Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee suala la NIDA, suala hili kwa kweli limekuwa ni kero. Mimi kama Mbunge naunga mkono Serikali kusema kila raia awe na kitambulisho cha NIDA, lakini ni jambo ambalo linashangaza, Serikali inatangaza wananchi hao wawe na vitambulisho, lakini ninachokiona hiki kilichotangazwa, Serikali ilikuwa haijajiandaa. Hawa wananchi wanasema sisi tupo tayari, mtupe vitambulisho, wanakwenda kwenye Ofisi za NIDA hawapati vitambulisho wanaambiwa shida ni mtandao, kwa kweli hili jambo halijakaa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Serikali iliangalie na nishauri kama Serikali katika hili bado haijajipanga vizuri, ni afadhali kulisitisha kuliko wananchi kuendelea kukosa huduma. Kwa sababu limekuwa ni kero kubwa sana na ukilinganisha kwa mfano mazingira ya kule kwetu Kyerwa, wananchi wanatoka maeneo ya mbali anakwenda wilayani zaidi ya kilomita 30, anashinda pale, hajapata kitambulisho anarudi nyumbani, imekuwa ni kero kubwa sana. Kwa hiyo niiombe sana Serikali ili iliangalie, ikiwezekana kama bado haijajipanga isitishe.

Mheshimiwa Spika, kule kwangu kuna shida, ukienda kwenye Ofisi za NIDA wanasema shida ni mtandao, mtandao mpaka wafuate Wilaya nyingine ya Karagwe. Kwa hiyo niombe zile wilaya ambazo zipo pembezeni na hakuna mtandao wangeacha hili jambo kwa sababu limekuwa ni kero kubwa sana, yaani kule kwetu ukiongelea NIDA wanasema hii ni hatari. Kwa hiyo niombe sana hili liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka nilizungumzie ni suala la watu wa Uhamiaji, kubainisha wale ambao ni raia na sio raia. Mazingira ya kule kwetu ukisema mwananchi aende wilayani ni kero kubwa. Ushauri wangu ninaotoa, Maafisa hawa wa Uhamiaji wawatumie Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji. Waende kule site wakawatumie hawa ndio wanaweza kutambua raia ni nani, haiwezekani Afisa Uhamiaji umetoka Dar es Salaam au Dodoma, unafika Kyerwa unasema huyu siyo raia, hili sio sawa. Wawatumie viongozi ambao wananchi wamewachagua Maafisa Watendaji, Wenyeviti wa Vijiji ili waweze kujua ni nani ambaye ni raia au siyo raia, vinginevyo hii biashara ni kama kuwaneemesha watu. Kwa hiyo hilo niombe sana tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ninalotaka kulizungumzia ni kuhusu hawa mapolisi wetu, pamoja na mambo mengine ambayo yanazungumzwa lakini wanafanya kazi kwenye mazingira magumu sana. Ukifika kule kwangu, sasa hivi wilaya ina zaidi ya miaka saba hawana ofisi, wanafanyakazi kwenye Ofisi ya Kijiji. Tulivyomaliza uchaguzi nilikwenda kuikagua ile ofisi inadondoka wakati wowote, imebidi nichukue fedha niwape milioni 10 angalau tuweze kuboresha ile ofisi ambayo ni ya kata. Kwa hiyo niombe sana, hili liangaliwe. Pia hawana nyumba, wanaishi kwenye mazingira magumu, yaani ni kama kundi fulani ambalo limetelekezwa. Kwa hiyo niombe sana tuliangalie, tuweze kuboresha mazingira wanayofanyia kazi, kwa sababu wanafanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ninaloomba, kule kwetu kuna kitu kinaitwa gongo, ile gongo inatokana na ndizi, hizi ndizi zinatengenezwa wanapata gongo. Serikali tunaomba ifanye utafiti hii gongo iweze kuhalalishwa. Kama tunaruhusu ndizi na hiki kitu kinatokana na ndizi, kwa sababu kuna gongo nyingine inatokana na vitu vya ajabu ajabu, lakini hii inatokana na ndizi. Kwa hiyo, naomba kwa Mheshimiwa Waziri, Wanakyerwa wamenituma, hili jambo liangaliwe. Kwa sababu imekuwa ni biashara ya watu…

SPIKA: Yaani hiyo hoja ni muhimu sana, kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mchungaji anaomba gongo hii.

MHE. CHARLES P. MWIJAGE: Taarifa.

SPIKA: Na kuna taarifa juu ya hayo. Taarifa ipo upande gani! Haya endelea.

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Spika, napenda nimpe taarifa ndugu yangu Mheshimiwa Bilakwate, wanachotengeneza Kagera sio gongo ni enkonyagi au Kaliinya. Kwa hiyo, enkonyagi ni tofauti na gongo, gongo ni haramu enkonyagi sio haramu. (Makofi)

SPIKA: Pokea taarifa Mheshimiwa Bilakwate.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, Ahsante hiyo taarifa nimeipokea kwa kweli inaitwa enkonyagi. Kwa hiyo hili niombe sana, Serikali iliangalie namna gani wanaweza kutafiti kwenye kinywaji hiki ili kiweze kuruhusiwa kwa sababu hata ukimuuliza Mheshimiwa Mwijage na Waheshimiwa wengine wanaotoka Kagera, wote wamesomeshwa kutokana na hiyo akaguri, akakonyagi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine niongelee suala la bodaboda. Hawa vijana wamejiajiri, hebu niombe sana Polisi wetu wajikite kuwapa elimu kuliko kukimbizana nao kila sehemu. Wanafanya kazi kwenye mazingira ambayo ni magumu, unamkamata bodaboda ambaye kwa siku akipata faida kubwa ni shilingi 30,000, unamtoza shilingi 50,000, unamtoza shilingi 200,000; hili kundi tutaendelea kulifanya kuwa maskini. Kwa hiyo niombe sana hili liangaliwe.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)