Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote naomba nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo kupata fursa ya kuchangia. Vile vile nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango wa Maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu yao nzima kwa kuandaa mpango mzuri ambao tulivyokubaliana huko nyuma mpaka sasa hivi unakwenda vizuri sana, pia mkakati ambao umewekwa wa kukusanya mapato na kuhakikisha kwamba yale yote ambayo yamepangwa kwenye Mpango na bajeti iliyopangwa basi inatekelezeka vizuri. Hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naishukuru Serikali kwa juhudi kubwa ambayo inafanya katika kuhakikisha kwamba maendeleo sasa yanaonekana kwa uwazi kabisa na tumeanza kuyaona. Lengo kuu ni kukuza uchumi wetu na tufikie katika uchumi wa viwanda, lakini hapo hapo tukifungamanisha uchumi wa Watanzania wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niweze kushauri katika maeneo machache. Lengo kuu hapa na kwenye mpango huu imeelezwa vizuri kabisa kwamba kutakuwa na eneo, hasa kwenye elimu kuendelea kufundisha kwa wingi wataalam ambao ni wa ngazi ya ufundi ambao ni adimu, hawapatikani ili waweze kuja kusaidia kuendeleza mahali ambapo tunahitaji wataalam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kwamba huko huko tuweke nguvu kubwa zaidi kwa sehemu kubwa. Kama tunataka kuwa na uchumi wa viwanda, tunahitaji kuboresha Sekta ya Skills Development, yaani upande wa ufundi mchundo (technicians). Huko ndiko ambako tukiwa na viwanda vingi itawasaidia Watanzania wengi ambao uhitaji wao mkubwa zaidi ni kuingia kwenye soko la ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iangalie tutakapofika kipindi cha bajeti iwepo kwenye huu Mpango kama ilivyowekwa wazi hapa kwamba wataalam ambao ni adimu watafundishwa kwa wingi, basi pia tufundishe wataalam wetu wa kawaida, hawa mafundi mchundo (technicians) kwa kupitia VETA zetu. Kwa maana hiyo itafanya kwanza ajira ziwepo ambazo ni blue collar jobs, yaani kazi ambazo zitafanywa kwenye viwanda vyetu vyote. Pia viwanda vinavyotakiwa ni vya kisasa, vinavyokwenda na mfumo wa teknolojia ya kisasa kwa kutumia mifumo ya IT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huko kwenye VETA kunahitajika kuwekezwa zaidi mbali na ile mifumo ya zamani. Tu-phase out mifumo ya zamani, tuondokane na mifumo hiyo iliyokuwepo ili twende na mfumo huu wa teknolojia kwa kutumia IT kwa sababu siku hizi hata mashine ya kushona ya kawaida hii ya cherehani ina programming ambapo unatakiwa uwe nayo; na huhitaji kuwa na degree wala Ph.D kwenye hilo. Ni basic skills kwenye IT ili uweze kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri ili tuweze kwenda kwenye uchumi wa viwanda tuwekeze zaidi kwa upande wa VETA na hasa wataalam ambao watakuwa hands on, yaani watakuwa na uzoefu tayari. Akitoka pale chuoni tayari ana uzoefu wa kutosha kwa kupitia mpango wa ufundi wa dual apprenticeship au wa DATS, yaani anasoma kwa miezi miwili, miezi miwili anakuwa yuko anafanya kazi kwenye yale aliyofundishwa, anakwenda ku-practise ili ndani ya miaka mitatu akitoka pale tayari yeye amebobea katika fani hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia hivyo hivyo kwenye kilimo, mifugo na uvuvi, hawa wote tukiweza kuwekeza zaidi katika elimu hiyo, ajira kwa Watanzania waliokuwa wengi itapatikana kwa sababu ajira ya watu wenye degree na Ph.D ni chache na ukiangalia Watanzania wengi ni vijana. Kwa hiyo, ni vizuri kuangalia mahitaji ya soko ni nini? Wanaotakiwa kwenye ajira ya aina hizo kwa kujiajiri au kuajiriwa, basi tuwekeze zaidi katika sekta hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kuanzisha miradi ile ya kimkakati. Mmoja ni huu wa kufua umeme wa kutosha kwa kupitia Stiegler’s Gorge ambapo tutakuwa na umeme wa kutosha, kwa sababu ifikapo mwaka 2021 vijiji vyote Tanzania tutakuwa tuna umeme. Huko huko ndiyo tunahitaji kuwa na viwanda vidogo vya kusindika mazao yetu na viwanda ambavyo tutaongeza thamani mazao yetu ili tuweze kupata kipato kikubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo kuu ni kuhakikisha kwamba tunafungamanisha ukuaji wa uchumi pamoja na watu. Ukuaji wa uchumi wa watu ni kuwa na spending power. Yaani hawa wakulima, wafugaji na wavuvi ni vizuri tukawekeza zaidi kwenye Sekta hii ya Kilimo. Tukiwekeza kwenye Sekta ya Kilimo kwa mapana yake; kilimo, mifugo na uvuvi ambapo asilimia zaidi ya 70 ya Watanzania wako huko, basi tutaweza kufanya vizuri na uchumi utakuwa kwa kasi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ni muhimu tuangalie namna ya kuondoa informal sector ili iendelee kupungua ili formal sector iendelee kukua. Leo hii trend iko tofauti. Sekta isiyokuwa rasmi ndiyo inaendelea kukua. Kwa hiyo, ni vizuri tukajipanga kuhakikisha kwamba tunarudisha mfumo ili sekta iliyokuwa rasmi ndiyo iendelee kuboreshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kuwa na viwanda ambavyo vitaweza kuzalisha na tukazalishe bidhaa ambazo zitakuwa na ushindani, katika soko la ndani, soko la kanda na soko la Kimataifa ambalo liko kwenye Mpango, ni vizuri suala lile la blue print tukalifanyia kazi. Leo hii gharama ya uzalishaji Tanzania ni kubwa kutokana na hizi regulatory authorities. Gharama ya uzalishaji kwa bidhaa zetu, zinakuwa kubwa kwa sababu hizi charges ambazo ziko kwa upande wa regulatory authorities ni kubwa mno. Kwa hiyo, hatuwezi kushindana. Hata viwanda vinavyozalisha ndani, ni bora utoe mali nje, itatoka China, itatoka nchi nyingine kwa gharama nafuu kuliko ile ambayo inazalishwa ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili uchumi wetu ukue na bidhaa zetu zipate masoko, hasa bidhaa zinazotokana na kilimo, mifugo na uvuvi, ni vizuri suala la blue print lisifanyiwe kazi kwa taratibu. Yaani mngehakikisha blue print mnaileta mara moja, sheria ije na yale yote ambayo yanatakiwa yafanyiwe kazi; zile tozo na ada zote ziondoke. Tulishawahi kupendekeza mara nyingi, mngekuwa na Tanzania Regulatory Authority ambapo kunakuwa na upper stream na lower stream. Jambo hilo mkilifanyia kazi, nina uhakika kabisa kwamba bidhaa tutakazozalisha hapa nchini zitakuwa zinaweza kushindana kwenye soko la ndani, soko la kanda, lakini pia soko la Kimataifa. Bila kufanya hivyo, nina uhakika kabisa kwamba bado Tanzania itakuwa net importer wa bidhaa kutoka huko nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana hata bidhaa zetu nyingi ambazo tunazalisha hapa nchini, zinapelekwa nje wanakwenda kuzalisha kule halafu bidhaa hizo hizo zinarudi nchini kwa kupitia pamba, kwa kupitia mazao yetu mengine. Bidhaa zinatoka nje halafu zinarudi ndani ya nchi kutokana na gharama za uzalishaji wa hapa ndani ya nchi kuwa kubwa. Sehemu kubwa ni kutokana na hiyo blueprint ambayo tulisema kwamba Serikali tayari imeifanyia kazi, tunashukuru maeneo mengi mmeweza kuyafanyia kazi lakini mngeleta kwa ujumla wake ili ianze kazi mara moja kabla hatujafika kwenye bajeti ya mwakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina uhakika haya yote yakifanyiwa kazi, mtaona kasi ya ukuaji wa uchumi wetu itaongezeka mara dufu na itaweza kufanya ajira nyingi zaidi ziweze kupatikana kwa sababu malighafi ambayo tunazalisha hapa nchini itakuwa inasindikwa hapa hapa nchini au kuongezewa thamani hapa hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwamba kwenye mpango huu mmesema kwamba mtawekeza zaidi kwenye utafiti kwa kupitia vituo mbalimbali, kwa kupitia COSTECH lakini Vituo vya Utafiti vya Mifugo, yaani TALIRI au TARI kwa upande wa kilimo. Ni vizuri tuongeze nguvu kubwa zaidi katika utafiti kwa sababu hakuna nchi inayoweza kufanya vizuri bila kufanya utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile utafiti siyo kwa upande wa kilimo na mifugo tu, kwenye sekta zote; iwe ni afya, hata biashara, kwenye huu Mpango ni vizuri fedha za kutosha ziwekwe, utafiti ufanyike ili tunapotekeleza huu Mpango na tunapopanga bajeti zetu, basi tunakuwa tuna uhakika na jambo ambalo tunakwenda kulifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni muhimu upande wa huduma kwa wananchi, kwa sehemu kubwa ni Sekta ya Maji. Sekta ya Maji hapa kwenye Mpango mmeiweka lakini bado haijapata kipaumbele kinachostahili. Ni vizuri tukaangalia namna ya kuhakikisha kwamba kwa upande wa maji tuweke mkakati na Mpango kuiwezesha RUWASA kupata fedha nyingi zaidi ili miradi ya maji katika maeneo mbalimbali hapa nchini, ambayo ndiyo changamoto namba moja kwa sasa hivi ziweze kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza kwa Sekta ya Afya, Elimu, kwa Sekta ya Miundombinu, huko kote tumefanya vizuri mno. Sasa cha muhimu ni kuangalia namna ya kuongeza uchumi kwa watu wetu ili wawe na uchumi wa kununua bidhaa. Wakiwa na spending power, Serikali itaendelea kukusanya kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia cha muhimu zaidi, badala ya kufikiria namna ya kuongeza kodi tu na mapato, ni vizuri vile vile tuangalie namna ya kupunguza matumizi ambayo siyo ya lazima. Bado kuna maeneo yanatakiwa kufanyiwa kazi ili tupunguze matumizi yasiyo ya lazima ili fedha inayopatikana hiyo hiyo kidogo iweze kufanya kazi kubwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Malizia Mheshimiwa Jitu.

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Njia kubwa ni kwa kutumia force account katika miradi yetu yote.