Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

Hon. Abdulhafar Idrissa Juma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtoni

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020

MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameendelea kutupa kibali cha kuwa hai na kutunusuru na mambo mbalimbali tunayoyaona na tusiyoyaona.

Mheshimiwa Spika, la pili, nikushukuru wewe, nami kwa mara ya kwanza leo nasimama katika Bunge lako Tukufu kwa ridhaa yako, nakushukuru sana. Kwa namna ya kipekee nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kilichonipa fursa ya kukiwakilisha katika nafasi ya kugombea Ubunge katika Jimbo la Mtoni; na hapohapo niunganishe kwa kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Mtoni Zanzibar kwa kunichagua mimi leo hii nikawa Mbunge katika Bunge lako Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa mara ya kwanza nikisimama leo hii nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Mtoni. Imani waliyoiwekeza kwangu sina mashaka yoyote kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu nitailipa kwa kuwatumikia wao na Watanzania wote kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nianze kwanza kwa kuunga mkono hoja na kuipongeza hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini hapohapo naendelea kumpongeza kwa kuendelea kuwa Mwenyekiti mwema wa chama ambacho kinaiongoza Serikali hii.

Mheshimiwa Spika, mimi binafsi kwa niaba ya wananchi wenzangu wa Jimbo la Mtoni, tulifarijika sana pale ambapo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliposema wazi ndani ya Bunge hili Tukufu akituhutubia sisi na akilihutubia Taifa hili kwamba katika awamu yake hii anaendelea kuahidi kuulinda Muungano wa Tanzania kwa gharama yoyote; tulifarijika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sisi kule Zanzibar Mapinduzi kwetu ni jambo la mbele yawezekana kuliko uhai wa mtu mmoja mmoja kwa maslahi ya Taifa hili, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kusema tena wazi kwamba Mapinduzi ya Zanzibar yataendelea kulindwa na kuheshimiwa katika utawala wake; tunampongeza sana katika hotuba yake hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nizungumze kwa uchache sana lile ambalo pia nimedhamiria kulichangia kwa maslahi hasa ya wananchi walionituma katika Bunge hili, wananchi wa Jimbo letu la Mtoni. Jimbo letu nasi linapakana na bahari, moja ya mambo ambayo Mheshimiwa Rais ameyasema atayasimamia na Serikali hii ya Awamu ya Tano katika kipindi cha pili tutayaona ni kuimarika uvuvi wa Bahari Kuu.

Mheshimiwa Spika, Uvuvi wa Bahari Kuu ni moja kati ya Sekta za Muungano. Ni kweli bado kwa nguvu zetu za ndani hatujafanya vizuri sana katika uvuvi wa Bahari Kuu, lakini pia Bunge lako tukufu hili katika mwaka 2018 moja ya ripoti za Kamati zilisema wazi kwamba kama tukiwekeza vya kutosha katika Bahari Kuu, Taifa letu linao uwezo wa kupata takribani bilioni 350 kila mwaka kutokana na uvuvi wa Bahari Kuu. Sina mashaka yoyote kwa haya yaliyosemwa 2018 yalitoa dira kwa Chama Cha Mapinduzi kuweka katika Ilani yetu, lakini yalitoa dira kwa Rais wetu kuja kuyazungumza mbele ya Bunge hili Tukufu na hivyo kuwahakikishia Watanzania kwamba meli nane za uvuvi katika Bahari Kuu zitakuja katika awamu yake hii ya pili.

Mheshimiwa Spika, sisi kule Zanzibar, hasa wananchi wa Mtoni, tumefarijika sana kwa sababu meli nne katika hizo, bila kuficha maneno Rais amesema hizi zitakwenda kufanya uvuvi wa Bahari Kuu Zanzibar na sina mashaka yoyote itachochea uchumi wa Zanzibar na wananchi wenzetu katika majimbo yetu kwa kule Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, Zanzibar sisi bahari ni kitu muhimu sana na eneo la bahari ni kubwa kuliko eneo la ardhi ambalo Mungu ametutunuku. Kwa hiyo kivyovyote Bahari Kuu ni kubwa kuliko bahari ndogo ambayo kwa sasa inatumika na inaleta maslahi kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa kule Mtoni wameniagiza niseme katika Bunge hili na nichangie hotuba hii kwamba ujio wa meli ile ama meli hizo zitakapofika hawaoni tu mabadiliko ya uchumi wa mtu mmoja mmoja lakini wanaona mabadiliko ya kifikra kwa wawekezaji wetu na wao sasa kuanza kuwekeza kwa kuleta meli zenye uwezo wa kuvua Bahari Kuu na hivyo kuongeza ajira kwa wananchi wetu wa ndani lakini kuongeza pato la fedha za kigeni kupitia kuuza samaki hawa nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kuipongeza hotuba ya Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo imejipambanua wazi kupambana na masuala ya kifisadi katika awamu hii ya pili. Ni kweli vijana wengi ama fursa nyingi za ajira zimejitokeza katika awamu iliyopita na tunatumai yale tuliyoahidi na yaliyoahidiwa na Ilani ya Chama chetu, Serikali yetu kupitia Rais wetu aliyo madarakani itayatizmiza kwa kuendelea kupambana na ufisadi.

Mheshimiwa Spika, tukipambana na ufisadi zile ajira milioni nane tulizowaahidi Watanzania katika ilani yetu, na chini ya usimamizi wa Dkt. John Magufuli, tuna uhakika zitatimia. Viongozi wenzetu katika Serikali mkimsaidia Mheshimiwa Rais kusimamia mianya ya upotevu wa fedha, hali za wananchi wetu zitaendelea kuimarika, fursa za Taifa hili kwa vijana zitaendelea kuimarika na sisi viongozi tuko tayari kuendelea kushirikiana na Serikali; na wananchi wa Jimbo la Mtoni wamenielekeza nimalizie kwa kusema wataendelea kuiunga mkono Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iyatende yale ya Muungano kwa maslahi ya Wazanzibari na Watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)