Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Taska Restituta Mbogo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Na mimi niungane na wengine kukupongeza, Kiti kimekuenea. Napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri Ndumbaro na Makamu wake Mheshimiwa Mary Masanja. Nampongeza Katibu Mkuu Allan Kijazi na watendaji wote wa Serikali. Napenda pia kumpongeza Profesa Silayo kwa kazi nzuri aliyoifanya nchini kwa kulinda misitu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 17 ya pato la Tanzania linatokana na utalii na asilimia 25 ya pesa za kigeni zinatokana na utalii nchini kwetu Tanzania. Nichelee kusema kwamba barabara zinazokwenda kwenye hifadhi za Taifa za nchini kwetu hazifai. Sasa kama barabara haifai, hili pato la Taifa litapanda vipi? Tulikwenda Ruaha National Park barabara kutoka Iringa Mjini kwenda Ruaha National Park, ukimpeleka mgeni pale, the moment anafika pale Ruaha National Park akirudi the business is finished there! Hatarudi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu, Wizara hii ishirikiane na Wizara ya Ujenzi waweze kujenga barabara zote zinazokwenda kwenye Hifadhi ili utalii uweze kukua nchini kwetu Tanzania. Kama tunavyojua, wageni wanapokuja wanataka kuona vitu mbalimbali. Hivyo basi, ninaishauri Wizara ya Maliasili na Utalii, isijikite kwenye utalii wa wanyamapori peke yake. Hebu fungukeni, nendeni kwenye utalii mwingine, nendeni kwenye utalii wa fukwe (Marine tourism); nendeni kwenye utalii wa nyuki (Api-tourism); nendeni kwenye utalii wa misitu (forest tourism); nendeni kwenye utalii wa malikale (traditional tourism); msijikite tu kung’ang’ania kuangalia tembo, faru na simba. Fungueni milango mingine ya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niyaseme hayo kwa sababu nimeona kila kitu ni wanyamapori, wanyamapori. Utalii mwingine, hautangazwi. Naomba mtangaze na utalii mwingine ambao unapatikana nchini mwetu kama nilioutaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze suala la uhifadhi wa malikale. Uhifadhi wa malikale nchini Tanzania haupo. Tunazo malikale nyingi nchini Tanzania, lakini hazijahifadhiwa vizuri na hatujaziweka kama ni kivutio cha watalii kuja nchini kwetu Tanzania. Labda kuzisema tu kwa uchache, tunayo mapango ya Amboni Tanga, tunayo Laitoni footprint ambayo iko kule Ngorongoro, tunayo magofu ya Kilwa, tunacho kimondo pale Mbozi, tunayo michoro iliyochorwa kule Kondoa Irangi; lakini pia UNESCO walizitambua hifadhi za Ngorongoro kama ni urithi wa dunia; walitambua pia magofu ya Kilwa kama ni urithi wa dunia; walitambua pia hifadhi ya Taifa ya Selous kama urithi wa dunia; walitambua pia hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro kama ni urithi wa dunia; walitambua Mji Mkongwe wa Jiji la Zanzibar kama urithi wa dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hivi vitu, Wizara ya Maliasili na Utalii ivizingatie na iviweke viwe kama ni vivutio vya utalii nchini kwetu Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo napenda kulizungumzia hapa ni suala la wanyama wanaovunwa. Kuna mito ambayo ina mamba mengi na kuna maziwa ambayo yana mamba wengi kama Rukwa, lakini pia kule Mpanda kuna bwawa moja la Milala ambalo lina viboko wamejaa pale mpaka siku hizi hatutumii yale maji ambayo zamani tulikuwa tunatumia. Naomba Wizara hii ya Utalii iangalie wale wanyama waharibifu kama mamba wavunwe na kama viboko wavunwe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Taska Mbogo.

MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja, maana yangu ni kwamba hatuwezi ku-compromise maisha ya binadamu na wanyama ambao tumepewa tuwatunze. (Makofi)