Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Katani Ahmadi Katani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tandahimba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema lakini nikushukuru wewe pia kwa kunipa nafasi hii kuchangia mapendekezo ya mpango huu. Niende moja kwa moja kwenye suala la kilimo ambapo ndio pananigusa sana kwa sababu natoka sehemu ya kilimo. Ukisoma mapendekezo ya mpango ipo sehemu inazungumzia kujenga maghala kwenye mazao ya mpunga lakini niliwahi kutoa pendekezo mwaka jana na leo narudia tena wakati anachangia Mheshimiwa Musukuma alisema ipo miradi inapelekwa maeneo ambayo haina return binafsi nilimwelewa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo unajenga soko lakini return ya soko unalolijenga inarudi kwa muda gani, kuna eneo kama Tandahimba ambalo tunazungumza la korosho unashindwa kupeleka fedha ya kujenga ghala wakati kutunza korosho ghalani ni shilingi 38 kwa kilo moja. Yaani ukiwekeza bilioni 5 Tandahimba return yake kwa Serikali ni miaka miwili kama umewapa mkopo wanakuwa wamerejesha hiyo fedha. Lakini unapeleka kujenga soko sehemu ambayo hakuna hata wafanyabiashara wenyewe. Nilizungumza hizi mwaka jana na leo narudia tena kwenye huu mpango mnazungumza kujenga maghala ya mpunga kwenye kuhifadhi korosho ghalani shilingi 38.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tandahimba wakizalisha tani 74,000 kama walivyozalisha msimu iliyopita maana yake wanakusanya bilioni 2 na milioni mia nane na, ukipeleka fedha hii inaweza kurudisha kwa miaka miwili tu. Niwaombe kwenye mpango wenu muangalie factor hizi mupeleke fedha maeneo ambayo wanaweza kuzirejesha kwa wakati zikaenda kutawanywa maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo hapa nataka nilikumbushe sitaki kukumbusha yaliyopita lakini nikumbushe kwenye bajeti ya mwaka jana wakati tunabadilisha sheria ya fedha ile ya korosho sheria namba 203 ninukuu maelezo ya Waziri wa Fedha alisema “ kufatia pendekezo hili shughuli za uendelezaji wa zao la korosho pamoja na gharama za uendeshaji wa bodi ya korosho zitagharamiwa kupitia bajeti ya Serikali chini ya usimamizi wa Wizara ya Kilimo kama inavyofanyika hivi sasa kwa mazao mengine ikiwemo pamba, kahawa na pareto.” Jambo la kusikitisha tarehe 07 mwezi wa Kumi tulivyokuwa kwenye kikao cha wadau pale, bodi ya korosho na wizara imeleta mapendekezo kwa wadau ya mkulima kukatwa shilingi 25 kupeleka TARI Naliendele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkulima akatwe 25 kupelekwa Bodi ya Korosho, OC ya bodi ya korosho itozwe kwa mkulima na haya yalikuwa ni maelezo mazuri ya Waziri japo mwanzo tulikuwa tunafanya argument ya kukataa ile 15% kwamba ibaki bodi ya korosho lakini Serikali ilivyoshawishi tukakubali tukaona kabisa kwamba hiyo 15% ya export levy ambayo inapoinunua korosho leo 2700 maana yake kuna zaidi ya 380 na inakwenda kwenye mfuko mkuu, leo wanakatwa mkulima shilingi 50 inakwenda TARI ambayo mmeingia makubaliano na Ox-farm mnapata zaidi ya bilioni 70 leo mnakwenda kumnyonya mkulima huyu tena. Kikao kimekataa lakini wizara mnasema mmetumwa na wakubwa, wakubwa gani ambao hawana huruma na mkulima? Ni wakubwa gani ambao wamewatuma ambao hawana huruma na mkulima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana kwenye mapendekezo ya mpango mwaka jana mmezungumzia uzuri mara nyingi tunaenda mbele tunarudi nyuma. Ni mwaka juzi Waziri Mkuu alisimama hapa akasema kumwondolea mzigo mkulima anaondoa tozo tano, tozo tano leo zimerudi tena mkulima yupi anayesaidiwa Tanzania? Niombe sana kwenye mpango huu tunapotafakari mapendekezo ya mpango wa maendeleo tuguse maslahi ya watu kwanza.

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa

T A A R I F A

MWENYEKITI: Mheshimiwa Katani kuna taarifa, Mheshimiwa Naibu Waziri kifupi

NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. HUSSEIN M. BASHE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi tu nilitaka nimpe taarifa ndugu yangu Katani kwamba tozo hii imejadiliwa kwenye kikao cha wadau ni kwa mujibu wa sheria na hakukuwa na mkubwa yoyote aliyeongoza kile kikao, kikao kile kiliongozwa na wadau wa kilimo.

Kwa hiyo, hakuna maagizo kutoka kwa mkubwa yeyote. Kama kuna any concern kuhusu tozo hii, utaratibu upo wazi, kikao cha wadau kikae kifanye maamuzi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Katani unapokea hiyo taarifa?

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake lakini pia na wewe nataka upate uelewa pia. Wadau wanaozungumzwa ndio walikataa kwenye kikao na clip ya audio ya mazungumzo yale yapo hili ni jambo limeletwa na Serikali sio jambo ambalo wadau wamelipitisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unayo Mamlaka, unayo nafasi tukisubiri wadau tu, wadau ndio walileta baadhi ya sheria ambazo tunazibadilisha humu, wadau hao ndio wamekataa, huu ni mpango wa Serikali kutaka kumnyonya mkulima, tusitengeneze maneno mengine. Wabunge walikuwepo hao waulize wote tulikataa pale sasa hili ni jambo ambalo inawezekana ulikuwa hulijui, nimeamua niliweke hapa kwa sababu nimeona kwenye suala la mapendekezo ya mpango na hili lilizungumzwa na Serikali mwaka jana vizuri kwamba fedha za bodi zinatoka wapi, fedha za kuendeleza zinatoka wapi hao TARI wana bilioni 70, dola milioni 32 ox-farm wameshafikia makubaliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo unakwenda kwa mkulima huyu mnyonge na ninyi mawaziri mnajua kwamba tunatoka kwenye mazingira magumu mliangalie hili kwa namna pana sana wala halihitaji majibu ya mhemuko, linahitaji kufanyiwa kazi kwa kuwajali wakulima wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli ana dhamira njema na wakulima. Waziri Mkuu ametoa tozo ambazo zimerudi hapa kwa namna nyingine, kwa mlango wa nyuma. Naomba sana, kwenye mapendekezo haya ya mpango mwangalie mambo ambayo yanaweza yakatupa tija kwa maslahi ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, mimi natoka vijijini. Naendelea kuungana na wenzangu walioshauri, fedha zile zinazokwenda TARURA kwa kweli hazikidhi mahitaji. Mfano mzuri, leo ukienda Jimboni kwangu ambako korosho zinatoka vijijini ili zifike bandarini pale, vijiji vile havipitiki. Fedha zinazokwenda TARURA, mbovu. Toka Nanyanga, pita pale unaenda Mdimba barabara haipitiki, lakini ni sehemu ambayo uzalishaji wake wa korosho wanazalisha zaidi ya tani 3,000 za korosho kwenye kata moja, lakini barabara ni mbovu, magari yanachakaa.

Mheshimiwa Spika, sasa badala ya kuzipeleka fedha TANROADS kuwe na uwiano aidha unaofanana, nusu kwa nusu; nusu mpeleke TARURA kwa sababu wanahudumia wananchi wengi kuliko hata TANROADS ambayo tunaitumia au 60 kwa 40. Asilimia 60 iende TARURA ili barabara za vijijini nazo ziweze kupitika. Mtakuwa mmewasaidia Watanzania wengi kuliko sisi ambao tunapata fursa tunapita kwenye ndege, siku nyingine kwenye magari, lakini vijijini wao kila siku shughuli zao zinahitaji barabara ziwe zinaboreshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tafakari kwenye hili ikiwezekana mnavyoleta Mpango wenyewe sasa, basi tukute TARURA inakwenda asilimia 60, TANROADS inabaki asilimia 40 ili tusogeze mbele gurudumu la maendeleo la Taifa letu. Ahsante sana. (Makofi)