Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini

Hon. Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Madini

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nianze kumshukuru Mungu kwa siku hii ya leo, lakini vilevile nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Madini pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo wamefanya na hivyo kuifanya Tanzania kufaidika na madini kama ambavyo imekuwa ikitarajiwa.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchangia katika maeneo machache kama ifuatavyo na ikizingatiwa kuwa hayo maeneo pia yanahusu Wizara ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Spika, suala la Mgodi wa TANCOL; ni kweli katika maneno ambayo yamezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge kwamba Tanzania tunawekeza na tunawaleta wawekezaji kwa lengo la kuhakikisha kwamba kunakuwa na tija na mafanikio ya kifedha, lakini vilevile mafanikio mapana katika uwekezaji unaofanyika. Katika mradi wa TANCOL, mafanikio tuliyoyapata ni kwamba mpaka sasa makaa ya mawe ambayo yanatumika katika viwanda vyetu hususan vya cement yote yanatoka Tanzania na mengine tumekuwa tukiuza hata nje ya nchi, kwa hiyo yameleta faida katika kuwezesha kupata malighafi katika viwanda vyetu vya cement.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, nikiri tu kwamba taarifa ambayo ilikuwa inazungumzwa ambayo imetokana na taarifa ya CAG, sisi kama Wizara tunayo na hatujaifumbia macho. Tayari tulishaunda Kamati ya kufuatilia namna gani tunatekeleza maoni ya CAG na kupata ni namna gani au kwa kiasi gani yashughulikiwe. Kwa hiyo, kuna mambo ambayo yanatakiwa yashughulikiwe katika mpango wa muda mfupi lakini mengine yalikuwa yanahitaji tafakari pana zaidi kwa muda mrefu. Suala hilo lipo katika mikono salama na niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge pale tutakapokuwa tumekamilisha hayo tunayoyafuatilia watapata taarifa ambayo inakusudiwa.

Mheshimiwa Spika, vilevile niseme tu kwamba, wao wenyewe TANCOL pamoja na kampuni zile ambazo walikuwa wanazitumia katika kuwezesha kutoa huduma wamekuwa na migogoro. Kwa mfano, katika Kampuni ya Caspian walipelekana mpaka mahakamani lakini wakaamua kufanya makubaliano nje ya mahakama na hivyo wakakubaliana kulipa zaidi ya shilingi milioni nane kwa ajili ya hayo makubaliano yao na hasa katika lengo la kuvunja mkataba wa kuendelea kuchukua huduma kwa hao Caspian. Kwa hiyo hayo ni mambo tu ambayo yalikuwa yanajitokeza katika migogoro iliyokuwa inaendelea. Niwahakikishie tu Wabunge kwamba kwa hali iliyopo sasa kwa Serikali hii ya Awamu ya Tano hatutakubali uwekezaji wowote usio na tija na hivi wote tunaangalia Taifa letu katika mtazamo huo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Mchuchuma na Liganga ni kwamba kweli huyo mwekezaji alipatikana na makubaliano ya awali yalikuwepo na hata kwa upande wa nchi kama Serikali tayari tulianza hata kuwekeza katika miundombinu kama ya barabara ili kuwezesha mradi huo uweze kuanza, lakini kama ambavyo nimezungumza na sheria ambazo tulikuwa tumetunga za kusaidia nchi inufaike zaidi na rasilimali zake, tulikuja kuangalia na tukaona kwamba katika baadhi ya taarifa ambazo mwekezaji alikuwa amezitoa hasa kuhusiana na madini zilizokuwepo zinaonekana haziendani na uhalisia kulingana na taarifa zingine tulizozipata kupitia utafiti wetu wa source nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa misingi hiyo, vilevile hata katika upande wa kuchukua mikopo, mwekezaji alizungumza kwamba ili apate mikopo kwa kupitia dhamana ya mashapo yaliyopo, sasa kama ndivyo yeye amekuja na nini? Kama dhamana inatokana bado na rasilimali ile ile ambayo tunayo sisi wenyewe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kuna mambo ambayo inabidi tuendelee kuongea na mwekezaji, tuweze kutafakari kama tutakuwa tumekubaliana basi ataendelea na kazi, lakini kama tutakuwa hatujakubaliana na pale Serikali inapoona kwamba hapa hakuna tija ya huo uwekezaji, basi sisi tuwaambie tu kwamba hatutakubali kuendelea nae kwa sababu msiimamo wa nchi utabakia vilevile kwamba kila uwekezaji lazima uwe na tija na manufaa mapana ya wananchi lakini pia na upande wa muwekezaji kuwe na win win situation. Kwa hiyo, hiyo ndiyo hali halisi na sisi hatutakubali kuja kuwajibika hapa kwa sababu eti tuliwekeza tu kwa ajili ya kuwafurahisha watu. Lazima tujipange kwa kupata ufumbuzi wenye tija.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno haya, naunga mkono hoja. Ahsante sana.