Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nami niweze kuchangia taarifa hizi za Kamati juu ya ripoti ya CAG.

Mheshimiwa Spika, nimeona Wabunge wengi wamezungumza kwa uzito ambao unastahili kabisa juu ya madhaifu yaliopo kwenye ripoti hii ya ukaguzi na hasa hatua kutochukuliwa.

Mheshimiwa Spika, Ningependa nizungumzie eneo la utaratibu mrefu wa manunuzi ya umma. Nitatoa mfano mmoja; kwenye miradi ya maji au miradi ya barabara, unakuta ule mlolongo wa kufanya taratibu za manunuzi unapishana na Mwaka wa Fedha wa Serikali. Tarehe moja mwezi wa saba, mpaka tarehe 30 mwezi June mwaka unaofuatia Serikali inakuwa imepanga mipango yake, lakini unakuta sheria ya manunuzi inakwamisha baadhi ya michakato. Kwa mfano, halmashauri inaweza ikawa imepewa mradi wa maji au mradi wa barabara. Ni na mfano mmoja kule kwangu Mawengi kuna mradi wa maji ambao mikataba imesainiwa mwezi wa pili, lakini mpaka leo tunakwenda Disemba msamaha wa kodi kwenye ununuzi wa mabomba haujatoka. Kwa hiyo sasa tuangalie hizi sheria pia zisiwe zinatukwamisha katika kukamilisha miradi mbalimbali ya utendaji kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunakwenda kule tunawaeleza wananchi kwamba Serikali imeleta mradi huu hapa Mawengi lakini utaratibu wa kupata ule msamaha, kwa sababu sheria inataka miradi ya maji vile vifaa vipewe msamaha wa kodi. Tangu mwezi Februari mkataba unaingia mpaka Novemba exemption hiyo haijatoka. Kwenye miradi ya barabara pia hizo exemption zinachelewa sana. Kwa hiyo ukija kuangalia kwa mikoa yetu ile mvua zinaanza mwezi Oktoba mpaka mwezi Mei mwaka unaofuatia; kwa hiyo unakuta mkandarasi anakuwa na miezi miwili tu ya kufanya kazi. Anakuwa na mwezi Juni, Julai halafu hapo mwaka mwingine wa fedha unaanza. Kwa hiyo unakuta kuna kuwa na miradi mingi haikamiliki kutokana na sheria zetu kuwa na urasimu.

Mheshimiwa Spika, ningependa kuishauri sana Serikali, ili kupunguza baadhi ya hoja tuangalie pia sheria yetu ya manunuzi na kuweza kuifanyia marekebisho. Hii inapelekea sasa miradi mingi; nitatoa hapa mfano mwingine; katika Kamati ile ya Hesabu za Serikali za Mitaa tuliona kwamba kuna halmashauri 147 hazikupeleka fedha benki. Halmashauri 83 hazikuchangia bilioni saba kwenye vikundi vya wanawake, lakini kuna halmashauri 21 ambazo miradi yake ilikuwa imetelekezwa. Ukija kufuatilia sababu za kutelekeza hii miradi na hayo mengine yote niliyoyasema, Serikali imeweza kupoteza jumla ya shilingi bilioni 74.

Mheshimiwa Spika, vitu vingine tunaweza kuwalaumu watendaji lakini hata sheria zetu nazo; naona Mwanasheria Mkuu anasikiliza vizuri, hiyo imenipa moyo kidogo; kwa hiyo tuangalie sheria zetu za manunuzi yale maeneo ambayo yana urasimu, yanatuchelewesha kukamilisha kazi kwa wakati, yanatuchonganisha Serikali na wananchi, tutuyafanyie kazi ili wananchi waweze kuwa na miradi ambayo imekamilika.

Mheshimiwa Spika, vile vile kuna changamoto moja ya kutokuwa na watumishi wa kutosha kwenye halmashauri zetu. Kwa mfano, Serikali inaweza ikawa imepeleka fedha labda bilioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa jengo la halmashauri au majengo ya hospitali. Anayeandika makisio ya gharama za ujenzi unaweza kukuta sometimes hana sifa. Tumeona kwenye taarifa humu, mtu ni technician anaandaa BOQ ambayo inahitaji mtu mwenye weledi mkubwa kitaaluma. Nishukuru mwaka jana, tulishauri TAMISEMI waliweza kupata wahandisi, hata mimi pale Ludewa nililetewa Mhandisi angalau mambo yanaanza kwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo utakuta ile BOQ mtu anakisia materials ambayo fedha nyingi inatumika kununua materials ambayo hatimaye yatabaki na mradi haukamiliki. Pia, tuangalie hizi fedha tunazopoteza; namuona Waziri wa Utumishi ananisikiliza; ile tuanita wage bill, tuangalie hizi fedha ambazo zinapotea huku. Tukija kuzijumlisha zote, hiyo ni mshaara wa watumishi wengi sana. Tutaweza kutatua tatizo la vijana wetu ambao wanalalamika ajira kila siku. Ukiweka QS pale, suala la kuandaa BOQ mtu anakaa darasani anafundishwa na anafanya mazoezi ya kutosha, sio kila mmoja anaweza akaandaa hiyo BOQ.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utakuta Serikali inapeleka fedha nyingi kwenye halmashauri zetu, kwenye taasisi mbali mbali za umma; lakini kutokana kuwepo na baadhi ya watumishi wasio na weledi wanaopewa kazi hizo za kuandaa hayo hesabu tunapoteza fedha nyingi ambayo ingeweza kusaidia Watanzania wengi, ambapo sasa hivi kuna crisis ya ajira.

Mheshimiwa Spika, tukienda hata kwenye zile ofisi za mikoa (RS) nazo tuziangalie vizuri. Ukiona kuna mtumishi halmashauri msumbufu, mkorofi ana changamoto nyingi ndiyo sasa tuanamuhamishia tunampeleka RS. Kumbe RS ndiyo zina wajibu mzito, zina wajibu muhimu wa kusimamia halmashauri au Mkurugenzi muda wake umefika wa mwisho ametenguliwa uteuzi wake tunampeleka pale. Halafu hatuna watumishi wa kutosha kwenye hizi RS. Kwa hiyo tutawalaumu ma-RAS na Wakuu wa Mikoa, lakini hawana watumishi wa kutosha na wenye weledi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ningeiomba sana Serikali, ili kuokoa hizi fedha, kutoa thamani kwenye fedha hizi ambazo tunapeleka kwenye halmashauri na taasisi mbalimbali tungepeleka pia wataalamu wa kutosha na wenye weledi. Tunaweza tukaziongezea uwezo hizi RS ili ziweze kusimamia vizuri miradi.

Mheshimiwa Spika, vile vile Ofisi ya CAG ina jukumu la udhibiti. Kuna Waheshimiwa Wabunge wamesema hili jukumu la uthibiti bado halijaonekana sawa sawa, zaidi wanakuwa kama polisi kama TAKUKURU, ambao wakati mambo yamesharibika ndipo wanakwenda. Kumbe wana jukumu lingine la kuthibiti, kuzuia matatizo yasiweze kutokea. Tunaweza tukapunguza hoja nyingi sana eneo hili. Kwa hiyo ningeomba sana wale wataalam Ofisi ya CAG wajengewe uwezo ili wasiendelee kuwa tu kama mapolisi kwenda kukamata mwishoni watu wakishaharibu mambo.

Mheshimiwa Spika, wanaweza wakafanya ule ukaguzi wakati miradi bado inaendela kujengwa. Umepeleka fedha, msingi umejengwa waende wakague pale, watoe taarifa wataokoa fedha nyingi sana au wale wakaguzi wa ndani kule tukiwajengea uwezo mradi tusisubiri mpaka uishe mambo yaharibike zaidi, ndipo tunakwenda kukagua. Wangekuwa wanafanya ile real time audit, mradi unapokwa unaendelea mara kwa mara wanafanya ukaguzi na kutoa ripoti. Sasa mradi umekamilika mwaka huu CAG anakwenda mwakani tunapoteza sana fedha.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni muhimu kufanya ni kuwajengea uwezo Waheshimiwa Madiwani hasa Mameya na Wenyeviti wa halmashauri, nao wana nafasi kubwa ya kuweza kuzuia na kupunguza hizi hoja za ukaguzi, hasa kwenye halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, kila mwezi taarifa ya mapato na matumizi inapelekwa kwenye Kikako cha Kamati ya Fedha, uongozi na mipango. Kwa hiyo, laiti wangekuwa wajengewa uwezo kuweza kusoma zile taarifa vizuri, kuzichambua vizuri na ukaguzi wa miradi, Kamati ya Fedha inafanya mara kwa mara; wajengewe uwezo, kama hawajengewi uwezo maana yake watakuwa wanapelekwa kwenye miradi kwenda kutembea na ku- justify perdiem. Tukiwajengea uwezo wataweze kubaini kama dosari zipo eneo na kuweza kuchukua hatua kabla hata CAG hajaweza kwenda kuona hizo changamoto.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo unakuta tunapoteza fedha nyingi sana ambazo zingeweza kwenda kwenye maeneo mengine. Pia, nimeona baadhi ya Wabunge wamechangia kuhusiana na bilioni 68 ambazo zimelipwa kama penalty. Hii ni fedha nyingi sana ambazo tungeweza kuzuia zisilipwe kama penalty na zingekwenda kutengeneza hata kilometa 100 za lami. Sisi kule Ludewa tunahangaika sana kipande kile cha kutoka Mawengi mpaka kwenda Manda, Mlima Kimelembe tumekuwa tukihangaika na bilioni 6 tu. Fedha hizi wananchi wanavyosikia itawatia uchungu sana. Naungana na Wabunge wote ambao wamesema tuchukue hatua kuzuia haya mambo kabla hayajatokea.

Mheshimiwa Spika, pia hii tabia ya kuchelewa kulipa wakandarasi tuiangalie kwa umakini sana. Jana nilikuwa naongea na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, wale wakandarasi waliopewa jukumu la kusambaza mbolea yaani wanafanya kazi wengine wanachuki kwa sababu kuna malipo ambayo nao wanadai kwa muda mrefu. Sasa, unakuta wanapaki lori kwa wananchi, anawalazimisha wananchi wote siku hiyo ndiyo waende kuchukua mbolea. Wananchi wanafika pale asubuhi na mapema, lori linafika usiku, wanakaa na njaa. Hii imetokea jana pale Lugarao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuangalie kwa makini sana. Hawa, kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri, walitakiwa wawe na maghala wameyafungua. Kwa sababu muda wa mwananchi kupata fedha haufanani; si kwamba wananchi wote watakuwa na fedha siku mmoja au wakati mmoja. Mwananchi akishahangaika akiuza ulanzi wake na komoni akipata fedha ya mfuko mmoja aweze kuipta pale, na si kusubiri mpaka lori lije lipaki pale, wananchi wanateseka sana. Nashukuru jana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo aliweza kuchukua hatua; nampongeza sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wale wandarasi wana kinyongo kwa kuwa baadhi ya madai yao hawajaweza kulipwa.

Mheshimiwa Spika, Baada ya kusema hayo, nashukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja.