Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, leo naomba nianze mchango wangu, kwanza kumpongeza sana Mheshimiwa Rais mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa muda wake mfupi wa kuongoza nchi yetu baada ya kifo cha Rais wetu wa Awamu ya Tano Mheshimiwa John Pombe Magufuli. Mheshimiwa Samia ameonesha umahiri mkubwa wa kuliongoza Taifa letu, na hatimaye kutuletea bajeti hii ambayo inakwenda kujibu kero nyingi za wananchi wetu na kuboresha uchumi wa nchi yetu. Mimi binafsi nampongeza sana Mheshimiwa Rais na namwombea kwa Mwenyezi Mungu ampe afya njema na umri mrefu wenye manufaa kwake na kwa Taifa letu.

Lakini pia nimpongezi Mheshimiwa Waziri na watendaji wote katika Wizara hii kwa kuja na bajeti nzuri yenye kuzingatia maoni mengi ya Waheshimiwa Wabunge walipochangia Wizara mbalimbali za kisekta. Hii inaendelea kuthibitika kuwa Serikali yetu inayoundwa na CCM ni Serikali sikivu, inayozingatia maoni ya wananchi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo yote sasa naishauri Serikali kuendelea kusimamia utekelezaji wa bajeti hii nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo hapo juu naomba sasa kuishauri Serikali kuzingatia yafuatayo ili kuboresha utekelezaji wa bajeti hii:-

Kwanza katika Wizara ya Ujenzi, iko miradi ya aina kuu mbili katika ujenzi wa barabara zetu hapa nchini; miradi ya upembuzi na usanifu wa kina wa barabara zetu, miradi imekuwa ikiigharimu Serikali fedha nyingi na miradi ya ujenzi wa barabara zilizokamilika kwenye hatua hiyo hapo juu.

Katika hatua hii naishauri Serikali kupunguza au kuacha kuendelea na miradi ya upembuzi yakinifu hadi pale barabara zote zilizokwishakamilika katika upembuzi na usanifu wa kina zitakapofikiwa hatua za ujenzi. Nayasema haya kwa kuwa tunazo barabara nyingi zilishafanyiwa upembuzi na usanifu wa kina kwa muda mrefu. Kwa kuwa zinakaa muda mrefu bila kujengwa, na pale tunapokwenda kuzijenga tunalazimika kuzirudia upembuzi upya jambo ambalo linaongeza gharama za ujenzi bila sababu, kwa nini tuendelee kufanya upembuzi kwenye barabara mpya kabla ya ujenzi wa zile zilizokamilika?

Pili ni kuhusu uhifadhi wa wanyama pori; hapa naomba kuishauri Serikali kuja na mpango mkakati wa kuimarisha hifadhi zinazomilikiwa na jamii zijulikanazo kama WMAs. Hifadhi hizi zinamilikiwa na jamii, lakini Serikali isipokuja na mkakati maalum zinakwenda kufa. Kuimarika kwa hifadhi hizi kungepunguza sana manung’uniko katika jamii hasa zile Halmashuri zinazopakana na hifadhi zetu za Kitaifa. Kuimarika kwa WMAs wananchi wetu wanaenda kuona manufaa ya moja kwa moja uwepo wa wanyama hawa, pale ambapo mfano WMAs watajenga darasa au choo na miradi mingine kama hiyo ambayo inaenda kugusa maisha yao ya kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, WMAs wasaidiwe kutafuta wawekezaji kwenye vitalu vyao na kuvifanyia matangazo ili kuvutia wawekezaji. Sambamba na hilo niiombe sana Serikali kuharakisha malipo yao ya hizi jumuiya yanatolewa kwa wakati. Hapa napo napendekeza malipo hayo yaende moja kwa moja kwenye jumuiya badala ya kupitia TAWA ambako zinachelewa sana kuwafikia walengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, narudia tena WMAs zikifanya vizuri zinasaidia sana kupunguza machungu kwa jamii yanayotokana na athari za wanyamapori. Lakini pia ni ukweli usiopingika kuwa uwezo wa kuzitangaza hifadhi hizi zinazomilikiwa na WMAs wakiachiwa wenyewe ni mdogo sana.