Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

Hon. Tabasamu Hamisi Hussein Mwagao

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sengerema

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Sengerema naomba ushauri wangu kwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Mpango. Nimeangalia Mpango wake nimeusoma vizuri uliowakilishwa hapa na Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa niaba yake, lakini kuna maeneo ambayo nataka nipite katika kuishauri Serikali katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kelele nyingi zimepigwa na Waheshimiwa Wabunge hapa kuhusiana na TARURA, wamezungumza sana kwamba TARURA iongezewe pesa na wengine wamekwenda mbali zaidi wakitaka pesa za kuongeza TARURA zitoke katika mafuta. Sishauri mafuta yaongezwe bei kwa sababu anayeumia ni mwananchi wa chini, mwananchi maskini na mfumuko wa bei utakuwa ni mkubwa sana na sisi tunajitahidi kupunguza mfumuko wa bei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kuhusu TARURA; kwa Waziri wa Serikali za Mitaa ni kwamba TARURA wabadilishe mfumo wao kwa hiki kidogo kilichopo. Hawa ma engineer wa TARURA waliopo katika miji, manispaa, majiji na halmashauri zetu wapewe mikataba performance watakayoifanya katika maeneo yao ndiyo itakayowapa nafasi ya kurudi. TANROADS wametoa mikataba kwa ma- engineer wao wa Mikoa na wamefaulu kwa mfumo huo. Haiwezekani meneja wa TARURA anaharibu, anahamishiwa sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ushauri wangu pia kwa Waziri Mpango katika Mpango huu aliyenao na kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, hawa TARURA sasa hivi waruhusiwe kufanya kazi za force account, tutaona matokeo yake. Kwa mfano, katika wilaya yangu, halmashauri moja tu, Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema, tuna kilometa 1,730, bajeti milioni 607, haiwezekani! Ukichukua kwa bei za TANROADS ambazo zipo za mikoa, kilomita moja inaanzia milioni 15 mpaka milioni 20. Kwa hiyo, milioni 600 inatengeneza kilometa thelathini na una kilometa 1,700, kwa hiyo nahitaji miaka 50, wakati huo nitakuwa nimeshindwa uchaguzi na nimezeeka na nimestaafu. Wabunge wote hakuna atakayerudi kwa mfumo huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu, TARURA waruhusiwe kununua mitambo na mitambo yenyewe watakayoruhusiwa kununua ni mitambo mitatu tu motor grader moja, roller compactor na roller excavator, vingine vinaweza vikakodiwa. Kwa hiyo, TARURA watatengeneza barabara kwa uzuri, pesa za TARURA zitatoka wapi? Hapa ndipo pazuri, ni kwamba uwagizaji wa mafuta katika nchi hii hapa kuna tatizo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wanapeleka Muswada huu wa kuagiza mafuta kuagiza mafuta kwa pamoja 2014; Muswada huu uliletwa hapa Bungeni kwa zimamoto, mbio mbio, sasa hapa ndiyo kuna tatizo. Kwa mfano, bei ya mafuta ya Januari, bei yake ilikuwa karibu shilingi 230 au 300 kwa lita, lakini bei ambayo imeonekana ipo kwenye kukokotoa kwa EWURA, bei ya mafuta imefika shilingi 708. Katika shilingi 708 ya petrol kuna nauli iko pale shilingi arobaini na tisa na senti. Mafuta yale ya petrol yamefika hapa shilingi 757 wakati bei halisi kwa wakati huo, mwezi Januari wakati yanaagizwa, hayakuzidi shilingi 300. Sasa kama nchi inataka kufanya mageuzi makubwa ya kiuchumi, hatukwepi sasa hivi nchi kuagiza mafuta yetu kama nchi, tuna matenki tipper yana mamilioni ya hifadhi, kwa nini tusinunue mafuta kwa shilingi 300. Katika nchi ambazo zinazouza mafuta nchi za OPEC wananauza mafuta haya kwa discount.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo bei ya mafuta ni dolla 160 kwa tani ambayo ni sawasawa na Sh.370 kwa lita. Kama huyo mwagizaji anayepewa tenda anayafikisha mafuta hapa kwa Sh.708, kuna gape pale karibu ya Sh.300. Hii ni hatari sana kwa uchumi wa nchi, sisi tunalalamika hatuna pesa, halafu tunawachia watu wanaagiza mafuta. Naomba ushauri wangu uzingatiwe katika hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Fedha, Mipango na Bajeti na Kamati ya Nishati na Madini, kwa ruhusa yako pamoja na Waziri wa Uwekezaji, tukutane kwa dharura, mimi naomba, tukajadili hili kwa manufaa ya nchi. Pamoja na tozo hizi, kuna pesa ambayo ni excise duty shilingi mia tatu na kitu, kuna pesa ambazo ni levy shilingi mia tatu na sabini karibu, kuna fedha ya petrol fees shilingi mia moja. Hizi ndiyo pesa zinazokwenda Hazina, zaidi ya shilingi mia saba, lakini kuna tozo, hapa ndiyo roho yangu inaniuma, kuna tozo ya shilingi 80 ya hizi mamlaka, zimeweka hapa pesa zao shilingi 85. Tukizichambua pesa hizi zitakazobakia halisia ni karibu shilingi 60, zitolewe kwa sababu hizi mamlaka ziko chini ya Wizara ambazo zinaleta hapa bajeti zao, tunawapitishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, wapeleke kule wakapewe hela Hazina. Shililingi 60 itakayobakia hapa katika hiyo 85, ninachotaka kuomba, pesa hizo ziende TARURA, zinatosha kugharamikia barabara zetu. Haiwezekani tukaliacha hili jambo likapita na tukikutana leo kwa dharura, kesho tunakuletea majibu hapa na tunaondoa hili jambo. Tuishauri Serikali, tumshauri Mheshimiwa Mpango atengeneze bajeti, lakini kuna pesa kwenye mafuta huku zinapigwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kuna GFI, hawa GFI hawa ni watu wanaweka marking katika mafuta wanachukua shilingi 14 kwa lita. Mauzo yetu ya mafuta ni karibu ni lita milioni sita mpaka 12 kwa siku. Huyu mtu anayechukua shilingi kumi na nne anaondoka na pesa zaidi ya milioni 90, kila siku ya Mungu huyu mtu anachukuwa milioni karibu kumi na mbili kwa mwezi, kwa mwaka na gharama za marking kuweka ile dawa ya marking utaona Finland na wapi, nchi zote zinazouza zinauza gharama ndogo sana. Mtu huyu ana wafanyakazi wawili wawili kila depot katika nchi hii ambao hawazidi wafanyakazi sabini, anachukua shilingi 14.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna EWURA sijui anachukua shilingi ngapi, kuna watu wa mizani wanachukua pesa pale, kuna watu wa survey kuangalia tu mafuta yamepita kwenye bomba hii shilingi 85, mambo mengine naogopa hata kuyasema hapa kwa ajili ya usalama wa nchi, haiwezekani! Naomba turudi mezani tufukue hii kitu Waziri wa Nishati hiki kitu wakati kinapitishwa hakuwepo, Waziri wa Fedha hakuwepo, Waziri wa Uwekezaji hakuwepo. Naomba kutumia Bunge hili kwa hizi kamati tulizopo, iwe ni msaada katika nchi, turudi mezani kwa amri yako, halafu kesho tuje na majibu. Hawa watu wote ambao wanaingiza tozo zao hapa uagize waje hapa Bungeni haraka leo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Aaaaaa.

Ndiyo ninachotaka kukwambia.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Tabasam, dakika kumi zimeisha.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kukwambia pamoja na hali hii, naomba tamko lako ili tuokoe hii pesa, tupate pesa za TARURA, tutengeneze barabara zetu. Ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)