Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi nami niweze kutoa machache niliyonayo kwenye Wizara hii muhimu ambayo inakwenda kuwahudumia Watanzania walio wengi. Kwa kuanza, nami naomba niungane na wenzangu kwenye suala zima la TARURA. Kwenye suala zima la TARURA nitaomba niende kwenye muktadha tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunapitisha hapa hii taasisi ya TARURA, mwaka 2017, Serikali ilituhakikishia kwenda kutoa ushirikiano wa kutosha kwa watumishi wetu ili waende wakatimize wajibu na majukumu yao kwa ajili ya kuwatumikia Watanzania. Hata hivyo, ninapata kigugumizi na sijui ni kwa nini? Serikali baada ya kuletewa TARURA ikatoa watumishi, wahandisi (engineers) waliokuwa kwenye Halmashauri ikawapandisha na kuwapa nafasi mbalimbali; Meneja wa Wilaya, Meneja wa Mikoa na Wakurugenzi. Baada ya kuwakabidhi majukumu hayo, watu hawa tunavyoongea mpaka leo hii, muda huu nimesimama, dakika hizi ninazoongea, watu hawa kuanzia Meneja wa Wilaya, Meneja wa Mkoa na Wakurugenzi wote, miaka minne kasoro hakuna hata mtu mmoja mwenye barua ya kuthibitishwa kazini kwenye nafasi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu watu hawa wana barua za kukaimu. Wanakaimu miaka minne kasoro, lakini Serikali mpo, halafu ni Ofisi ya Rais, ambayo inakwenda kuhudumia Watanzania walio wengi kwenye Sekta muhimu inayokuza uchumi wa Taifa letu kutokana na kilimo! Mtu ambaye amethibitishwa kazini ni mtu mmoja tu, Mkurugenzi Mkuu wa TARURA, baba yangu Victor ndiye amethibitishwa kazini. Mtu ambaye alifanya kazi hii kwenye Taifa letu na ninatambua mchango wake mkubwa, amelitumikia Taifa lake, akastaafu, lakini akarudishwa tena kwa mkataba, yeye ndio mwenye barua ya kuthibitishwa kazini, wenzake wote wana barua za kukaimu mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Ummy, nakuamini katika uwajibikaji na uchapaji kazi. Kama tunataka kuwasaidia Watanzania na kukuza uchumi wa Taifa letu na watumishi wetu waweze kufanya kazi vizuri kwenye taasisi hii, naomba ukitoka hapa, kesho tunahitimisha bajeti yako, nenda kaanze na suala zima la kuhakikisha watumishi wetu wote wa ngazi ya Wilaya na Mkoa, Wakurugenzi wapate barua zao za kuthibitishwa kazini. Kama mnaona hawafai, waondoeni, tafuteni watu wanaofaa, wapeni mamlaka waweze kufanya kazi. Siyo kuwakaimisha watu miaka minne, ni kitu ambacho hakiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto zinazokwenda kutokana na kukaimisha watu hawa na kutokuwa na mamlaka ya kwenda kutimiza wajibu na majukumu yao ripoti ya CAG inatuambia kutokana na udhaifu huo, TARURA kwa miaka mitatu mfululizo, nitaisema miwili tu mfululizo, imebaki na bakaa. Yaani fedha ambazo zimebaki bila kwenda kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2018/2019 TARURA walibaki na bakaa ya shilingi bilioni 72.3 ambazo leo Wabunge tunapiga kelele humu ndani zingeweza kwenda kufanya kazi. Hakuna mtu wa kufanyia maamuzi, yuko mtu mmoja pale, kazi zimelala, fedha zinarudi, halafu bado sijui tunataka kufanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019/2020 shilingi bilioni 1.5 ziko pale, zimerudi. Barabara tunalalamika, miundombinu ni mibovu, wananchi wanakufa barabarani kwa kukosa huduma za barabara, akina mama wajawazito wanashindwa kwenda kujifungua watoto wao, wanajifungulia barabarani kwa sababu tu ya jambo dogo ambalo tunatakiwa tulisimamie ili watu wetu waweze kupata hiyo huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hebu twende tukafanye hii kazi ya kwenda kuwathibitisha hawa watu kazini ili tuweze kufanya kazi ya kulijenga Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye suala zima la posho za Madiwani pamoja na Wenyeviti wa Vijiji. Tuna chaguzi mbili; tuna uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Uchaguzi Mkuu. Madiwani tunafanya nao uchaguzi pamoja. Tukija kwenye suala la malipo tunawabagua Madiwani wakalipwe na Halmashauri kwenye mapato ya ndani, wakati watu hawa ndio tunaokwenda nao katika uchaguzi wetu. Ni kitu gani kinachosababisha Madiwani wetu wasiwekwe kwenye mfumo wa Serikali wa kulipwa mishahara yao na posho zao ili waweze kutimiza wajibu na majukumu yao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Madiwani leo ndio watendaji wetu wakuu kule chini. Sasa hivi tuko humu Bungeni, vikao vya Mabaraza ya Madiwani vinaendelea kule. Wao ndio wanaojua nini kinachoendelea kwenye kata zao, lakini watu hawa hawathaminiwi, tumewasahau. Namwomba Mheshimiwa Waziri na Serikali, tuone ni namna gani tunawatoa Madiwani wetu kuwaleta kwenye Serikali Kuu; mishahara walipwe na Serikali Kuu na vikao vyao pia vigharamiwe na Serikali Kuu ili tuachane na biashara ya kuendelea kuwakopa Madiwani kila mwaka na kila vikao na vikao vingine havifanyiki kwa sababu Wakurugenzi wanakuwa na kigezo cha kwamba hakuna fedha, kwa hiyo, siwezi kuitisha baraza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la Wenyeviti wetu wa Vijiji, Mitaa pamoja na Wenyeviti wa Vitongoji na Wajumbe. Watu hawa nao pia ni watu ambao wanafanya kazi kubwa sana. Tukae tukijua Wenyeviti wa Vijiji pia ndio wanaoishi huko na ardhi zetu za vijiji ambavyo leo vimekuwa na migogoro mikubwa, chanzo kikubwa pia ni Wenyeviti wetu wa Vijiji kwa sababu hawana chochote mkononi.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wanakwenda kule wanatafuta ardhi na Mwenyekiti akiambiwa bwana, Mwenyekiti mimi nina shilingi 50,000 hapa, wewe nikatie hapa kidogo tu. Mwenyekiti anaona sasa hii shilingi 50,000 wakati wewe umenisahau, nifanye nini? Anamkatia eneo pale, anachukua shilingi 50,000 yake, maisha mengine yanaendelea, tunakuja kurudi kwenye timbwili la kuanza kusuluhisha migogoro kwamba mimi nilipewa na Mwenyekiti wa Kijiji, huyu anasema hii ilikuwa ni hifadhi, huyu anasema vingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji na Wajumbe wa Vijiji pamoja na Mitaa, watu hawa tukiwatoa Madiwani wakaenda Serikali Kuu, tuwarudishe Wenyeviti wetu wa Vijiji walipwe na Halmashauri kwa sababu tunakuwa tumeipunguzia Halmashauri mzigo wa kulipa Madiwani na hivyo waende wakaanze kuwalipa Wenyeviti wetu wa Vijiji kupitia mapato ya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la ahadi ya shilingi milioni 50 kila Kijiji. Uchaguzi wa mwaka 2015 kwenye Ilani ya Chama cha Mpainduzi mliwaahidi Watanzania kuwapatia shilingi milioni 50 kila kijiji ili waweze kukuza uchumi kwenye maeneo yao.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba ahadi iliyotolewa ilikuwa ya mwaka 2015 – 2020, nasi tulienda tukawaeleza wananchi juu ya jambo hilo kwamba tuliahirisha kufanya mambo mengine. Kwa hiyo, Ilani inayotekelezwa sasa ni 2020 - 2025. Kwa hiyo, hayo ya nyuma hayako kwenye tender hiyo sasa hivi. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti Majala, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru naomba niendelee, nam-ignore tu Mheshimiwa Getere. Nimefunga, kwa hiyo, naomba aniache tu nisije nikatengua swaumu yangu. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliwaahidi wananchi wetu shilingi milioni 50 kwa ajili ya kwenda kuhuisha uchumi wao kwenye maeneo yao, lakini kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ambaye yeye ndiye anaye-deal na vijiji vyetu, sijaiona hiyo milioni 50 humu. Nakumbuka mwaka 2017, nilichangia kwenye bajeti kuu ya Serikali na nikaambiwa…

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mnzava.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nimpe Taarifa mzungumzaji anayeendelea kwamba, ahadi ya milioni 50 ya kwenye ilani ya mwaka 2015 ilitekelezwa kwa namna mbalimbali ikiwemo kupeleka mikopo kupitia fedha za mapato ya ndani ya halmashauri. Kwa sababu ya utekelezaji wa namna hiyo ndio maana wananchi walikiamini tena Chama Cha Mapinduzi kikashinda kwa kishindo kwenye uchaguzi wa mwaka 2020. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti unaipokea Taarifa hiyo?

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Hizi ahadi kila ahadi ilikuwa inajitegemea. Waliahidi vituo vya afya, waliahidi maji kumtua mwanamke ndoo kichwani, waliahidi barabara ambazo wameshindwa kuwathibitisha hata watendaji wa TARURA na waliahidi milioni 50. Kwa hiyo, tunachokitaka nataka kujua kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI milioni 50 ya kila Kijiji ambayo ilani yao hiyo, kama watakuwa wanaandika ilani kila baada ya miaka mitano wanasema hii ilipita hatuwezi kutekeleza tunaanza na mpya, Waheshimiwa basi kwa kweli, tusiendelee kuwaibia Watanzania kwa style hii, lakini kama tunaendeleza yale yaliyokuwa yamebaki…

MHE. AGNESS M. MARWA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hii itakuwa Taarifa ya mwisho. Mheshimiwa Agness Mathew Marwa.

MHE. AGNESS M. MARWA: Mheshimiwa Naibu Spika, natoa Taarifa kwa muongeaji kwanza anatoa lugha ya maudhi, lakini kingine anatakiwa ajue kwamba, mpaka sasa hivi muda bado. Mama atayatekeleza yote, kwa hiyo, aache kashfa. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti malizia sekunde zako chache zilizobaki.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikushukuru. Hata ninyi wenyewe mmepoteana huko, yaani hamjui nini ambacho mnakifanya, kwa hiyo, mimi niwashauri tu na najua Mheshimiwa Mama Samia ni mwanamke ambaye anaweza kusimama na anasimama. Nina hakika atakuwa amenisikia na atakwenda kuwapoza Watanzania hiyo milioni 50 ili isiwe ahadi ya uwongo. Naye tunamwamini na mwanamke siku zote akimuahidi mtoto wake kwamba, nitakuletea pipi, basi akitoka akirudi anakuja na pipi, atakwenda kutekeleza hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dakika chache ama sekunde chache zilizobaki, naomba niendelee na suala zima la mikopo ya akinamama, vijana na watu wenye ulemavu kama wenzangu walivyosema. Mikopo hii kwenye halmashauri zetu nyingi imekuwa ni mikopo kichefuchefu naweza nikasema. Kwanza vikundi vinavyokopeshwa vina walakini na vikikopeshwa fedha hizo hazirudi, zikichukuliwa zimechukuliwa jumla. Ukihoji hakuna maelezo yoyote ya kina ya kutosha yanayokwenda kutoa majibu kuhusiana na mikopo hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo hii tulisema tuwapatie wanawake wetu na vijana na watu wenye ulemavu ili kuweza kupunguza familia tegemezi ambazo Serikali imekuwa ikiendelea kutoa mchango kwenye kupitia mfumo wa TASAF kwenda kuzisaidia familia tegemezi ama familia maskini. Kwa hiyo, niiombe sana Wizara ya TAMISEMI iweze kuona na kufuatilia suala zima la mikopo hii ya asilimia 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa muda wako na Mungu akubariki sana. (Makofi)