Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kumshukuru Mwenyezi Mungu, kunipa afya leo naongea mbele ya Bunge lako Tukufu. Pili, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Mpango kwa kazi kubwa aliyoifanya na ninajua kazi hiyo inaakisi kazi kubwa inayofanywa na Serikali nzima ya Awamu ya Tano, ikiongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, nawapongezeni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli, katika vipaumbele ambavyo umetuletea, kama rasimu, nimevisoma sana, umesheheni vyote, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, niombe mambo machache, mengi yamesemwa na wenzangu, lakini ninayo machache, kama utapata nafasi uyaongeze katika vipaumbele vya rasimu hii ambayo umetuletea. Nianze na eneo la sekta ya kilimo, wengi wameongea, kwamba kilimo ndiyo kinachoibua na kuimarisha sekta ya viwanda. Nikuombe, sekta ya kilimo ikiunganisha maeneo yote matatu, kilimo cha mazao, ufugaji mifugo na uvuvi, vipewe kipaumbele zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ilivyowekwa kwenye mpango, nina wasiwasi haijakaa vizuri. Katika eneo hili la kilimo cha mazao, ningeomba sana uliangalie sana eneo la pembejeo, hususani mbolea, lakini vilevile mbegu na viuatilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa mbolea, ni kweli, tumeondoa ruzuku, nikuombe hilo uliangalie upya. Kilimo, ndiyo kinachukua watu wengi zaidi na wengi wanaojihusisha na kilimo hawana uwezo wa kumudu bei ya mbolea ambayo sasa tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali ya Awamu ya Tano, kama ambavyo imeweka kipaumbele kikubwa katika miundombinu, niombe muweke kipaumbele katika mbolea, mbegu,viuatilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza tu, kwamba katika mbolea, tuna uwezo kabisa wa kuweka ruzuku kwa asilimia 100, kwa maana ya kwamba, wakulima wapate bure. Kama hilo haliwezekani, walau ukaweka bei kama shilingi elfu 10, kama ambavyo mkulima wangu, Kuhoa amependekeza katika meseji aliyoniletea leo, kwamba walau ukiweka hata shilingi elfu 10 kwa mfuko katika kilimo, utakuwa umewasaidia sana wakulima wengi sana ambao kwa kweli hawana uwezo wa kununua mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa mbegu, hata Wizara ya Kilimo inafahamu, kwamba matumizi ya mbegu bora, ni kwa kiwango kidogo sana kwa sababu bei yake ni kubwa. Bei iliyopo katika mbegu wakulima hawaiwezi. Tunaishia kutumia mbegu zetu za asili ambazo hazina ufanisi katika uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ama tuimarishe taasisi zetu zinazozalisha mbegu nchini, tuingize fedha nyingi upande huo, badala ya kutegemea mbegu zinazotoka nje ama zinazozalishwa ndani, lakini zinazofadhiliwa na makampuni ya nje, bei muda wote itakuwa kubwa. Hebu tuliangalie lile eneo, kama tunaweza tukaingiza ruzuku ya kutosha, nina uhakika mazao yatakayozalishwa katika kilimo, tukiondoa ruzuku, yatarudisha hasara ambayo unadhania utaipata ukiweka ruzuku katika eneo hilo, nikuombe uliangalie hilo kwa makini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ni maji, kipaumbele katika ulivyovyiorodhesha, hata katika eneo hili la maji nalo halijakaa vizuri sana. Nikuombe, jaribu kuliangalia kwa macho manne, matano, sita, hapo peke yenu mlipokaa una macho manne hapo, ya Waziri pamoja na Naibu, hebu ongezeni macho mengine katika eneo hili la maji. Najua mna sababu za msingi kukataa kuongeza shilingi elfu 50 kwenye mafuta, kwa ajili ya kuuongeza ule mfuko wa maji, ili utoke kutoka shilingi 50 uende shilingi 100, najua mna sababu za msingi, lakini hebu liangalieni hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumelipigania sana hilo la kuongeza shilingi elfu 50 zaidi, siyo kwa sababu tunataka kuongeza bei ya mafuta, lakini tunataka maji. Kwa hiyo, kama kuna namna ya kutuwezesha kupata maji, angalia katika vipaumbele vyako na eneo hilo nalo liguswe kwa namna ambayo kwa kweli watanzania watafurahia maisha, hasa watanzania wa kijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la miundombinu, umeelezea kwa kirefu sana maeneo ya reli yanayoshughulikiwa, lakini hii reli ya kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay kupitia Namtumbo, umeiweka chini sana ni kama umeificha hivi na kwa kweli ukiangalia kazi inayotakiwa kufanywa katika reli hii, inaonekana kabisa umeiweka pembeni. Yaani pamoja na kwamba umeandika sehemu ya kipaumbele, lakini in reality, nadhani bado haijaingia kwenye matrix yako kichwani mwako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe, tumeamua reli hii ijengwe kwa PPP, wenzangu waliotangulia wameeleza, kwamba fursa za wawekezaji binafsi wanaotaka kushughulika na hiyo reli wako wengi, lakini tatizo lipo katika masharti, liko katika masharti yanatakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu mliangalie hili kwa makini. Kwanza linapunguza matumizi ya fedha za Serikali. Tunatumia fedha kutoka sekta binafsi, hebu tujaribu kuangalia kama tunaweza tukapunguza masharti ili reli hii iweze kujengwa. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mpango, reli hii ukiikamilisha ukaipitisha pale Namtumbo ikafika mpaka Mbamba Bay na hatimaye ikafika Liganga na Mchuchuma, itajiendesha yenyewe na gharama zake zitarudi haraka zaidi. Kwa sababu mzigo ulioko katika hiyo corridor mwingi sana; ukiacha ile chuma ya Liganga na Makaa ya mawe ya Mchuchuma kuna madini mengine mengi sana ikiwa ni pamoja na Uranium ya Namtumbo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi madini ya Uranium yanashindikana kuchimba kwa sababu bei ya Uranium iko chini sana. Kwa sababu ya gharama zilizopo za usafirishaji, tukipunguza gharama za…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Engineer Ngonyani.

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)