Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye taarifa hizi za Kamati na niungane na Waheshimiwa Wabunge waliotangulia kwa kuanza kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita iliyo chini ya Mama Samia Suluhu Hassan, maana hata kule Jimboni kwangu Ludewa kila kona ambako wananchi wapo, kuna miradi ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, naye nimkumbushe kwamba ana ahadi na wananchi wa Ludewa na wanamsubiri sana kule. Ziara yake ameshaiahirisha mara nne, kwa hiyo, wananchi wameniomba sana niweze kumkumbusha, wana hamu naye sana, wanataka aende akashuhudie kazi nzuri ambazo Rais wetu amefanya ikiwemo daraja la Ruhuhu, barabara ya zege na mambo mengine lukuki. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika nakupongeza kwa kuchaguliwa. Nami binafsi nikiri kwamba nakufahamu tokea Law School ukiwa mwalimu wangu Cohort ya 12. Kwa kweli Mwenyezi Mungu amekupa karama nyingi, naamini hata Bunge hili litaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo machache nirudi sasa kwenye hoja mahususi ambapo ningependa kuanza kuchangia kwenye Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Nimemsikiliza RC wangu wa zamani wa Mkoa wa Njombe, Mheshimiwa Ole-Sendeka, amezungumzia hoja ya Ngorongoro ambayo vilevile imekuwa ikijadiliwa sana kwenye vyombo mbalimbali vya Habari. Wako ambao wanasema kwamba wananchi waendelee kuwepo vilevile kwa sababu ni aina ya pekee ya utalii; watu, mifugo na wanyama wa asili, lakini wapo ambao wanaona kwamba ongezeko la mifugo kama ng’ombe, kondoo, mbuzi na wanadamu inaharibu ekolojia ya eneo lile na wanyama wale walikwenda pale kwa sababu za kiasili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata tukisoma maandiko matakatifu tutaona kwamba Mwenyezi Mungu baada ya kuumba mbingu, ardhi, wanyama, ndege ndiyo akamuumba mwanadamu. Kwa hiyo, tuna jukumu vile vile la kutunza hizi maliasili. Ila hoja ya mahususi na ya msingi ni kwamba tunavyoshughulikia mambo haya kama alivyoongea Mheshimiwa Ole-Sendeka, tuweze kuzingatia haki za binadamu, kwamba Serikali inavyotekeleza wajibu wake wa kulinda hifadhi ile ambayo iko kwenye urithi wa dunia, Hifadhi ya Ngorongoro, ni sharti na ni muhimu sana kuheshimu haki za binadamu. Tunapowahamisha wale watu, lazima tuangalie sheria zinasemaje kuhusu haki za binadamu? Zikoje? Vile vile kuwe na ushirikishwaji wa hali ya juu.

Nimemuona Mheshimiwa amesisitiza zaidi ushirikishwaji kwa hiyo hoja zote ni za msingi lakini ile Hifadhi ya Ngorongoro ambayo ina sheria yake, Sura ya 284 na Kifungu cha 6 kama alivyokinukuu, kinaelezea majukumu ya ile mamlaka ya uhifadhi wa Ngorongoro. Kwa hiyo, mamlaka ile ilikuwa na majukumu ambayo imepewa na sheria na ilikuwa na wajibu wa kuyasimamia. Kwa hiyo, watu walikuwa wanaongezeka tunaangalia, lakini sasa tunavyotaka kuilinda ile Hifadhi tuzingatie haki za binadamu, lakini hoja ya ile hifadhi kuendelea kuwepo ni muhimu sana ikapewa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika kwenye Kamati yetu tuliona kwamba Serikali imewekeza fedha nyingi sana kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere na takribani shilingi trilioni
6.5 zimewekezwa pale na asilimia siyo chini ya 60 ya maji yanatokana na bonde la Mto Kilombero. Kwa hiyo, na kwenyewe ni muhimu sana Serikali ikachukua hatua za haraka pasipo kuathiri haki za binadamu. Wale wananchi wote ambao wanafanya shughuli zinazoathiri ustawi wa bonde hili la Mto Kilombero na kuathiri uwepo wa maji ya kutosha yatakayoenda kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere, kwa kweli ni vizuri Serikali ikachukua hatua za haraka bila kuathiri haki za binadamu. Ninavyosema haki za binadamu, nafikiri ni neno ambalo ni pana kidogo.

Mheshimiwa Spika, halikadhalika tukija kwenye masuala ya utalii, huku Nyanda za Juu Kusini kuna vivutio vingi sana vya utalii, kule Jimboni kwangu Ludewa, Ziwa Nyasa kuna samaki wa mapambo, kuna milima ya Livingstone, ingawa bahati mbaya kuna Kata nne pale hazifikiki kwa gari; Kata ya Lumbila, Kata ya Kilondo, Kata ya Makonde na Kata ya Lifuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika zile safu za milima ya Livingstone kuna nyani wale wakubwa, wazuri, ni kivutio kizuri cha utalii. Pia kuna miamba ile ya Ziwa Nyasa na Kitulo kule kwa Mheshimiwa Festo Sanga, Makete. Kwa hiyo, vivutio ilikuwa ni vizuri vikatambulika na Wizara hii ya Maliasili na kuweza kukuza utalii wa Nyanda za Juu Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halikadhalika kuna ngoma za asili. Mheshimiwa Naibu Waziri tulimpelekea ngoma moja ya Mganda ya Boma la Mtumbati, kulikuwa na tukio la watu wa Makete. Alivutiwa sana na ile ngoma, mavazi yao wanavaa kaptura nyeupe na shati jeupe. Ngoma ile kwa kweli ni kivutio kizuri sana na muhimu cha utalii. Pia kuna ngoma nyingine kama Ngwaya, Matuli; hata vyakula vya asili. Kwa hiyo, ni vizuri Wizara hii ikatambua vitu vile na kuviingia kwenye mradi wa regrow, itasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikirejea kwenye Wizara ya Ardhi, Wizara hii inafanya kazi kubwa sana na sasa hivi wamewekeza sana kwenye mifumo ya kielektroniki; Teknolojia Habari na Mawasiliano kuna mfumo unaitwa Landrent Management System, kuna mfumo unaitwa Molis na mifumo mingine mingi. Mifumo hii kwa kweli inasaidia sana katika kuongeza ufanisi. Isipokuwa Wizara hii inakabiliwa na upungufu mkubwa sana wa wafanyakazi. Takribani wafanyakazi 2,000 wanahitajika waongezeke. Kwa hiyo, Wizara hii iangaliwe kwa jicho la karibu ili isaidie kupunguza migogoro.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)