Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021

Hon. Christopher Olonyokie Ole-Sendeka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Simanjiro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi ya kwanza kukushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Nachukua nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Amiri Jeshi Mkuu na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, kwa jinsi anavyoliongoza Taifa letu kwa viwango ambavyo kila mtu anakiri na kazi yetu ni kuendelea kumwombea kwa Mwenyezi Mungu, ampe afya njema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kukupongeza wewe binafsi kwa kuchaguliwa kwa kura zote na Bunge hili la Jamhuri ya Muungano kuwa Spika wa Bunge letu. Hakika Mbeya imetupa mtu, hakika Magufuli alimwona mtu makini, hakika aliyekuteua kuingia kwenye Bunge la Katiba aliona mbali na leo Watanzania watashuhudia uwezo wako katika kipindi cha uongozi wako. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, nisiwe mwizi wa fadhila, niwapongeze Wabunge ambao wamepata dhamana ya kuaminiwa na Rais kwa nafasi mbalimbali; nampongeza Mheshimiwa Shangai kwa kuchaguliwa na wananchi wa Ngorongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze mchango wangu sasa kwanza kwa kuwashukuru waliowasilisha taarifa za Kamati zote mbili, lakini nianze na Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Mtakumbuka tumekuwa na mgogoro wa muda mrefu kati ya wananchi au watumiaji wa ardhi na Hifadhi zetu za Taifa kwa muda mrefu; na Rais wa Awamu ya Tano aliunda Kamati ya Makatibu Wakuu na Mawaziri na baada ya kazi kukamilika, alisema maamuzi yatatolewa.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alisema kazi inaendelea, alitekeleza uamuzi huo kwa kufanya uamuzi wa haraka na kwa muda mfupi sana aliweka historia ya kuwatuma Mawaziri wapatao nane kuzunguka nchi nzima kutoa maamuzi ya Serikali ya kilio cha muda mrefu cha wananchi wa maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, Mawaziri hawa wanane wakiongozwa na Mheshimiwa Lukuvi, wakati huo akiwa Waziri wa Ardhi, walifika Jimbo la Simanjiro kutokana na mgogoro uliokuwepo kati ya Kijiji cha Kimotoro kwa upande mmoja na Pori la Mkungunero Game Reserve kwa upande mwingine; na pia kushughulikia mgogoro uliokuwepo kwa Vijiji vya Wilaya ya Kiteto kwa maana ya Erikiushi, Bwawani na Katikati, lakini kushughulikia pia mgogoro ulioko kati ya Mkungunero na Jimbo la Kondoa Vijijini la Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji na maamuzi yale yalitangazwa na wananchi walipata faraja na hakika walimsifu sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kinachoshangaza mpaka sasa, baada ya maamuzi na maelekezo ya Rais ambayo yalikuja kutamkwa na Mawaziri, watendaji na wataalam walioambiwa wafanye kazi hiyo, mpaka sasa wameshindwa kukamilisha kazi hiyo kwa sababu wanazozijua wao wenyewe. Ombi langu kwa Waziri Mkuu na kwa Serikali, wale waliotumwa kufanya kazi hiyo wakamilishe haraka ili wananchi…

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Venant.

T A A R I F A

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, mchangiaji anaongea vizuri sana juu ya Mawaziri hawa, lakini nataka nimpe taarifa kwamba kweli walitumia fedha nyingi kuzunguka kuja kutatua migogoro hii, lakini cha ajabu wataalam waliachiwa hili jukumu la kusaidia kutatua migogoro hii, wenyewe wanasema wanahitaji maelekezo kutoka kwa wahusika kwa barua. Kwa hiyo nampa taarifa kuwa Serikali sasa ipeleke maelekezo kwa barua ili sasa migogoro hii iweze kwisha.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Christopher Ole-Sendeka.

MHE. CHRISTOPHER O. SENDEKA: Mheshimiwa Spika, napokea taarifa yake na ninaungana naye kuiomba Serikali ifuatilie kazi ambayo watendaji walipewa ya kuhakikisha kwamba wanamaliza mgogoro huu ili ahadi ya Rais iweze kuwa ni ya kweli kama alivyoahidi mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende sasa katika suala ambalo ninaliomba Bunge hili lijipe muda wa kuungana na Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii kupata muda wa kulitafakari, nalo ni suala la mgogoro uliopo katika maeneo mawili ya Wilaya ya Ngorongoro. Kwanza Tarafa ya Ngorongoro yenye kilometa za mraba 8,000 eneo ambalo kuna maisha mseto kati ya wanyamapori, binadamu na mifugo inayofugwa na binadamu ambayo imeanza mwaka 1959.

Mheshimiwa Spika, mgogoro mwingine ni katika eneo la kilometa 1,500 za Tarafa za Loliondo ambayo inatakiwa ifanywe kuwa ama Game Reserve au Game Control Area. Jambo hili ni vizuri sana Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania likaelewa, likapata muda wakati Serikali inafanya tathmini, Bunge lako likapeleka Kamati ya kuyajua mambo haya. Kwa sababu upotoshaji unaoendelea kufanywa na baadhi ya vyombo vya habari na upotoshaji unaofanywa na social media hakika hauwatendei haki wananchi wa Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba ninukuu maneno haya ya gazeti la Jamhuri la tarehe 1 mpaka 7 Februari, linasema hivi: “Loliondo na Ngorongoro kwa ujumla wake ni za Watanzania. Hivyo sote tuna wajibu wa kuona ikiendelea kuwepo ili iwe na manufaa kwa Watanzania na walimwengu wote. Haiwezekani kabila moja katika nchi likatae kutii mipango ya Serikali hasa ikizingatiwa kuwa kinachofanywa na dola kina manufaa makubwa kwa Umma na kwa nchi.” (Narudia), “haiwezekani kabila moja likatae kutii.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Spika, lugha hii siyo njema hata kidogo. Haiwezekani! Unaposema haiwezekani kabila moja; wanaosemwa hapa, walioko Loliondo na Ngorongoro ni kabila moja linaloitwa Wamasai. Wamasai hawa wamekuwa waungwana kwa uhifadhi. Kama kuna kabila lililoonesha uhifadhi bora na kuweza kuishi na wanyama katika eneo moja bila kuwadhuru ni Tarafa ya Ngorongoro katika Wilaya ya Ngorongoro ambalo wengi wa wananchi wanaoishi hapo ni Wamasai.

Mheshimiwa Spika, wananchi hao hao walitoa ardhi yote ya Serengeti, Tarangire, Ngorongoro na Lake Manyara. Leo unapozungumza kilometa za mraba 1,500 ambayo Mheshimiwa Waziri Pinda aliundia Tume na baada ya Tume yeye mwenyewe alikwenda; CCM iliunda Tume iliyoongozwa na Dkt. Mwigulu Nchemba, nami nilikuwa Mjumbe wake tukaleta taarifa. Waziri Mkuu wakati huo Mheshimiwa Mizengo Pinda akaenda Loliondo akatoa tamko la Serikali, juu ya msimamo wa Serikali kuhusu eneo la Loliondo na msimamo wa Serikali kuhusu eneo la Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, Wakati huo huo Rais wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, baada ya kelele kuendelea alisema hivi akiwa kwenye matibabu; na haya ni maneno yake naomba ninukuu kwa ruhusa yako. Haya ilikuwa ni tarehe 23 Novemba, 2014.

Mheshimiwa Spika, nami naomba ninukuu kwa sababu aliandika kwenye twitter yake kwa Kiingereza: “There has never been, nor will there ever be, any plan by the government of Tanzania to evict the Maasai people from their ancentral land.” Mwisho wa kunukuu. Haya ni maneno ya Rais wa Awamu ya Nne. Baada ya kelele za waandishi wa habari kutumia social media na kutumia magazeti yao kutuma ujumbe usio mzuri kwenye ulimwengu mzima.

Mheshimiwa Spika, hata leo naungana na Kamati, wanaposema mfumo wa matumizi bora ya ardhi, usimamizi hafifu ndiyo unapelekea tishio hili lililoko Ngorongoro. Nataka nikwambie, magazeti haya ambayo nilikuwa nakukuu ambayo ni mengi, ninayo hapa, yalikuwa ni matokeo ya semina iliyofanywa na Dkt. Fredy Manongi, Kamishna wa Uhifadhi wa Ngorongoro kwa kuwaita Wahariri wa Habari ili watoe picha wanayoitaka wao na huku wanasahau kwamba hata log yao Mamlaka ya Ngorongoro ina kichwa cha Faru, ina picha ya ng’ombe hapa, kuonyesha kwamba Ngorongoro ni kwa ajili ya wafugaji wa uhifadhi. Hata hivyo, anasahau section 6 ya sheria iliyoanzisha Mamlaka ya Ngorongoro inasema hivi, naomba ninukuu tena ili hawa wenzetu waelewe kwamba walioko Ngorongoro hawako kwa ajali. Inasema hivi: -

“The functions of the authority shall be to conserve and develop the natural resources of the conservation area;” ya pili, anazungumza: “to promote the tourism; na ya tatu: “to safeguard and promote the interest of Maasai citizens of the United Republic.” Hayo ndiyo malengo makuu matatu.

Mheshimiwa Spika, naomba niishie hapo kwa sababu ujumbe wenyewe umefika, lakini kwa kukuomba na wewe utupe muda, isaidie Kamati hiyo iende Ngorongoro, ikae na wananchi wa Loliondo na wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro. Serikali nayo iunde Tume yake, tutekeleze maelekezo ya Mheshimiwa Rais, amewaambia wasaidizi wake, nendeni mkakae na viongozi wa mila…

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Sendeka, dakika moja, malizia.

MHE. CHRISTOPHER O. SENDEKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa dakika moja.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ametoa maelekezo kwamba viongozi wa Serikali wakakae na viongozi wa Ngorongoro, wakae na viongozi wa mila wa Ngorongoro ili watafute ufumbuzi wa namna ya kuendelezwa kwa ufugaji na uhifadhi katika eneo la Ngorongoro. Ninachoomba Serikali isimamie maelekezo ya Rais kama alivyoelekeza.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuichangia hoja hii. (Makofi)