Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

Hon. Edwin Enosy Swalle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati

MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, asante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kuungana na Wabunge wenzangu kutoa pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri wake na timu nzima ya Wizara hii. Hata mimi ni shuhuda ambaye nimekuwa nikiongea na Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, wamekuwa ni wasikivu sana.

Mheshimiwa Spika, Sera yetu ya Umeme inasema Umeme kila Kijiji. Hata kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri inaeleza idadi ya vijiji ambavyo bado kupata umeme lakini sisi katika Jimbo la Lupembe bado tupo kwenye shida ya kupata umeme kwenye ngazi ya kata. Zipo kata ambazo hazina umeme hata katika level ya kata, achilia mbali vijiji.

Mheshimiwa Spika, Kata kama za Ukalawa, Ikondo, Mfiriga na Idamba, hakuna umeme. Maeneo haya palikuwa na mtu binafsi alikuwa na umeme unaitwa umeme wa Sefa ambapo watu wa Wizara waliwapa nafasi ya kutoa umeme kwa baadhi ya vijiji. Hata hivyo, kwa masikitiko makubwa sana ule umeme ambao ni wa Sefa kwanza ni wa bei ghali sana kwa sababu ni wa mtu binafsi, lakini pili umekuwa na changamoto nyingine, ule umeme hauna uwezo wa kuendesha hata mashine ya kukoboa na kusaga.

Mheshimiwa Spika, viko baadhi ya vijiji kwa mfano sehemu za Image, ikifika jioni saa 02.00 wananchi wamerudi mashambani wakiwasha TV zao haziwezi ku-operate kabisa kwa sababu umeme hauna nguvu, hata redio za kawaida, TBC au redio ndani ya mkoa umeme huu hauna uwezo wa kuziendesha. Kilichobaki sasa wananchi hawa wanaendesha hizi mashine na redio kwenye sehemu za starehe kwa kutumia mafuta. Kwa hiyo, nashauri sana Serikali katika karne hii ya 21 kwa muda ambapo tupo katika Sera ya Viwanda kuwa na jimbo ambalo hata umeme kwenye kata haujafika, hatutendi haki kwa wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Lupembe lina fursa nyingi za utajiri kwa ajili ya viwanda; Lupembe tunalima sana zao la chai kuna viwanda zaidi ya viwili vinahitaji umeme, Lupembe inalima sana matunda, hasa nanasi, wako watu wengi wana nia ya kuwekeza kwenye nanasi maeneo ya Madeke lakini kwa sababu hakuna nishati ya umeme wanashindwa kuweka viwanda ambavyo vingetoa ajira nyingi sana kwa vijana wetu. Pia kulikuwa na fursa nzuri ya kuweka viwanda vya parachichi kwenye jimbo hili lakini kwa sababu ya changamoto ya umeme wawekezaji wengi hawaji tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishauri sana Wizara ya Nishati pia kwenye maeneo ambayo kuna umeme wa REA kiasi kuna shida kubwa na mara kadhaa nimeongea na Naibu Waziri, Mheshimiwa Byabato kwamba umeme ambao upo umekuwa na wenyewe ni kero kuliko hata usingekuwepo. Wananchi wana mashine zao mfano, mteja amekuja kusaga unga kabla hujamaliza kusaga umeme umekatika. Kwa hiyo, mwananchi anashindwa kwenda kufanya kazi nyingine anasubiria mpaka umeme urudi na hajui unarudi saa ngapi.

Mheshimiwa Spika, pia kuna wananchi wa mashine ndogo au viwanda vidogo vya kuranda mbao. Kuna msiba, inabidi watu warande mbao kwa ajili ya shughuli ya msiba, umeme unakatika. Kwa hiyo, tatizo la kukatika umeme kwa nchi nzima ni kubwa na namuomba sana Waziri kama walivyoongea Wabunge wengi humu ndani, hii ni shida kubwa ukiachilia mbali kupeleka umeme kwenye kila kijiji, lakini kuwa na umeme ambao hauna uhakika pia ni kero kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu wako wananchi wamepata hasara sana, wameunguza redio, kuna mwananchi wangu mmoja mpaka nyumba yake imeungua kwa sababu ya kero ya umeme kukatika. Kwa hiyo, nimuombe Waziri pamoja na sifa nyingi ambazo tumetoa kwenye Wizara yake lakini tatizo la umeme kukatika, kutotabirika, kutokuwa na nguvu, Wizara hii itoe kipaumbele wasiweke tu kipaumbele kupeleka umeme kwenye kila kijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)