Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021 – Ofisi ya Waziri Mkuu

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye hotuba ya Waziri Mkuu. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri ambapo imeeleza mambo mengi kwa kweli ambayo yamefanyika na mengi ameyachukua yaliyofanyika katika kipindi cha miaka mitano ambayo amepewa dhamana na Serikali ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Spika, nitoe pole kwa tatizo la Corona linalotukabili Watanzania. Naamini Mwenyezi Mungu atatuepusha pamoja na kuchukua tahadhari mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2015, Chama cha Mapinduzi tulitengeneza Ilani ya Uchaguzi. Wakati tunaitengeneza Ilani tuliweka kazi zitakazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano. Tulipoikamilisha tukaanza kumtafuta mtu atakayefanya kazi tuliyoiweka kwenye Ilani. Wakati ule walijitokeza watu wengi walioomba kazi hiyo na Chama cha Mapinduzi mwishoni tukamteua Mheshimiwa John Pombe Magufuli kufanya kazi ya kutekeleza Ilani. Hakuteuliwa kwa bahati mbaya, tuliona ana uwezo wa kuifanya kazi tunayompa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haikuwa bahati mbaya, chama hiki ni kikubwa sana. Tulitengeneza kazi, tukamtafuta mtu mwenye uwezo, jasiri, mzalendo ambaye atakwenda kutekeleza kazi tuliyompa. Sina mashaka chama hiki kikifanya tathmini leo tuliyempa kazi ameifanya vizuri na hivyo anastahili kupewa tena miaka mingine mitano ya kukamilisha kazi tuliyompa lakini pia tumpe nafasi nyingine kwa sababu amefanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitapitia maeneo machache. Eneo la kwanza, Ilani ya Uchaguzi ilimtaka huyu tutakayempa kazi yeye na Serikali yake, wafanye kazi ya kutafsiri ukuaji wowote wa uchumi kwenye maisha ya kawaida ya Watanzania. Kazi hii imefanyika vizuri sana kwa takwimu ambazo zimo ndani ya hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza lilikuwa ni kwenye afya. Kwenye afya tulitaka tusogeze hizi huduma za afya na kuziboresha. Katika kipindi cha miaka mitano Serikali ya Awamu ya Tano imejenga vituo vya afya 352. Kama uchumi usingekuwa una-perfom isingewezekana kufanya kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki cha miaka mitano zimejengwa hospitali 67 za Wilaya. Hata Jimbo langu la Mtama siyo Wilaya lakini tuna Hospitali ya Wilaya. Kazi hii imefanyika vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna mikoa mipya ambayo ilikuwa haina Hospitali za Rufaa. Mikoa ya Njombe, Songwe, Katavi, Geita na Simiyu zimejengwa Hospitali za Rufaa na kazi inaendelea vizuri. Pia zimejengwa Hospitali tatu za Kanda: Kanda ya Kusini tuna Hospitali Mtwara; Kanda ya Magharibi tuna Hospitali Tabora; na Kanda ya Ziwa inajengwa hospitali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kazi hii, sina mashaka chama changu kitampa fursa tena Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli awe mpeperusha bendera mwaka huu. Sina mashaka kwamba Watanzania wameona tafsiri ya kukua kwa uchumi kwenye huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wa umeme, nilikuwa naangalia takwimu mpaka asubuhi tayari tumeshakwenda kwenye vijiji zaidi ya 9,000. Vijijini kabisa umeme unawaka. Kama uchumi ungekuwa hauendi sawa kazi hii isingewezekana. Kazi hii imefanyika vizuri tafsiri yake ni kwamba maisha ya watu yanabadilika, inaonesha kwamba kuna kazi nzuri ya uchumi inakua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, elimu, kila mwezi zinatolewa zaidi ya shilingi bilioni 24 kwenda kwenye elimu bure. Tulisema kwenye Ilani ya Uchaguzi tutatoa elimu bila ada shilingi bilioni 24 kila mwezi zisingewezekana kama siyo kazi nzuri ya kutafsiri ukuaji wa uchumi kwenye maisha ya kawaida ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye maji kuna takwimu nyingi nzuri. Kwenye maji kuna ujenzi, ukarabati na upanuzi wa miradi mbalimbali ya maji, Arusha, Babati, Dodoma, Kigoma, Iringa, Lindi, Musoma, Morogoro, Moshi, Mtwara, Mwanza, Sumbawanga, Shinyanga na mingine mingi. Kama isingekuwa uchumi umekwenda ndiyo maana fedha zikapatikana kupelekwa huko, kazi hii isingewezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili la kwanza tulimpa Mheshimiwa Dkt. Magufuli alifanye. Mimi kama Mwenezi Mstaafu wa Chama ambaye nilisimamia utengenezaji wa Ilani ya Uchaguzi nataka niseme kazi imefanyika vizuri na tuna sababu ya kumpa tena fursa Mheshimiwa John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu ni wakati mzuri wa kufanya tathmini. Kazi ya pili, kwenye Ilani ya Uchaguzi tulimpa Mheshimiwa Magufuli kazi ya kubadilisha utamaduni wa namna tunavyofanya mambo kwenye nchi yetu. Ndiyo maana tukawa na kauli mbiu ya Hapa Kazi Tu, wapo watu wengi pengine hawajui. Tuliiweka kwa makusudi kwa sababu ulianza kujengeka utamaduni, mtu unaweza ukawa unafanya kazi unapata kipato kikubwa hakilingani na kazi unayoifanya. Wakati mwingine biashara hewa au kazi hewa, tukasema lazima tubadilishe utamaduni huu ili nchi yetu iende.

Mheshimiwa Spika, kwenye uchumi ndiyo vyuma vinakaza lakini vinakaza kwa sababu wakati mwingine tulizoea dili, dili zikifungwa kwa vyovyote vile vitakaza. Kwa mujibu wa Ilani ya Uchaguzi ukisikia kelele maana yake kazi hii imefanyika vizuri. Ndiyo maana itabidi tumpe fursa tena kwa miaka mingine mitano amalizie kazi ambayo alikuwa ameshaianza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye siasa, siasa na yenyewe ilishazoea hivyo hivyo, kuna kelele ndio lakini leo ukiangalia namna tunavyofanya tumekuwa more serious. Nimeona watani zangu CHADEMA wamefanya Uchaguzi, angalia uchaguzi walivyofanya, angalia walivyofanya ACT kwa vyovyote vile kuna mabadiliko hata kwenye namna ya kuendesha siasa zetu ambayo naamini ni kazi nzuri ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nina-recommend kwamba kwa kweli Mheshimiwa Magufuli na Serikali yake wamefanya vizuri. Nimpongeze Waziri Mkuu, Makamu wa Rais, Mawaziri, Watendaji wa Serikali, Vyombo vya Ulinzi na Usalama wameitendea haki Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata mtaani hali imebadilika, watu kidogo wako serious, hii ndiyo kazi tuliyomtuma Mheshimiwa Magufuli. Mwalimu alituambia ukiwa unasafisha nyumba unaweza ukafagia shilingi, kufagia shilingi hakufanyi nyumba isisafishwe. Mimi naamini upungufu wa hapa na pale katika kutengeneza mambo haya tukakanyagana vidole yatumike vizuri kutusaidia turekebishe mambo siku za usoni ili Tanzania iendeleee kuwa nchi njema ya fursa ya kila mmoja. Kwa hiyo, kwa kweli niipongeze sana Serikali kwa kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu nikupongeze Bunge la Kumi na Moja limefanya mabadiliko makubwa sana ya namna ya kuendesha mambo kutoka Bunge la analojia kwenda Bunge la digitali na mengine mengi ambayo umeyafanya. Utakumbuka Bunge hili la Kumi la Moja ulifanya uamuzi wa kijasiri hapa wa kuamua kuanzisha studio ya Bunge ambayo ni uamuzi ulifanywa na Bunge la Kumi, ukaamua sasa twende tutekeleze. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni katika mambo matatu. La kwanza, nimeangalia kwenye randama ya Bunge, nilidhani ni vizuri tukaitengea fedha studio ya Bunge ili ifanye kazi vizuri zaidi. Kwa sababu huyu ni mtoto wako, umemsimamia wewe ndani ya Bunge hili, tusipomtengea fedha ya kutosha bado mambo hayatakwenda sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, tusimuache nyuma kwenye mabadiliko haya ya teknolojia unayoenda nayo na wao tuwape vifaa vya kisasa ili waweze kufanya kazi vizuri. Hii kazi umeisimamia wewe na mimi naamini wananchi wa Kongwa watakuchagua tena urudi uje ukamilishe kazi hii uliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu kwenye studio ya Bunge, nimeona tumeanza kupitia Kanuni za Kudumu za Bunge, si vibaya tukazungumzia Kanuni ya kuendesha hii studio ya Bunge nayo ikawa sehemu ya Kanuni za Kudumu za Bunge ili mambo yakaenda vizuri zaidi. Tupanue wigo ikiwezekana tukafanye coverage hata kwenye Kamati za Bunge na kwenye shughuli mbalimbali za Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia 100 na naipongeza Serikali kwa kazi nzuri waliyofanya. Ni matumaini yangu Chama cha Mapinduzi kitasimama tena na Mheshimiwa Magufuli, ni matumaini yangu Watanzania watamchagua tena turudi kufanya kazi ambayo tulimpa mwaka 2015. Ameifanya vizuri kwa miaka mitano, tumuongezee miaka mingine mitano akamilishe kazi tuliyomtuma. Ahsante sana. (Makofi)