Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia muda huu nami niweze kuchangia hoja ambayo ipo mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, nashukuru hoja ambayo ilitolewa na Waziri Mkuu. Zaidi namshukuru Waziri Mkuu kwa mkutano wake alioufanya Mkoani Kagera, Wilaya ya Karagwe kutoa suluhu na mweleko wa zao la Kahawa Mkoani Kagera. Nadhani tunakoelekea ni kuzuri, hasa sisi ambao tunatoka katika mikoa inayolima zao la kahawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nitajikita kwenye migogoro ya ardhi. Ninavyoongea leo kuna watu wamelala nje jana. Tuna Kampuni yetu ya ranchi kwa jina mashuhuri, NARCO. Kama kuna kitu ambacho wamefanikiwa Mkoa wa Kagera, ni kutengeneza migogoro mikubwa baina ya wakulima na wafugaji. Kwa kweli, NARCO ni mtambo wa kufyatua migogoro kuliko ufugaji ambayo ni kazi ya msingi waliopewa na sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kagera, hususani Wilaya ya Muleba, NARCO wana ranchi mbili. Wana ranchi Rutoro na Mwisa, lakini wamepata hizo ardhi katika Wilaya ya Muleba kwa njia ambayo mimi kama Mwanasheria sijui walipataje. Bahati nzuri Mheshimiwa Spika ni Mwanasheria, na ninamwona Waziri wa Ardhi yupo hapa. Upatikanaji wa ardhi ya Mwisa ambayo ni mali ya Halmashauri ya Wilaya ya Muleba, hawa watu walivyoipata tuna mashaka makubwa. Nimepitia GN zote, tangu mwaka 1960 mpaka leo, nimetafuta GN ambayo inawapa uhalali NARCO kumiliki ardhi ya Mwisa, sijaipata. Tunapoongea, hawa watu wa NARCO wapo eneo la Mwisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la Mwisa katika Wilaya ya Muleba linahusisha Kata saba; tuna Kata za Kemitembe, Karambi, Kasharunga, Mbunda, Burungura, Ngenge na Rutoro. Ndani ya hizo Kata tunavyo Vijiji 12 na Vitongozi 19. Eneo lote hilo tunavyoongea wananchi hawajui kama leo watalala kwenye nyumba zao, hawajui kama kesho wataamka kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba tuna wasiwasi haya maeneo waliyapataje; kwa sababu haya maeneo ni mali ya Halmashauri ya Wilaya ya Muleba, ni maeneo ambayo yanakaliwa na vijiji; na vijiji vimepimwa tangu mwaka 1975 na vingine vimepimwa mwaka 2010, lakini hawa watu wanasema ni mali yao.

Mheshimiwa Spika, tunazo sheria za nchi hii; tunayo Sheria ya Vijiji (Land Village Act (No. 5) ya Mwaka 1999, lakini tulikuwa na Sheria ya Land Acquision Act; tunao utaratibu wa kutoa ardhi ya vijiji; tunao utaratibu kwamba Rais akihitaji eneo lolote atalitwaa, lakini kuna utaratibu wa kufanya hivyo. Waziri wa Ardhi ataandaa utaratibu ambao utakuwa gazetted, itatoka GN then hilo eneo litatwaliwa kwa matumizi mapana ambayo yana maslahi mapana kwa ajili ya uchumi na matumizi ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachoendelea, nimeangalia kote huko, hakuna kitu kinachofanyika au kilichofanyika. Watu wamekwenda wamepima maeneo ya Halmashauri, maeneo ya vijiji; na leo tunavyoongea, katika Vitongoji vya Kabwensana, Maigabili, NARCO wanahamisha watu kinyume cha sharia. Hawafuati Sheria ya Ardhi ya Vijiji, hawafuati sheria ya kuhamisha makaburi ya wapendwa wetu (Grave Remove Act (No. 9) ya Mwaka 1999, pia hawafuati mila na desturi za Wahaya. Wanakwenda pale, wanafukuza watu, wanawaambia ninyi mnahama, mnatoka hapa mnakwenda kule, hakuna notice iliyotolewa, Waziri wa Ardhi hajatoa notice kwa ajili ya kuhamisha makaburi kama ilivyo kwenye Graves Remove Act. Watu hawana amani, hakuna usalama kwenye eneo la Mwisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili nalisema, nashukuru umekalia Kiti, namwona Naibu wa Waziri ni Mwanasheria, naomba mtusaidie. Hatuwezi kuruhusu vitendo vya namna hii, wananchi wanateseka, wanafukuzwa kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, mbaya zaidi, naomba niliseme hili: lugha inayotumia kule, wanasema ninyi ni wavamizi. Mimi nashangaa! Mtanzania ambaye amezaliwa Tanzania, amekaa kwenye ardhi tangu mwaka 1975, leo NARCO anamwambia ni mvamizi. Tunalipeleka wapi Taifa? NARCO wanalo tatizo. Naomba, haya mambo yanayoendelea Kagera na Muleba, hayawezi kuishia Muleba tu, yatakwenda hata kwenye mikoa mingine tusipochukua hatua leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo hili lilianza mwaka 2016 kwenye upande wa Mwisa. Wakavamia eneo, wakaanza kupima. Tulipokwenda kwenye uchaguzi wakanyamaza. Tumemaliza uchaguzi, wameendelea na leo wapo wanaendelea. Nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Mifugo, ndugu yangu Mheshimiwa Ndaki Mashimba. Mwaka 2021 alikuja Wilaya ya Muleba kwa ajili ya kutafuta suluhu ya Mwisa, tukakaa tukaenda field, tukafanya mikutano na wananchi. Tukawaambia, vijiji ambavyo vimesajiliwa pamoja na vitongoji vyake, kwenye huu mradi wa Mwisa havitaguswa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumetoka kule, hawa NARCO walivyo wa ajabu, wakaanza kuwaambia wananchi msiwasikilize wanasiasa. Mimi nashangaa, kama wanasema msiwasikilize wanasiasa, Diwani ni Mwanasiasa, Mbunge ni Mwanasiasa, wewe Mheshimiwa Spika ni Mwanasiasa; na Bunge hili ni la Wanasiasa; ina maana hawatamsikiliza Diwani, hawamsikilizi Mbunge na hata Bunge lako hawatalisikia. Sasa wengine wa juu yake sitawasemea. Nashindwa kuelewa, hivi NARCO hawa, wanatoka Taifa gani? Wanatumikia Taifa gani? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, tulikubaliana pale, tukaja na kitu tunakiita community ambayo ina maazimio 16. Moja ya Azimio, ambalo ni Na. 16 tukasema Ardhi ya Vijiji pamoja na Vitongoji vyake visiguswe. Tumetoka, leo tunavyoongea, wapo kwenye Vitongoji, wanawahamisha watu kwa nguvu zote. Hapo ukumbuke, hawana GN ya kuwapa hiyo ardhi, kwenye makaburi ya watu wanaleta mifugo kulisha pale. Sasa mila zetu ziko wapi? Sheria ziko wapi? Labda kama Waziri amewapa hiyo ruhusa jana, lakini mpaka leo naongea, hakuna taarifa ya kuhamisha makaburi ya wananchi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)