Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, lakini nitumie fursa hii kukupongeza kwa nafasi uliyonayo. Hongera na naamini utakitendea haki kiti hicho. Naomba nianze kuchangia Wizara hii alipoishia Mheshimiwa Olelekaita kwenye migogoro ya hifadhi na watumiaji wengine wa ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi watu wa Mkoa wa Dodoma tuna mapori mawili ambayo yako Wilaya ya Chemba na Wilaya ya Kondoa. Pori la Mkungunero ambalo lipo Kondoa na Pori la Swagaswaga ambalo lipo Wilaya ya Chemba. Pori hili la Mkungunero limekuwa ni kichaka cha Maafisa wa Wanyamapori kutesa Watanzania wasiokuwa na hatia eti kwa sababu tu wana ng’ombe, eti kwa sababu tu ni wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2019 nilizungumza ndani ya Bunge hili nikaeleza mateso na manyanyaso wanayopata wananchi wa wilaya ya Kondoa kwa Kata ya Keikei, Kata ya Kinyasi pamoja na Kata ya Itasu. Mheshimiwa Waziri nimekuja kwako mara kadhaa nikiwa nakulalamikia suala hili na ninyi Wizara mnasema kuna shida gani? Pale tumemaliza kabisa Mkungunero. Ukweli ni kwamba mnafukia kombe mwanaharamu apite wakati Watanzania wanaumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki mbili zilizopita kuna wananchi watatu ambao wamekamatiwa ng’ombe wao. Wawili wamelipa kwa makubaliano na Maafisa Pori wa Hifadhi ya Mkungunero. Mmoja akakataa akapelekwa Mahakamani, ng’ombe 50 kalipa shilingi milioni 10 faini. Hivi huyo mwananchi mkulima, mfugaji anayetegemea mifugo yake kwa ajili ya kuendesha maisha yake ya kila siku na kulichangia kodi Taifa hili, mnachomtafuta ni nini watu wa hifadhi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi, katika hifadhi ile kuna akina mama ambao wanafanya shughuli zao mbalimbali za kujitafutia uchumi, wamekuwa wakibakwa kwenye Hifadhi ya Mkungunero, wamekuwa wakipata mateso ya kurushwa kichurachura, kupigwa na kila aina ya mateso kadha wa kadha wanayoyapata kwa ajili ya hilo pori. Mheshimiwa Waziri, kuna shida gani? Serikali ni moja, chama kimoja, Mawaziri mnakaa kwenye Baraza la Mawaziri, mnashindwaje kukaa chini na kuweza kutatua mgogoro wa pori hili? Serikali Sikivu, Serikali ya wanyonge mnaotamani kuwapigania Watanzania, hawa Watanzania hawana hatia, ardhi haiongezeki Mheshimiwa Waziri, watu tunaongezeka.

Pori lile Mheshimiwa Waziri kwa akili tu ya kawaida, Warangi sisi hatuna mahali pa kwenda. Lile ndiyo eneo letu tumezaliwa kule, twende wapi? Tunaomba Pori ya Mkungunero, kagaweni eneo, tuachieni na sisi watoto na wajukuu tuendelee kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pori la Swagaswaga Wilaya ya Chemba Kata ya Lahoda, pale kuna wafugaji; na ninashukuru Mheshimiwa Mpina amelisema. Kuna wafugaji mwaka 2018/2019, Mheshimiwa Mpina ukiwa Waziri wa Mifugo, Mheshimiwa Ulega akiwa Naibu Waziri wako; Mheshimiwa Ulega alienda Wilaya ya Chemba Pori la Swagaswaga akakutana na wafugaji waliokamatiwa ng’ombe wao wasiokuwa na hatia wamewekwa pale, hawana chakula, hawana maji, hawana dawa, hawana chochote. Ng’ombe wamekufa zaidi ya 500. Tulisema humu ndani, hamkutaka kusikia eti tu kwa sababu mnalinda uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji uhifadhi lakini siyo kwa maisha ya mateso ya namna hii mnayotufanyia Watanzania. Mkitushirikisha wananchi, tutaulinda huo uhifadhi kwa sababu na sisi tunautaka na tunauhitaji sana. Ila kama mtaendelea kutunyanyasa, kututesa na kutuonea, hata hao wahifadhi wenu mnaowaleta kule, ipo siku hapatatosha. Tutachoka kunyanyaswa, tutaamua kuchukua hatua mkononi, kitu ambacho sitamani kitokee. Mheshimiwa Aida amesema, kwake imeshatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri Mstaafu Mheshimiwa Mpina kasema. Zaidi ya ng’ombe 400 mpaka leo Wizara ya Maliasili hamtaki kurudisha ng’ombe wale, mnachotaka ni nini? Mmewapeleka wapi hao ng’ombe? Nani anao mpaka leo miaka miwili?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)