Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

Hon. Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Waziri wa Viwanda na Biashara na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwa kuwasilisha vizuri hotuba ya bajeti na ripoti ya Kamati. Pia niwapongeze sana wataalamu na wadau kwa kazi kubwa wanazofanya kwenye kuipeleka nchi yetu kwenye Tanzania ya viwanda, ndoto iloyobebwa kikamilifu na Serikali ya Awamu ya Tano na Sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkoa wa Kilimanjaro ulikuwa una historia ya kuwa na viwanda vingi ambavyo vilichangia sana kwenye ajira na mapato ya mkoa na Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vingi vya zamani vilivyokuwa na majina makubwa kimkoa na kitaifa kwa sasa vimefungwa. Baadhi ya viwanda maarufu ambavyo havifanyi kazi ni Kilimanjaro Machine Tools Manufacturers Ltd., Twiga Chemicals Ltd. cha kuzalisha madawa ya kilimo, Kiliwood Products Ltd. cha kuzalisha bidhaa za mbao, Kibo Paper Ltd. cha kuzalisha karatasi, Tanzania Packaging Manufacturers (1998) Ltd. cha kuzalisha magunia, Kiwanda cha Viatu Msuni kilichofunguliwa miaka ya 1970 na Baba wa Taifa, Kibo Match Ltd. cha viberiti na Kilimanjaro Paddy Hulling Co. Ltd. cha kukoboa mpunga kilichopo Chekereni, Kata ya Mabogini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufa kwa viwanda hivi kwa kiasi kikubwa kumesababishwa na baadhi ya wawekezaji kutokuwa na nia thabiti ya kuviendeleza, kubadilika kwa teknolojia za uzalishaji na ushindani wa bidhaa kutoka nje kama vile mifuko ya jute iliyoua soko la magunia ya katani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuhamasisha uanzishaji wa viwanda vipya mkoani Kilimanjaro kama ilivyo kwenye mikoa mingine hapa Tanzania. Kuanzia Disemba, 2017 hadi kufikia Machi, 2020 mkoa wa Kilimanjaro ulikuwa na viwanda vipya 113; kati ya hivi, viwanda 80 ni vidogo sana, viwanda 26 ni vidogo, viwanda vinne ni vya kati, na viwanda vitatu ni vikubwa. Viwanda hivi vinachangia kikamilifu kwenye pato la mkoa na Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa viwanda katika kujenga uchumi wa nchi yetu na kutoa ajira, ninaishauri Serikali iwe na programu maalumu ya kufufua viwanda vya zamani vilivyowahi kutoa mchango mkubwa wa kiuchumi na iendelee kuhamasisha uanzishwaji wa viwanda vipya mkoani Kilimanjaro kwani kuna miundombinu rafiki na hii itaboresha uchumi wa mkoa na Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda muhimu vyenye tija na ninavyopendekeza vifufuliwe ni kwanza Kiwanda cha Kukoboa Mpunga cha Kilimanjaro (Kilimanjaro Paddy Hulling Company Ltd.) kilichopo Kata ya Mabogini. Serikali ilikabidhi kiwanda hiki kwa Chama Kikuu cha Ushirika (KNCU) kinachojishughulisha na biashara ya kahawa na tokea mwezi wa Septemba, 2014 kimekuwa hakifanyi kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili lilikuwa kosa kubwa sana na KNCU, walishindwa kukiendesha, na ulikuwepo mgogoro mkubwa sana wa umiliki wa kiwanda hicho na Umoja wa Wakulima wa Mpunga wa CHAWAMPU ambao ni wakereketwa wa mpunga. Msajili wa Hazina amekirudisha kiwanda hiki Serikalini toka mwezi Oktoba, 2018.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishauri Serikali iwasiliane na wadau mbalimbali ikiwemo CHAWAMPU ili apatikane mwekezaji atakayekifufua na kukiendesha kiwanda hiki kwa tija. Kiwanda hiki kimezungukwa na wakulima wa mpunga wanaozalisha mara mbili kwa mwaka.

Pili ni Kiwanda cha Viatu Msuni kilichopo Kata ya Uru Kaskazini; kiwanda hiki kinamilikiwa na Kamati ya Maendeleo Kata ya Uru Kaskazini (WDC). Kina uwezo wa kuzalisha bidhaa mbalimbali za ngozi. Ninaiomba Serikali itume wataalamu wa TiRDO kwenye kiwanda hiki ili ushauri wa kitaalamu upatikane na kiwanda hiki kifufuliwe na kuunga juhudi za wana ushirika huu kwenye kukuza uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu ni Kiwanda cha Magunia; kiwanda hiki kinamilikiwa na Mohamed Enterprises Ltd. Kiwanda hiki hakijafanya kazi toka kinunuliwe miaka 14 iliyopita (2006). Tunaishauri Serikali ifuatilie utekelezaji wa mwekezaji wa kuanzisha uzalishaji wa magunia. Ikibainika kuwa safari ya uzalishaji kama bado ni ndefu, Serikali ichukue hatua stahiki kwa manufaa ya Taifa.

Nne, ni Kiwanda cha Madawa ya Kilimo cha Twiga Chemicals; kiwanda hiki kinamilikiwa na Twiga Chemicals Ltd. na bado miundombinu yake ni mizuri. Kwa kuwa kiwanda hiki kimerudishwa Serikalini kupitia kwa Msajili wa Hazina toka Oktoba, 2018, ninaishauri Serikali iharakishe kumtafuta mwekezaji ili dawa za kilimo zizalishwe hapa nchini na kuokoa fedha zetu za kigeni ambazo hutumika kuagiza madawa ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tano niKiwanda cha bidhaa za Mbao (Kiliwood Products Ltd.); kiwanda hiki kilikuwa kinamilikiwa na Hans Industries na kwa kuwa alishindwa kukifufua, kupitia kwa Msajili wa Hazina kimerudishwa Serikalini. Ninaishauri Serikali iharakishe kumtafuta mwekezeji ili uzalishaji urejee na kuliwezesha Taifa kuzalisha bidhaa za mbao na kuachana na utaratibu wa kuagiza bidhaa kutoka nje. Malighafi za mbao zinapatikana kwa wingi hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sita ni Kilimanjaro Machine Tools; kiwanda hiki kinamilikiwa na Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC). Kiwanda hiki kinaweza kutoa mchango mkubwa sana kwenye kuzalisha vipuri vya mashine za aina mbalimbali na kuokoa matumizi ya fedha za kigeni za kuagiza vipuri kutoka nje ya Tanzania. Ninaiomba Serikali iisaidie NDC kwenye kuingia ubia na wadau mbalimbali na kukifufua kiwanda hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkoa wa Kilimanjaro una fursa nyingi sana za kuanzisha viwanda vipya. Mkoa huu una fursa kubwa za kilimo cha mboga, kahawa, ndizi, mahindi, maharage, mpunga, matunda na maziwa. Bidhaa hizi zinaweza kutumika kuanzisha viwanda vidogo vidogo na kuongeza thamani ya mazao yetu yanayozalishwa mkoani Kilimanjaro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufanikisha hili ninaishauri Serikali ianzishe programu maalumu itakayowashirikisha wadau muhimu wa viwanda kama vile TiRDO, SIDO, TCCIA, VETA na CTI ili watoe mafunzo ya kuhamasisha ujasiriamali wa viwanda mkoani Kilimanjaro. Mkazo uwe kwenye kusindika matunda, mbogamboga, maziwa, unga wa mahindi, michele na maharage. Kuna uwezekano mkubwa sana wa kuanzisha viwanda vya usindikaji wa kahawa na kutengeneza juice au mivinyo ya ndizi mbivu. Serikali ikiweka mazingira wezeshi, wajasiriamali wengi wa Kitanzania watatumia fursa hii kutengeneza ajira na kuingizia mkoa na Taifa mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.