Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Sylivia Francis Sigula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia. Nianze kwa kuiongeza Wizara, hasa kumpongeza Waziri na timu yake. Wakati uliopita nilitoa kero zangu hapa kuhusu wavuvi wa Ziwa Tanganyika, lakini Waziri alifika Kigoma akaongea na wavuvi na baadhi ya kero akazitatua. Wavuvi wa Kigoma na wavuvi wa Mwambao mwa Ziwa Tanganyika wanaipongeza sana Serikali Sikivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nitakuwa na uchangiaji mdogo sana; na leo nina kero chache ambapo naamini Serikali yetu ni sikivu itakwenda kuzifanyia kazi. Namwomba Mheshimiwa Waziri wakati wa majumuisho aweze kutupatia ufafanuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati nachangia nilieleza umuhimu wa Ziwa Tanganyika. Kwa tafiti zetu zilizofanyika, nilisema Ziwa Tanganyika lina kina kirefu ambacho ni mita 1,470. Masikitiko yangu makubwa ni kwamba hili Ziwa Tanganyika ni kama Serikali hailioni. Naongea haya nikiwa na masikitiko makubwa kwa sababu moja. Ziwa Victoria lina urefu wa kina cha mita 120, na Ziwa Tanganyika ni mita 1,400 lakini tunaona kwamba kuna kanuni kandamizi kwa wavuvi wetu wa Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na tafiti zilifanywa na TAFIRI zinasema kwamba uwezo wa samaki kuishi, oxygen inayopatikana ni mita 150 kutoka kwenye water surface (kina kile cha juu). Leo wavuvi wa Ziwa Tanganyika wanaruhusiwa kutumia nyavu ambazo zinakwenda kwa mita saba tu. Mbali ya kuwa na kina kirefu, wavuvi wa Ziwa Victoria wanaruhusiwa kwenda mpaka mita 16. Hii siyo sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Wizara watueleze sisi wavuvi wa Ziwa Tanganyika, watuambie ni vigezo gani vinavyotumika ili sisi wavuvi tujue, maana tunaona kwamba hiki kitu siyo sahihi. Kwa hiyo, wavuvi wa Ziwa Tanganyika wanaomba angalau waweze kupatiwa nyavu ambazo zitaweza kwenda hata mita 20 au 25.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kero namba mbili ya wavuvi wa Ziwa Tanganyika, wanatumia taa lakini kanuni zinawataka wasitumie taa zinazozidi watt tano; na kwa chombo kimoja zisizidi watt 50. Sasa kulingana na urefu wa kina cha Ziwa Tanganyika, hiyo taa ya watt 50 kwa chombo inaweza kwenda chini, yaani light intensity kwenda chini ni mita 20 tu. Sasa hao samaki ambao tunasema wako kwenye mita kuanzia moja mpaka 150 tunawapata vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Wizara iingilie kati jambo hili kwa sababu linakuwa ni kikwazo na linasababisha upatikanaji mdogo wa samaki katika Ziwa Tanganyika. Leo hii ukienda Kigoma, kilo moja ya dagaa ni shilingi 28,000/= mpaka shilingi 30,000/=. Hebu ona, mwananchi wa kawaida huyu masikini hatakuwa na uwezo wa kula dagaa ilhali wanavuliwa wanapoona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Wizara itueleze mambo haya wakati wa majumuisho kwamba ni kwa nini tunawazuia wavuvi wasitumie taa ambazo zitaweza kuangaza chini sana? Mapendekezo ya wavuvi wanasema, angalau wapatiwe ruhusa ya kutumia taa ambazo zinaweza kwenda hata mita 200. Kwa hiyo, naomba sana, wavuvi wanasema kama watatumia taa zenye watt 200 wanaweza kwenda chini kuona mpaka mita 70 au 80. Kwa hiyo, naiomba sana Wizara, Waziri wewe ni msikivu na Naibu Waziri wako pia ni msikivu, tunaomba sana jambo hili liangaliwe kwa umakini mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa sababu leo sikuwa na mambo mengi. Wavuvi wa Ziwa Tanganyika wana masikitiko makubwa sana. Mbali ya kuwa ziwa la pili duniani lenye kina kirefu, lakini wamesahaulika. Waziri amesema kwamba Serikali imepeleka zaidi ya shilingi milioni 505 katika Ziwa Victoria, lakini ni aibu, Serikali haijapeleka hata shilingi 100/= kwa wavuvi wa Ziwa Tanganyika. Sasa tuambiwe: Je, wavuvi wa Ziwa Tanganyika ni sehemu ya nchi hii au siyo sehemu ya nchi hii? Kwa sababu tunaona hawanufaiki na Ziwa hili Tanganyika ilhali wanaliona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema haya kwa sababu mimi ni mwakilishi wa vijana na wanaojishughulisha na uvuvi, wengi ni vijana. Nisiposema haya nitakuwa sijawatendea haki vijana wenzangu. Nitaomba sana Mheshimiwa Waziri, atuambie kwa sababu kwa taarifa nilizonazo, mbali ya kupatiwa hiyo shilingi milioni 505 plus, bado kuna vikundi 20 vya Ziwa Victoria tayari uthamini umekamilika na muda wowote wanapewa mikopo hiyo. Ila Ziwa Tanganyika hatuoni. Kama shida ni vigezo, mtuambie tufanye nini ili tu-qualify kupata hiyo mikopo. Haiwezekani tuachwe ilhali tunateseka na sisi ni Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Wizara, watakapokuja kufanya majumuisho, watupatie majibu hayo. Kama sitaridhika na majibu hayo, kwa kweli nakusudia kutoa shilingi kwenye mshahara wa Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze kidogo sana kuhusu mifugo. Mkoa wetu wa Kigoma una mifugo mingi, lakini huwezi kusikia inasemwa kokote kwa sababu moja tu. Miundombinu ya Mkoa wa Kigoma ni hafifu. Kigoma kuna ng’ombe wengi, lakini leo nikitaka kumsafirisha ng’ombe kumpeleka sokoni ni gharama, yaani ng’ombe mmoja naweza nikatumia zaidi ya shilingi 200,000/=. Kwa hiyo, kama nitamnunua ng’ombe Kigoma kwa shilingi 300,000/= ili nimpeleke sokoni, nitahitaji kuongeza shilingi 200,000/=, mpaka anafika sokoni ni shilingi 500,000/. Je, mimi sokoni nitamuuza kwa shilingi ngapi? Kwa hiyo, siyo kwamba Kigoma hakuna mifugo; ipo, lakini miundombinu siyo rafiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzoni kulikuwa kuna mabehewa yanabeba ng’ombe, lakini leo mabehewa yamekufa. Kwa hiyo, naomba kwa sababu jambo hili ni mtambuka, Wizara zishirikiane; Wizara ya Ujenzi na Wizara ya Mifugo, tutakapokuwa na miundombinu ya uhakika tutasafirisha mifugo yetu, tutasafirisha samaki wetu na pia tutaweza kuongeza mzunguko wa fedha katika Mkoa wetu wa Kigoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzoni wakati Waziri anawasilisha, alielezea vizuri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)