Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Tatu wa Bunge na Mkutano wa Nne wa Bunge pamoja na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa katika Mkutano wa Tatu wa Bunge na Mkutano wa Nne wa Bunge pamoja na Kanuni za Uvuvi za Mwaka 2009

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuwa mchangiaji wa pili kwenye taarifa hii ya Kamati ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuunga mkono taarifa nzuri ya Kamati ya Sheria Ndogo na niipongeze sana Kamati kwa kazi kubwa ambayo wameifanya ya uchambuzi wa Sheria 487.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili pia nimshukuru sana Mheshimiwa Spika, kwa kuipa muda wa kutosha Kamati ya Sheria Ndogo na hii inaashiria kwamba Ofisi ya Mheshimiwa Spika inatambua na kujali madhara ya Sheria Ndogo ambazo ndiyo zinatumiwa kwenye shughuli za kila siku za wananchi wetu wa Tanzania. Wakiwemo wale wavuvi na watu wa chini katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirejea kwenye taarifa ya Kamati kama ambavyo imesomwa na Mwenyekiti wa Kamati, ukitazama kwa ujumla unaweza ukapata picha kwamba katika uchambuzi ambao Kamati imefanya kumekuwa na kosa ambalo mara nyingi linafanywa na mamlaka za utunzi wa hizi Kanuni au Sheria Ndogo. Hii inapelekea kwamba mtazamo wa utunzi wa Kanuni hizi wakati fulani unaangalia kuwa na lengo la kukataza, lengo la kuzuia, lengo la kutoa adhabu na lengo la kukataza watu wasifanye shughuli mbalimbali za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ndiyo maana miongoni mwa Kanuni ambazo zimebainika kuwa na dosari ni Kanuni ya Wanyamapori na Uhifadhi kwenye Kifungu cha 24. Kanuni hii ambayo inahusu ajira za Wahifadhi Wanyamapori ilikuwa inataka mtu akiajiriwa kwenye Uhifadhi wa Wanyamapori asifanye shughuli nyingine yeyote ya kumuingizia kipato chake halali. Kanuni hii kama ingeachwa kama ilivyo tafsiri yake ni kwamba mtu anayefanya kazi ya ulinzi kwenye hifadhi hataweza kufanya hata shughuli zingine za kumuingizia kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya Kamati inakuwa je, kama asifanye shughuli yoyote ya kumuingizia kipato ina maana kwamba haruhusiwi kuwa na duka lake binafsi, ina maana kwamba haruhusiwi kuwa na shamba lake binafsi. Kwa hiyo, Kanuni hii ilikuwa haitoi taswira sawa sawa kwamba asifanye shughuli nyingine binafsi maana yake nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Kamati imeona hii dosari kwamba kwa mujibu wa Katiba yetu ukisoma kuanzia Ibara ya 12 hadi ya 30 ni wazi kwamba Watanzania wanayo haki ya kufanya kazi na wana haki ya kupata ujira. Kwa hiyo, ni maoni ya Kamati kwamba Kanuni hii ilikuwa na dosari hiyo kwa hiyo pamoja na kuzuia shughuli maalum ya ulinzi, lakini Mlinzi ana haki ya kufanya shughuli zingine za kumuingizia kipato kama raia wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo jambo lingine kwenye Kanuni ya Misitu inayohusu uzalishaji, usafirishaji na uuzaji wa mkaa mbadala. Waheshimiwa Wabunge wote mnajua dunia sasa hivi inatazama uhifadhi wa mazingira na siku za karibuni Mheshimiwa Rais alikuwa kwenye mkutano mkubwa duniani unaozungumza kuhifadhi mazingira, maana yake ni kwamba kuelekea kwenye kanuni za kutengeneza mkaa mbadala ni kitu muhimu cha kuhimiza wananchi wetu watengeneze mkaa mbadala badala ya kuharibu maliasili ya misitu kwa maana mkaa wa asili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kanuni hii ya Tisa ukitazama kwenye maudhui yake inatoa katazo au inatoa mamlaka kwa Mhifadhi wa Misitu kwamba anaweza kusitisha leseni ya mtu anayefanya kazi ya uzalishaji wa mkaa mbadala au usafirishaji au uuzaji na haitoi akisitisha hicho kibali, atasitisha kwa muda gani na haielezi atarudishiwa kwa namna gani akikidhi masharti ya kibali husika. Kwa hiyo, hii pia ilikuwa ni dosari kubwa tunadhani ni wakati sasa Kanuni zetu nyingi ziwe ni Kanuni za kuwezesha wananchi kufanya shughuli zao za maendeleo badala ya kukataza na kutoa adhabu peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho na la muhimu napenda pia kuishauri Serikali kwamba inapoendelea kutunga hizi Kanuni na Sheria Ndogo ndogo tuwe na mtazamo zaidi wa kutunga Sheria na Kanuni za kuwezesha shughuli za wananchi kuendelea badala ya kuwa na sheria ambazo kazi yake kubwa ni kukataza, kuzuia na kutoa adhabu peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Jenista Mhagama Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu kwamba hata Mawaziri walipokuja kwenye Kamati ya Sheria Ndogo wakati wote ilipobainika dosari ya kufanyia marekebisho walikuwa tayari na kutoa ushirikiano mkubwa sana kwa ajili ya ujenzi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)