Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami kuchangia kwenye Wizara hii.

Kwanza nami niungane na wenzangu kumshukuru Waziri na Naibu wake kwa hotuba nzuri ambayo wameiwasilisha. Lakini pia niungane na michango mingi ambayo imetoka ukiwepo ule ambao wewe mwenyewe umeuzungumza kwa uchungu sana jana wa NARCO ni hali halisi ambayo Waziri anatakiwa aone ni namna gani chombo kile kilivyo kwa sasa kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kulingana na muda nitachangia maeneo mawili na nitaanza na eneo moja la rasilimali za malisho na maji kwa ajili ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, tunalo tatizo kubwa sana linalosababisha ukosekanaji wa malisho ya mifugo na hii inasababishwa na ufinyu wa maeneo ambayo wafugaji wetu wa kawaida wanafugia na jambo hili linasababishwa vilevile na watu hawa ambao ni wafugaji wadogo wa kwenye maeneo yetu kutokuwa na uhakika wa kumiliki ardhi. Matokeo yake wanakwenda kwenye maeneo ambayo yana maji ya asili kama mabonde ya Mto Ruvu, mabwawa mbalimbali na kwa kuyafuata maji hayo wanasababisha kuwe na matatizo makubwa ya migogoro ya wakulima na watumiaji wengine wa ardhi hasa hasa wafugaji. (Makofi)

Kwa hiyo, nilikuwa naushauri kwa Wizara, ipo migogoro ambayo inasababishwa na matatizo haya na ufumbuzi wake ni kutaifisha maeneo ambayo hayatumiki kwa sasa na kupewa hawa wafugie, maeneo ya kwanza yakiwa haya naitwa NARCO. Hizi Ranchi nyingi, ranchi hizi ni sawasawa na wawekezaji wengine wowote, kama Serikali kupitia Wizara ya Ardhi inayouwezo wa kufuta hati kwenye mashamba makubwa ya wawekezaji na yakagawiwa wananchi au wakarudisha Serikali kwa ajili ya kupangiwa matumizi mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ningeshauri Wizara ya Ardhi itazame hizi ranchi ikiwezekana wazifutie umiliki, wazirudishe kwa wafugaji wadogo, wapewe bure, wakakatiwe vitalu kule ndani na wasilivipie, wamilikishwe ili waendeleze shughuli zao kwa sababu wao ni Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili ambalo ninataka nilizungumzie ni suala nzima la utatuzi wa migogoro. Nimeona kwenye hotuba ukurasa wa 48 Waziri ameeleza namna alivyoshungulikia migogoro hasa kwenye jimbo langu na amevitaja vijiji ambavyo amehisi kwamba amemaliza migogoro.

Mheshimiwa Spika, kwanza niombe nimueleze Waziri kwamba migogoro hii anayohitaji haijamalizwa na mimi wasiwasi wangu inawezekana wataalam hawa wamemaliza mgogoro kupitia ofisi kwenye ramani, wameitazama ramani ya ukubwa wa shamba, wakaligawanya kwa majibu haya walioyatoa, lakini halialisi kwa wananchi siyo hii. Leo hii ukienda Dutumi ambako wao wanazungumza wamewaachia hekta 1,600. Ukienda kule kuna mgogoro mkubwa hili jambo siyo kweli, wametaja wamekwenda Madege wamewakabidhi hekta 400 siyo kweli maana yake juzi tu Wizara ya Ardhi imepeleka kule wapimaji kwa ajili ya kurekebisha maeneo kwa ajili ya kutaka kuwapatia Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha eneo la kuliendeleza pale katika eneo la bandari kavu, bado kule wamekwenda wataalam wamekwama. Kuna mizozo mikubwa, wananchi hawajaridhika, hawaelewi na wanachozungumza wao hawa wananchi ni kwamba hili shamba linatajwa kwamba ni mali ya Wizara ya Mifugo, lakini ukweli halisi kwa maisha yao yote hawajawai kuona likiendelezwa wao wameishi mle kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa nilitaka niikumbushe Wizara kwamba tukukumbuke historia ya nchi yetu, maeneo mengi tulianzisha operation vijiji, na tulipovianzisha vijiji vile watu walienda kuingia kwenye maeneo ambayo yalikuwa wazi, leo wao wanapokwenda kumaliza migogoro kwa kutazama ramani zao za miaka iliyopita ufumbuzi unakuwa haujapatikana kwenye maeneo husika. Ningeomba Wizara ifike kwenye maeneo haya ili ikaone namna gani tunaweza tukamaliza tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini pia lipo tatizo la migogoro kwenye maeneo haya na ningeomba Waziri...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Mwakamo dakika tano ni chache.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)