Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango huu wa Maendeleo wa Taifa. Sisi tunatokea kwenye maeneo yanayozalisha kilimo. Katika eneo hili, kila Mbunge atawajibika kuelezea yale ambayo ni ya msingi kwa ajili ya wananchi ambao wanategemea sekta hii ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeuangalia Mpango, haujawa na suluhisho la kudumu na kutatua kero ya wakulima hapa nchini. Kilimo kinahitaji mambo ya msingi; la kwanza ni suala la umwagiliaji. Mungu alitujalia kwenye maeneo yetu, karibu kila sehemu ya nchi yetu inapata mvua za kutosha na tunapata maji mengi yanayoishia kwenda baharini bila kuwa na mfumo sahihi wa kuyavuna yale maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa na maendeleo ya sekta ya kilimo kama hatujawa na mipango thabiti ya umwagiliaji. Umwagiliaji pekee ndiyo utakaofanya kilimo kiweze kukua hapa nchini. Kwenye Mpango hatujaona mipango ambayo ipo ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni suala la ruzuku ya mbolea. Bila ya kuweka ruzuku ya mbolea hatutawasaidia wananchi. Bei za pembejeo ni kubwa kiasi kwamba uwezo wa kumudu kununua hizo pembejeo hawatakuwa nao. Tunaishauri Serikali iangalie umuhimu sasa wa kutenga fedha kwa ajili ya kuweka ruzuku ya mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada zinazofanywa na wakulima binafsi, bado wana kero nyingine kubwa sana ya ukosefu wa masoko. Eneo hili lazima Serikali waongeze fedha hasa za kununua mazao ya wakulima. Tunaomba Serikali iangalie uwezekano wa kuwawezesha wananchi waweze kulifikia soko la nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wa Mikoa ya Mbeya, Songwe, Rukwa, Katavi na Kigoma ni maeneo ambayo yana eneo kubwa sana la mwambao la Ziwa Tanganyika, na wanaweza wakapata soko kupitia nchi ya DRC Congo. Serikali haijatafuta soko hili vizuri na kuwawezesha wananchi wakapata nafasi ya kulitumia hili soko. Tunaishukuru Serikali imejenga bandari kule eneo la Karema, bandari ya Kasanga na kule Kigoma, lakini bado tunahitaji barabara ambazo zitaunganisha maeneo haya yaliyo na bandari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali imejenga barabara eneo la Kasanga kutoka Sumbawanga kwenda Kasanga, lakini tuna barabara ya kutoka Mpanda Mjini kwenda eneo la Karema ambako kunajengwa bandari. Eneo hili ni muhimu sana, ni vyema ijengwe barabara ambayo itasaidia kujenga mazingira ya soko lililoko nchi ya DRC Congo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia nchi jirani ya Zambia ina vikwazo vikubwa sana kwenye maeneo ya usafirishaji. Kwa hiyo, tukitengeneza maeneo ambayo yanaweza yakawasaidia wananchi kwenye maeneo hayo, yatasaidia sana masoko kuwa mazuri na yatavutia na kuhakikisha soko la DRC Congo tunalishika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali iangalie maeneo mengine na kuongeza fedha za NFRA kwa ajili ya kununua mazao ya wakulima. Eneo hili ni muhimu sana ili tuweze kuwasaidia wakulima wawe na uhakika wa masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta nyengine ambayo tunahitaji kuishauri Serikali ni sekta ya uvuvi. Kwenye eneo la uvuvi bado Serikali haijapeleka fedha wala kuwasaidia wananchi. Tukiwasaidia wakulima, wavuvi na wafugaji, ni maeneo ambayo yanaweza yakasaidia kukua kwa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashauri kwenye uvuvi hasa nizungumzie Ziwa Tanganyika. Sisi wa Ziwa Tanganyika tunapakana na nchi ya Burundi, Kongo na Zambia. Wanufaikaji wakubwa wa hili ziwa ni nchi ya Congo DRC, Burundi na Zambia. Sisi ambao tuna eneo kubwa la Ziwa Tanganyika, sheria tulizoziweka sisi wenyewe, siyo rafiki kwa wavuvi wa wetu. Nichukulie mfano tu kwamba mvuvi wa Tanzania haruhusiwi kuvua mazao yake mchana, lakini nchi zinazotuzunguka wao wanavua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia, karibu mazao yote ya Ziwa Tanganyika, asilimia kubwa wasafirishaji wa mazao hayo ni nchi jirani ya DRC Congo ndiyo wanaouza au Zambia. Kwa hiyo, naomba zile sheria ambazo zinawabana hasa wavuvi wanaokatazwa kuvuna mazao kwenye kipindi cha mchana, waruhusiwe wawe wanavua mazao hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie eneo lingine ambalo ni katika kulisaidia Shirika la Ndege la ATCL. Shirika hili kama Serikali hawataweka dhamira ya kulisaidia, halitasimama. Shirika hili lina madeni makubwa, linadaiwa karibu shilingi bilioni 215 ambazo ni fedha zinazodaiwa za kipindi hicho cha nyuma shirika lilipokuwa limekufa. Mzigo huu bado shirika hili linao. Kwa hiyo, tunaomba Serikali ichukue hili deni ili tuweze kulisaidia hili shirika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utapanda ndege kutoka hapa Dodoma kwenda Dar es Salaam, nauli ya ndege kutoka hapa kwenda Dar es Salaam ni sawa na ya kwenda Dubai, kitu ambacho ni kigumu kwa Mtanzania wa kawaida kuweza kumudu kusafiri. Naomba hili Serikali waliangalie…

MWENYEKITI: Una maana gani Mheshimiwa Mwenyekiti?

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nauli ya ndege kutoka Dodoma, ukipanda ndege ya Shirika la Ndege la ATCL kwenda Dar es Salaam, nauli yake ni kati ya shilingi 500,000 mpaka shilingi 600,000 na mpaka wakati fulani inafika shilingi 700,000. Nauli ya kutoka Dar es Salaam kwenda Dubai ni shilingi 500,000 mpaka shilingi 600,000. Sasa haiwezekani kwamba shirika hili utaweza kulibeba; na linakuwa na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Naona ni kengele ya pili.

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Ndiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba Serikali ilisaidie shirika hili kulipunguzia madeni makubwa ambayo yapo ambayo kimsingi tukilipunguzia litaweza kumudu kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)