaka yetu tunamwamini sana, kwa hiyo tunaishiwa hoja za kusema kwa sababu tayari ameonyesha mwelekeo wa kwenda kumsaidia mkulima. Ahsante sana Serikali, tunamtia moyo Mheshimiwa Waziri kwenye suala zima la kilimo, akaze buti tuko nyuma yake, aendelee kuwa ngangari, ahsante sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi sasa niinge kwenye changamoto za Mkoa wangu wa Rukwa. Nianze kwenye changamoto ambayo inawasibu sana wana Rukwa kiasi kwamba wamenituma nije niseme mbele ya Waziri Mkuu. Kwa kweli tunashukuru sana Serikali imeweza kutujengea stendi mpya ya kisasa ambayo iko mbali kidogo na Mji wa Sumbawanga Mjini. Pamoja na mafanikio hayo kutujengea stendi mpya, stendi hiyo imekuwa na machungu ndani yake kwa sababu wananchi wa Mkoa wa Rukwa wanapata mateso makubwa sana pale ambapo Serikali imepiga marufuku wananchi wale kupanda magari wakiwa Mjini Sumbawanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, magari yamepigwa marufuku kushusha au kupandisha pale Mjini Sumbawanga. Kwa hiyo adha hii imewafanywa wananchi wa Mkoa wa Rukwa hasa Sumbawanga Mjini wanapata mateso makubwa sana. Tunaomba Serikali pamoja na kwamba imejenga stendi mpya ya nzuri mpya ya kisasa hiyo stendi iko mbali na Sumbawanga Mjini, kwa hiyo tunaomba zitumike stendi zote mbili wananchi wapandie stendi ya zamani ambayo iko mjini, lakini pia wapandie na ile stendi mpya, zitumike stendi zote mbili, kuliko sasa hivi wananchi wanapata adha kubwa sana wanatumia usafiri kutoka pale mjini kwenda kufuata stendi ambayo iko mbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule unakuta wananchi wanaamka asubuhi saa 10 kufuata stendi iliko mbali, ni gharama kubwa, lakini pia magari yanayotoka mikoani au wilayani yanaishia huko nje ya mji, kwa hiyo inakuwa ni adha kubwa sana. Tunaomba leo hii ningechangia kwenye wizara husika ningeweza kushika shilingi ya Waziri mhusika wa hiyo, lakini kwa vile nimechangia kwenye Hotuba ya Waziri Mkuu namheshimu sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu amekuwa akifanya kazi nzuri kazi kubwa kwa hiyo siwezi kushika shilingi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Naomba atakapokuja kuhitimisha hoja yake hili suala la kutumia stendi zote mbili, basi atoe neno moja tu ili wananchi wa Mkoa wa Rukwa na wananchi wanaoishi Sumbawanga Mjini waweze kupona roho zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kwenye changamoto za Mkoa wangu wa Rukwa. Tuna changamoto ya maji, lakini naishauri Serikali, suluhisho kubwa la tatizo la maji katika Mkoa wa Rukwa, tunaomba tuna chanzo ambacho kinaweza kuwa ni suluhisho la kudumu, chanzo cha kutoa maji kwenye Ziwa Tanganyika na kuleta kwenye Wilaya zote za Mkoa wa Rukwa. Hiki ni chanzo ambacho hakiwezi kuleta tena shida, tunaomba kama ikiwezekana, basi Serikali iweze kutoa maji Ziwa Tanganyika na kuleta kwenye Mkoa wa Rukwa kwa ujumla na mikoa mingine ya pembezoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine, tunaomba barabara narudia tena, nimewahi kuleta hoja hii hapa barabara ya kutoka Tunduma mpaka Sumbawanga Mjini. Barabara ile nilisema ina matuta mengi makubwa sana, matuta yale yaliweza kusababisha viuno vya wanaume wa Mkoa wa Rukwa kutokufanya kazi ipasavyo, sasa naleta tena hoja hii naomba sana, Serikali inapata ugumu gani wa kutoa yale matuta? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana yale matuta yanatuletea matatizo makubwa sana, hata kwenye magari yanaharibika, ile barabara tunaitegemea kwa uchumi wa Mkoa wa Rukwa, matuta yamekuwa ni kitu ambacho kinatuletea matatizo. Rais hayati aliyekuwepo…

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa tu Mheshimiwa anayezungumza hivi sasa hoja ya matuta na viuno wanaume wa Mpanda wamethibitisha wanalalamika sana humu ndani ya hili jingo. Nakushukuru sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Bupe, taarifa hiyo?

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa tena kwa mikono miwili. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameona tunavyopata tabu sana wanaume wa Mkoa wa Rukwa, kwa kweli ni shida nyumba nyingi zinavunjika chanzo ni matuta, matuta ni makubwa sana hata hayati Dkt. Magufuli alimwambia Waziri wakati ule alikuwa Waziri wa Mambo ya Uchukuzi, alimwambia matuta yale nakupa mwezi mmoja yatoke, lakini haikutosha hata Katibu wa Chama Cha Mapinduzi alipofanya ziara kuja Mkoa wa Rukwa alipata tabu mgongo siku hiyo hakulala. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, akawaa anawapa wiki mbili watoe hayo matuta, lakini mpaka leo hii imekuwa ni kimya. Tunaomba basi Serikali iweze kulitilia maanani suala hili matuta yale yaweze kuondolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, naomba kuhusiana na barabara inayotoka Kibaoni kwa Waziri Mkuu Mstaafu Mheshimiwa Pinda inayopita Muze, Kilemba, Kiriyamatundu inakuja kutokea...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)