Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Cecil David Mwambe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ndanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni ya leo na mimi niweze kuchangia mjadala ulioko mbele yetu, wa Wizara ya Kilimo. Ningependa kujikita kwenye mambo mengi sana lakini kwasababu ya muda ninaomba tu niende sehemu chache lakini nitazitaja zile ambazo ningependa nichangie.

Suala la kwanza ambalo nitalizungumzia ni kuhusiana na mkataba wa Indo na hekaya ya Profesa Kabudi suala la pili ambalo ningependa nizungumzie ni suala la export levy ambalo tulijadili ndani ya Bunge hili hili, suala la tatu ni madeni ya wakulima ya zamani; na Mheshimiwa Waziri nitaomba u- note down wakulima wa korosho walikuwa wanadai pesa ambazo zilifanyiwa auditing tukaambiwa watakuja hapa kutakuwa na kesi vitu vingine havijafanyika pesa ya misimu iliyopita, tunaomba hili ulichukulie.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwambe kabla hujaanza sasa nimeshatoa uamuzi kuhusiana na hilo endelea kuchangia semea, kosoa Serikali.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa.

Kwa hiyo kuna hayo madeni, na nishauri kabisa hapa kwamba sheria ya export levy pale ambapo tuliondoa haimaanishi kwamba zile pesa ambazo Serikali ilikuwa inawajibika kuzirudisha kwa wakulima wa korosho zisiende. Kwa hiyo tunaomba na hizo pesa nazo ziende.

Suala lingine ni suala la mradi wa SAGCOT tunataka hapo mtakapo kuja mje mtupe majibu kabisa kuna taarifa kwamba mradi wa SAGCOT umefutwa kwasababu tumeshinda ku-comply, sasa mtueleze ni kwanini. Pia kukosekana kwa pesa kwenye mradi wa ASDP II ilhali nimeona kwenye vitabu vyenu mnautaja na mkisema kwamba ni mradi wa kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine; nitaomba utueleze Mheshimiwa Waziri, kama ni wewe unahusika au dada yangu pale Mheshimiwa Manyanya ambaye alituambia mbaazi ni mboga. Yeye tunataka mtueleze waziwazi ni shilingi ngapi mpaka sasa hivi imetumika kwa ajili ya kuwalipa wale askari na gharama zima La zoezi la kukusanya zile korosho na je gharama hii itaingia kwenye bei halisi ya kuuzia korosho na ndiyo maana mnashindwa kuziuza hizi korosho? Tunataka sasa mtupe ufafanuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine hapa ni suala la Chuo cha Naliendele. Ningependa kabisa Mheshimiwa Waziri utueleze mna mpango gani hasa mahsusi na Chuo cha Naliendele? Kwasababu tumesema tuna nia ya kutaka kuendeleza hapo. Sisi kwenye kitabu chetu cha Kambi Rasmi ya Upinzani ambayo Waziri wetu alikiweka pale kwenye ukurasa wa 24 kifungu namba 85 ambacho hakikufutwa na Waziri aliyesoma pale hakukisoma kwa wakati ule. Sasa mimi naomba niwasomee na Watanzania wakielewe;

“Katika mazingira ya utatanishi Serikali ilisaini mkataba wa kuuza korosho tani laki moja na Kampuni ya Indo Power ya Kenya mkataba ambao haukutekelezeka licha ya kupigiwa debe na Waziri wa Katiba na Sheria wa wakati huo Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi (Mb) na Gavana wa Benki Kuu., Kambi Rasmi Bungeni inataka Serikali kuwawajibisha wahusika wote kwa kulipotosha Taifa na kuliingiza katika hasara kubwa kutokana na mkataba ambao haukufanyiwa upembuzi yakinifu.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ndio yalikuwa mawazo yetu sisi Kama Kambi Rasmi Bungeni.

KUHUSU UTARATIBU

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Nisimame nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Profesa Kabudi kwa kuwalostisha au kuwasababishia hasara wakulima wa korosho Tanzania na kwa kufanya hivyo…(Makofi)

MHE. GOODLUCK A. MLINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwambe, usinifanye kama logic sizifahamu, nimeshaliamulia, kama wewe tusaidie kutoa ushauri ni nini twende mbele.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoshauri…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MWENYEKITI: Hakuna mtu anayeongea hapa, unampa nani utaratibu, kaa chini, kaa chini.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoshauri kuna kitu kinaitwa ministerial responsibilities na ninachoshauri kabisa kwa Serikali hii kutokana na ubovu wa mkataba ulioingiwa kati ya kampuni ya Indo Power pamoja na Tanzania, uliosababishia hasara Tanzania na Serikali ya Tanzania nashauri wale Mawaziri wote waliohusika wawajibishwe. Hawa wana haja ya kupisha, kumwacha Mheshimiwa Rais afanye kazi zake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona hapa Mheshimiwa wetu mama Manyanya pale akishauri anaongea habari za rushwa, sisi kama Kamati tumefanya ziara kwenye ziara mbalimbali tunaambiwa huyu mama ni mpenda rushwa, mpaka wawekezaji wanashindwa kunakuja kuwekeza hapa Tanzania. Sasa leo kinachokuja hapa kutokea yeye anatuambia tunapenda mambo ya rushwa huku anatuambia mbaazi mboga, anakuja hapa mwingine anesema korosho ni dawa ya kuongeza nguvu za kiume. Wizara hiyo hiyo moja, sisi tunaangalia tu hamuwezi kutudhalilisha hivyo watu wa Mtwara.

MWENYEKITI: Kaa chini. Mheshimiwa Mwambe tuchangie kwa mujibu kwa kuzingatia kanuni za Bunge na kurudisha tena changia hoja yako bila kumtaja Mbunge kwa kumtaja jina.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na control unayojaribu kuifanya ukweli huu utabaki kuwa ukweli. Waheshimiwa hawa Mawaziri tunawalaumu watu wa Wizara ya Kilimo, lakini jambo hili la korosho linahusu watu wa biashara huyu mama yupo pale kwa muda mrefu amekaa na Mawaziri wawili hawezi hiyo kazi ampishe Rais afanye kazi hiyo. (Makofi)

MWENYEKITI: Hakuna mama humu, hakuna mama humu.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa, Mheshimiwa Naibu Waziri yule pale. Tunasema hivyo kwa sababu tuna uhakika sisi tunazunguka kufanya mikutano na wawekezaji wanamlalamikia. Yeye ni mmoja ya watu wanaokwamisha juhudi za watu hata wenye viwanda, anawapa majibu ya hovyo, anakwenda kufanya ziara akiwa na mood, kitu ambacho ni kibaya kabisa. She is out of mood all the time, you see. Kwa hiyo tuombe kabisa waangalie kabisa namna ya kufanya tumsaidie Rais, Rais anawapenda wakulima, wasiowapenda wa kulima na wasiotaka kuwapa hela wakulima ndio walioanzisha haya matatizo, kuanzia waliotayarisha mikataba na sasa hivi hii Wizara inashindwa kuuza korosho. Msmu wa korosho unaanza karibuni, maghala ya korosho yamejaa korosho kule ndani, wakulima wanadai pesa zao, korosho haziondoki baada ya wiki tatu nne zijazo maghala yale korosho tunakwenda kuweka wapi na yenyewe yataharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu kinaitwa old stock, maana yake ni kwamba zitakapoanza korosho mpya hizi za zamani hazitanunuliwa. Hakuna mtu atakayetaka anunue korosho mbovu ambazo hana uhakika nazo. Kwa hiyo, niombe pamoja na kwamba mnazuia hizi taarifa tuliandika vizuri kabisa kwenye taarifa yetu ya Kambi Rasmi lakini zipo kwenye taarifa yetu hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine baya kuliko zote, wadau mbalimbali wa korosho hawalipwi pesa zao. Rais ametangaza hata halmashauri hawezi kupewa pesa, halmashauri zetu zitajiendeshaje? Madiwani wanashindwa kulipwa Mheshimiwa Bobali amesema na hiyo sio halmashauri moja. Halmashauri ya Wilaya ya Masasi ambapo mimi natokea 85% ya mapato yake yanategemea ushuru wa korosho. Leo hii tunaenda kuambiwa pesa hizi hazitapelekwa, halmashauri zitajiendeshaje, tunashindwa kufanya kazi zetu pale kimsingi. Kwa hiyo tunaomba hili jambo liangaliwe kwa makini itumike busara hata kama bei ni mbovu tunafahamu Serikali wanalazimisha kuuza korosho kwa Sh.3,700 ndio ushauri mbovu unaotolewa na hawa watu tunaosema watoke wamuache Rais asadiwe, sisi tuna uwezo, natamani niwe Naibu Waziri Viwanda na Biashara na ndio nafasi yangu upande wa huku kwa sababu hawawezi waliopo pale na sisi ndio kazi yetu. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine baya kuliko yote tuna Vyama vya Ushirika kule kwetu lakini havipewi pesa zao kwa wakati, tunaomba wamsaidie Mrajisi Mkuu, tunafahamu sasa hivi huyu Mrajisi aliyepo ni wa pili baada ya yule wa kwanza kushindwa kutimiza majukumu yake. Naye hapelekewi pesa imeandikwa kwenye vitabu hapa, Serikali hii ndio haimpelekei pesa, atafanyaje kazi zake, atatimizaje wajibu wake kule chini, tunaua Vyama vya Ushirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limekuja jambo la kangomba, nishukuru Mheshimiwa pale amesema kwamba kangomba anatambua kwamba ni wajasiriamali lakini tuwaambie kabisa kangomba inazaliwa kutokana na ubovu wa kutekeleza mikakati ya Serikali. Serikali zamani ilikuwa na utaratibu wa kupeka pesa kwenye Vyama vya Ushirika, lakini utaratibu huu umeachwa. Sasa wale wananchi kati ya mwezi wa Tano mpaka wa Nane waniishi kwa kutumia nguvu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, aibu kabisa, tunazidi kudhalilishwa, Mheshimiwa Waziri anafikiri sisi Mtwara hatuna uwezo wa kuzaana, juzi anaongea na waandishi habari anasema kwamba kuleni korosho kwa wingi zinaongeza nguvu za kiume, sio malengo ya sisi kulima korosho kuongeza nguvu za kiume. Tulikuwa tunalima korosho ili tuweze kupata pesa kigeni, nchi yetu iweze kupata pesa kigeni maendeleo yasonge mbele leo unasimama Waziri ambayo ndio unamsaidia Rais anatuambia kuleni… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)