Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini nikushukuru wewe pia kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze na ushauri. Kwenye Bajeti hii ya Wizara ya Fedha kwenye Sekta yetu ya Kilimo bajeti yake yote ni 0.93 ya bajeti kuu. Kwa hiyo, nashauri sana, Waziri wa Kilimo na Waziri wa Fedha kwenye jambo hili mnapokuja na bajeti ya mwakani kwenye Wizara yetu hii ya Kilimo ambayo inachangia pato la Taifa kwa asilimia 26, vile vile inachangia chakula kwa asilimia 100, basi mlete mpango ambao utakuwa endelevu, utakaoifanya Wizara hii iweze kukimbia. Hii tumeshapitisha, lakini naomba sana Waziri wa Fedha na Waziri wa Kilimo mtakapokuja mwakani, msije tena na bajeti ya kilimo ambayo haifiki hata 1% ya gross budget ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wote mnajua kabisa kwamba kwenye kilimo ndiyo tunategemea malighafi zote za kiwanda, kwenye kilimo ndiyo huko tunakotegemea kwenye chakula, kwenye kilimo ndiyo hiyo asilimia 26 ambayo kama inaleta pato la asilimia 26 halafu unawekeza asilimia 0.93 maana yake hatukitendei haki kilimo. Kwa hiyo, ni rai yangu na ombi langu kwa Serikali mwakani mnapoleta bajeti ya kilimo, leteni bajeti iliyojaa ili itusaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasisitiza tu kuwaomba Wizara ya Fedha na Wizara ya Kilimo wanapoleta bajeti ya kilimo mwakani, basi waongeze fungu la bajeti ya kilimo kwa kuwa kilimo kinachangia pato la Taifa kwa asilimia 26 na kinachangia chakula kwa asilimia 100. Sasa ukilinganisha bajeti yetu hii ya kilimo ya 0.9 percent haioneshi kwamba tunakwenda kukifanyia kilimo yale mabadiliko ambayo tunayahitaji. Kwa hiyo, ni maombi yangu sana kwa Serikali hii ya CCM Sikivu, kwenye hili mlibebe kwa ajili ya bajeti ya mwakani, mlifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana bajeti hii. Tarehe 31 ya mwezi wa 12 mwaka 2020, watu wa TRA waliandika barua kupeleka kwenye vyama vyetu, kwa Wakuu wa Mikoa wakitaka wakulima watoe tozo kwenye korosho ya Income Tax ya 30 percent. Sasa kwa sababu Wizara imekwishatoa maelekezo na wanaopaswa kulipa Income Tax pato lao ni lazima lianzie shilingi 270,000/= na kuendelea, ukifanya overall ya wakulima wa korosho wote, kwa maelezo ya Wizara kupitia Naibu Waziri Mheshimiwa Bashe, mkulima wa kawaida anazalisha shilingi 1,400,000/= kwa mwaka. Maana yake pato la kawaida kwa mwezi halizidi hata shilingi 120,000/=.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba sana Wizara ya Fedha iiambie TRA, wakulima hawa ambao wanachangia Export Levy kama korosho inakuwa shilingi 3,000/=, 15 percent Export Levy ni shilingi 400/= na kidogo. Ukijumlisha na cess shilingi 50/=, mkulima huyu anachangia zaidi ya shilingi 506/=. Sasa unapokaa ukawataka wakulima tena walipe Income Tax hii ni kutaka kuigombanisha Serikali na Chama cha Mapinduzi ambacho kinaongoza dola, kwa sababu hawa ni watu ambao ni wa chini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawaomba sana Wizara ya Fedha na Msaidizi wako, mwaambie watu wa Mamlaka ya Mapato maana ninanyo hapa barua waliyoiandika tarehe 31 kutaka wakulima walipe Income Tax; mwaambie wakulima hawa pato lao haliwafanyi wao kulipa Income Tax. Kwa hiyo, nawaomba sana. Hawa wakulima kuna tozo nyingi ambazo wanapita kulipia bila hii ambayo mnataka kuwatoza tena. Kwa hiyo, mtoe maagizo kwa TRA waiondoe hii kitu kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tena kwa Wizara, nimeona mnaleta Miswada ya Sheria ya Fedha hapa, ile Export Levy tunayoiomba ambayo 2017 tuliondoa kifungu kile Na. 17(a) tunaomba mnapoleta Mabadiliko ya Sheria ya Fedha, kwa sababu na yenyewe iko ndani ya Mabadiliko ya Sheria ya Fedha, basi na ile muilete tena ili tuirudishe Export Levy wale watu wa CIDTF wapate fedha ili kwenye korosho mpunguze mzigo wa haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu walishagusia hapa mambo ya Madiwani. Naiomba Wizara, wakati mnajiandaa kufanya maboresho ya mambo haya, hata ile posho kama mnaweza, bajeti ya mwakani itawaruhusu vizuri, basi mwongeze posho ya Madiwani, at least wao ndio wanafanya kazi kubwa na ndio wasaidizi wetu kule chini wakati wote tunapokuwa tuko kwenye shughuli zetu hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tena Wizara ya Fedha kama itawapendeza, wenzangu wamesema sana, zile fedha ambazo mmesema kuwapa wale watendaji wetu wa Kata, basi ikiwezekana mzitoe moja kwa moja na kama hamna hizo fedha, mwandike waraka kwa Wakurugenzi. Wakurugenzi hawa na Watendaji wetu wa Kata; Mtendaji wa Kata hawezi kwenda kwa Mkurugenzi kumwomba hiyo shilingi 100,000/=. Hata ingepita miezi mitano hajapewa, hawezi kwenda kumwomba. Fuatilieni mifano rahisi sana kwenye ofisi hizi za ma-DC, Maafisa Tarafa hizo posho walishakaa na Mheshimiwa Rais Marehemu Dkt. Magufuli lakini hizo posho bado hawapati kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawaomba sana, mnapokwenda kutekeleza hii sheria mbayo mmetaka wapewe posho hizi la shilingi 100,000/=, basi ikiwapendeza Wizara ya Fedha mzipeleke ninyi wenyewe moja kwa moja ili kuondoa conflict baina ya Watendaji wa Kata na Wakurugenzi na mara nyingi Wakurugenzi wanaweza wasiwape kabisa kwa sababu tunajua hali za Halmashauri zetu. Wakati mwingine wanafanya bila kukusudia kwa sababu mapato yao na makusanyo yao siyo mazuri. Nawaombeni sana kwenye hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuomba, kilio cha Wenyeviti wetu wa Serikali ya Vijiji kwa kweli kimekuwa kikubwa sana. Hata hiyo posho ndogo ya shilingi 10,000/= ambayo baadhi ya maeneo wanasema wapewe, unaweza ukashangaa miezi minane hajapata hata shilingi 10,000/= moja. Kwa hiyo, naiomba Serikali na Wizara, kama itawapendeza hawa Wenyeviti wetu wa Serikali za Vijiji nao mwaandalie posho, siyo hii shilingi 10,000/=; mtakayoona inafanana na maisha ya sasa ili wafanye kazi zao kwa uadilifu mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)