Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Vile vile kipekee sana namshukuru sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini na sasa amenipa kuisimamia Wizara ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi nampongeza tena Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, kwa kuchaguliwa kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Zungu kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizipongeze sana Kamati zote mbili; Kamati ya Katiba na Sheria na Kamati ya Utawala na Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, dakika moja tu. Waheshimiwa Wabunge, kwa mujibu wa Kanuni ya 34(5), ninaongeza muda bila kulihoji Bunge mpaka shughuli yetu itakapomalizika.

Endelea Mheshimiwa. (Makofi)

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza sana Wajumbe wa Kamati zote mbili; Kamati ya Katiba na Sheria na Kamati ya Utawala na Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa kazi nzuri wanazofanya. Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama na Mheshimiwa Chaurembo, pamoja na Wajumbe wote wa Kamati ambao kimsingi kwa upande wetu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Kamati ya Katiba na Sheria ikiongozwa na Mheshimiwa Mhagama, na wewe mwenyewe Makamu Mwenyekiti, mmekuwa watu wa karibu sana nasi, mnafanya kazi yetu iwe nyepesi, nanyi ni walezi wazuri. Kwa hakika mara zote hata wakati mwingine msipotuita tunajikuta tunawa-miss kwa sababu, tukifika kwenye Kamati yenu mnatusaidia sana katika kuhakikisha kwamba jukumu letu la Serikali linakwenda sawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yamesemwa mengi na Kamati. Kwa hakika kama ingekuwa hakuna ulazima wa kusema, wala hakukuwa na sababu ya kusema. Ilikuwa ni kusema amina, amina, amina, kwa sababu, tunatakiwa tu tuyachukue, tuyapokee na kwenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nimeona niguse tu maeneo machache, hasa moja tu la hatua kubwa ambayo imefikiwa na Mhimili wa Mahakama. Katika jukumu ambalo pia ninalo kama Waziri wa Katiba na Sheria ni pamoja na kusimamia mhimili huu. Unaposimamia mhimili ni kitu kikubwa sana, na hasa mhimili huu wa Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nilifahamishe Bunge lako Tukufu na wananchi wa Tanzania kwamba, mhimili huu umepiga hatua kubwa sana katika maendeleo ya kimtandao. Wamepiga hatua kubwa sana kiasi kwamba, sasa unaweza ukasajili kesi yako ukiwa nyumbani na simu yako na ukasajili shauri lako, lakini unaweza ukapata majibu yote ukiwa nyumbani wala usitoe hata hatua moja nje ya nyumba yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kuna uwazi mkubwa katika uendeshaji wa mashauri ambapo unaweza ukasikiliza shauri lako na wala usifike hata Mahakamani. Maendeleo haya ni makubwa na wakati mwingine tunasema tumeenda mbele kuliko hata uelewa wa wananchi wa kupokea huduma yenyewe hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameenda zaidi sana kwamba, yako malalamiko ya wananchi kuhusu kutokutendewa haki au rushwa na mambo mengine na mhimili huu wa Mahakama. Yenyewe hiyo wameweka ukurasa mahususi ambao unaweza ukaingia na ukaandika uko wapi? Umetendewa nini? Uki-post tu pale, mfumo mzima wa Mahakama, viongozi wote wanaona, kwamba kuna mahali, mfano Tandahimba au wapi, kuna hakimu au kuna mtu mwenye wajibu wa kutoa haki amefanya hiki na hiki. Ni hatua kubwa mno Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunafikiri ikitupendeza na nilikuwa naongea na Mkuu wa mhimili huu, Jaji Mkuu - Prof. Ibrahim Juma, pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Ole-Gabriel, wakasema ikipendeza na kama kutakuwa na nafasi tupate fursa ya kuja kutoa semina kwa Wabunge ili muone mifumo hii na system hizi zinavyofanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutakapopata muda na kama muda utaruhusu, basi Bunge lijalo tupate slot hata angalau siku moja tuje tufanye semina hiyo ili Wabunge mwelewe iwe rahisi kwenda kuwaeleza wananchi hatua kubwa ambayo imefanywa na mhimili huu wa Mahakama. Yamesemwa pia maeneo mengine ya namna ambavyo taasisi kama ya RITA, NIDA, Uhamiaji, PSSF, Bima ya Afya, Bodi ya Mikopo na mifumo mingine kwamba, iunganishwe ili iweze kusemana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie kwamba, maandalizi ni makubwa. Hatua kubwa imefikiwa na sasa mifumo hii inasema kwa pamoja na mawasiliano yapo na mahusiano yapo, yanaendelea kujengwa kwa mifumo zaidi ili kuhakikisha kwamba, mawasiliano ya vifo, usajili, utambuzi na vyote hivi vinapatikana katika mfumo wa pamoja katika Serikali.

Niwahakikishie tu kwamba, hatua hii imefikiwa na Wajumbe wa Kamati mmelisema hili sana na nirudie kusema, tunaendelea nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema, yote mliyoyasema hakuna hata moja ambalo tutafuta. Tunayachukua kama yalivyo na tunahakikisha kwamba tunayatekeleza. Tutakapokutana mwezi wa Tatu tutawapa mrejesho wa hatua tutakayokwenda na ninyi mtatushauri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)