Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Kuridhia Itifaki ya Kinga na Maslahi ya Kidiplomasia ya Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (The East Africa Community Protocol on Information and Communication Technology)

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Kuridhia Itifaki ya Kinga na Maslahi ya Kidiplomasia ya Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (The East Africa Community Protocol on Information and Communication Technology)

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nitajitahidi, naomba kuchukua fursa hii kwanza kukushukuru mwenyewe kwa kuongoza kikao hiki, lakini pia kuwashukuru Wabunge waliochangia na Wabunge wote lakini pia nimshukuru Mheshimiwa Mbena kwa maoni ya Kamati na Mheshimiwa Salome Makamba kwa maoni ya Kambi ya Upinzani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru Mheshimiwa Ruth Mollel, Mheshimiwa Daniel Nsanzugwanko, Mheshimiwa Cosato Chumi na Mheshimiwa Almas Maige.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuanza na jambo ambalo wewe, unalifahamu vizuri zaidi kwa sababu wakati huo ulikuwa Mwanasheria wa Serikali. Jumuiya ya Afrika Mashariki ya zamani ilivunjika mwaka 1977 na ni vyema tukasema ukweli mpaka Jumuiya ya Afrika Mashariki inavunjika nchi ya Uganda iliendelea kutoa michango yake yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nchi ya Uganda, chini ya Iddi Amin iliendelea kutoa michango yake yote mpaka Jumuiya inavunjika, ni ukweli wa Kihistoria kwamba nchi ambayo haikutoa michango yake kabla ya hapo inafahamika, lakini baada ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kuvunjika katika namna ile iliyovunjika na Tanzania kulazimika kufunga mpaka na Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jitihada zilifanyika chini ya aliye chaguliwa kuwa msuluhishi na Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa aliyeitwa Victor um Rishi ambaye nina hakika unamfahamu na mlikutana na mimi nilipata bahati ya kufundishwa na Victor um Rishi mwaka 1984 nilipokwenda kusomea kozi ya mambo ya Diplomasia Mjini Cairo nchini Misri na nchi hizi zikakubaliana katika kitu kilichoitwa The East African Community Mediation Agreement ya mwaka 1984.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika makubaliano hayo, waliangalia net assets na net liabilities na baada ya hapo, mali lazima ziendelee kuwa mali za jumuiya, mali za pamoja ingawa jumuiya imevunjika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakumbuka, Benki ya Maendeleo ya Afrika Mashariki iliendelea kuwa ni mali ya pamoja, pamoja na jumuiya kuvunjika na ilikuwa Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili, Soroti Flying School ya kufundisha marubani ilibaki Uganda na ikawa mali yetu wote. Tatu, Interuniversity Council for East Africa, nayo ilibaki Uganda. Kwa hiyo, baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, mali zilizobaki kuwa zetu wote, baada ya usuluhishi wa Dkt. Victor Umbricht, zote zilikuwa Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye East African Development Bank, ilikubaliwa kwamba daima Mwenyekiti na Mkurugenzi Mtendaji atatoka Tanzania. Akawa Idd Simba, akawa George Mbowe. Nilitaka niweke rekodi hii vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ambayo katika net assets haikufaidika ni Uganda na ndiyo maana ndani ya mkataba ule, ilikubaliwa tuwe na compensation to Uganda for short fall of net assets, interest payments; na Kenya na Tanzania tulipewa viwango vya kuifidia Uganda na kama tutashindwa kuifidia Uganda, tutalipa riba ya asilimia saba. Wewe ulihusika, katika hilo. Nilitaka lieleweke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mkataba huo kusainiwa mwaka 1984 na unafahamu haikuwa rahisi, nchi iliyotoa ushirikiano mkubwa ilikuwa ni Uganda. Ndipo kila nchi mwanachama, kama tunavyofanya leo, ilipeleka katika mabunge yake sheria ya kuridhia The East African Mediation Agreement. Kenya walifanya hivyo mwaka 1985 chini ya The East African Mediation Agreement Act Cap 4 of The Laws of Kenya. Tanzania ilifanya hivyo hivyo, chini ya The African Community Mediation Agreement Act, ya mwaka 1987 ambayo ni sura ya 232 ya sheria za Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nimeanza na hiyo? Hakuna ombwe panapotokea mgogoro hata kama mkataba huo na sheria hiyo haijatamka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana wewe pia ulihusika ukiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Mkataba wa sasa, The Treaty of the Establishment of the East African Community ya sasa, is a framework agreement. Kila jambo tutakalotaka kulitekeleza, lazima tujadiliane itifaki, kwa sababu tulianza kwa kutokuaminiana baada ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 1977 kuvunjika. Ndiyo maana itifaki hii inazungumza maslahi na kinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitaka kujua nini kitatokea Jumuiya ya Afrika Mashariki ikivunjika, rudi kwenye treaty, soma Ibara ya 145, 146, 147 na 149. Kwa pamoja zinaeleza nini kitatokea, siyo tu Jumuiya ya Afrika Mashariki ikivunjika, lakini nchi ikijitoa. Chini ya Ibara ya 145 ya mkataba wa sasa, nchi ina haki ya kujitoa na chini ya Ibara ya 146, nchi inaweza ikasimamishwa uanachama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyote hivyo vikitokea, tukienda kwenye Ibara ya 149, ndiyo tunajua nini hatima ya mali zilizomo? Kwa nchi iliyojitoa yenyewe kwa hiari yake, kwa nchi iliyosimamishwa uanachama, vyote vipo na hilo ndilo lililomfanya Dkt. Victor Umbricht kuandika kitabu kuhusu Multilateral Mediation, Practical Experience and Lessons, cha mwaka 1989; Mediation Cases, The East African Community and Short Commence on Mediation Efforts Between Bangladesh, Pakistan, India, Vietnam, USA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, likitokea hilo ambalo hatutarajii litokee tena, kwa sababu sasa mwaka huu tunasherekea miaka 20. Ile ilikufa ndani ya miaka 10; likitokea, utaratibu wa Kimataifa upo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, wewe ulikuwa ni mmojawapo na sisi wengine tulikuwa tunasaidia, tulihakikisha mkataba huu wa sasa, unatungwa kwa namna ambayo tutajenga imani kila siku zinapoendelea. Kwa hiyo, niwahakikishie, huu mkataba ni kwenye haki, maslahi na kinga, lakini tuusome pamoja na treaty nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, ndani ya kipindi hiki cha miaka 20, tumejenga jumuiya imara na ili jumuiya hii iendelee kuwa imara ni lazima ibebwe na misingi miwili; pragmatism and flexibility.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Sudani ya Kusini; nchi zote zinazojiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki baada ya nchi tatu zilizoianzisha, ni lazima ziingie kwenye kitu kinaitwa, Accession Treaty. Kuna Accession Treaty kati ya Jamhuri ya Rwanda na Jumuiya ya Afrika Mashariki; na Accession Treaty kati ya Jamhuri ya Burundi na Kumuiya ya Afrika Mashariki; na hivyo hivyo Accession Treaty kati ya Jamhuri ya Sudani Kusini na Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Accession Treaty, ili nchi hiyo iweze kufungwa na mikataba yote inayoikuta wakati inajiunga na jumuiya hiyo. Kwa hiyo, hapa ni kukwepa lile suala la retrospective application, kwamba kwa kuingia mkataba siku ile, moja ya vifungu ni kwamba, ninafungwa na yale yote niliyoyakuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Sudani imefungwa na mambo yote iliyoyakuta, lakini ndani ya mkataba huo na sisi na Sudani ya Kusini, kipo kipindi cha mpito, Sudani ya Kusini imepewa kipindi cha mpito lakini inafungwa na yale yote iliyoyakuta kwa sababu imeasaini The Accession Treaty kama Burundi na Rwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jumuiya hii pia tuna ile tunasema dhana ya undugu (solidarity principal) na nchi ya Sudani Kusini, inahitaji kipindi cha mpito kwa sababu nyote mnafahamu hali ambayo Sudani ya Kusini imepitia. Sudani ya Kusini imekuwa katika migogoro iliyonayo toka mwaka 1956 mpaka leo. Kwa hiyo, haya mnayoyaona kwamba Sudani inakwenda taratibu, haifanyi makusudi, lakini ni kwa sababu imeomba iwe na kipindi cha mpito, kuiwezesha kuunda taasisi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, katika mfumo wake wa kodi na mamlaka ya kodi, Sudani ya Kusini inasaidiwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wanafunzi wake wanasoma katika Chuo cha Kodi na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kuwasaidia kuwa na mfumo huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalize la wafanyakazi wa Afrika Mashariki. Kwanza tufahamu katika ule mkataba wa Umbricht, Sura ya 10, ilieleza kuhusu National Provident Fund ya watumishi wote wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na fedha yao yote ambayo ilikuwa imetunzwa Uingereza kwenye Crown Agency, na fedha hizo zilitumwa kwenye kila nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Tanzania tulikuwa na wafanyakazi 31,831 na hawa waliingia katika makubaliano na Serikali walipwe shilingi bilioni 111 kwenye deed of settlement na wafanyakazi hao walilipwa wote na walipewa miezi sita kwa yule ambaye hakuridhika, apeleke malalamiko, hakuna aliyepeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya miezi sita, wakajitokeza wafanyakazi 5,598, wakidai shilingi trilioni 2.15, wakaenda Mahakama Kuu, wakashindwa; wakaenda Mahakama ya Rufaa, wakashindwa; wakaenda kwenye East African Court of Justice, wameshindwa. Kwa hiyo, Serikali ilishatekeleza jukumu lake la kuwalipa fedha kwa mujibu wa Deed of Settlement na maadamu wameshindwa kwenye Mahakama zote, Serikali haiwezi kutoa hisani zaidi ya hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali haidaiwi hata senti tano. Orodha ya wafanyakazi wote ipo kutoka Crown Angency, walio hai na walikufa. Wamechukua haki yao Mahakamani, wameshindwa. Kwa hiyo, tuweke rekodi sawa, hakuna mfanyakazi wa iliyokuwa Jumuiya ya Afrika Mashariki anayeidai Serikali fedha yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nahitimisha kwamba, naomba kutoa hoja.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.