Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naunga mkono hoja na nampongeza Waziri wa Viwanda na Biashara pamoja na Naibu wake na watendaji wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi sina, naomba nimpongeze Rais wangu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya kuhamasisha ujenzi wa uchumi wa kati wa viwanda. Miradi mikubwa ya ujenzi wa miundombinu inayoendelea ikijumuisha njia za reli, umeme, barabara, viwanja vya ndege na bandari ni ishara tosha kuonyesha dhamira njema ya Rais ya kujenga uchumi wa viwanda inakwenda kutekelezwa kwa vitendo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa msingi huu, nashauri sasa Serikali iwekeze juhudi za dhati za kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji wa viwanda vya aina mbalimbali nchini kwa kuondoa au kupunguza kodi zisizo za lazima, kuharakisha utoaji wa vibali na kutangaza fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo katika nchi yetu. Hizi fursa ni pamoja na kuanzisha na kufufua viwanda vya mazao ya kilimo, mifugo, madini na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe hoja kuhusu mradi wa Magadi Soda Engaruka. Mradi huu umezungumziwa katika kitabu cha hotuba ya Waziri ukurasa wa 17. Pamoja na utafiti wa kina ambao umeanza kufanyika kubaini upatikanaji wa rasilimali ya magadi, maji safi, athari za mazingira na kijamii, naomba nitoe angalizo kuhusu masuala yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ingawa eneo kubwa la mradi wa magadi liko katika Wilaya ya Monduli, vilevile kuna sehemu ya ardhi iliyopimwa ambayo imeingia ndani ya eneo la Wilaya jirani ya Longido (Kijiji cha Sokon). Hivi sasa tunavyojadili bajeti ya Wizara hii, wananchi wa Kijiji cha Sokon wanaoishi katika eneo ambalo limeingia ndani ya ardhi iliyopimwa na kufanywa sehemu ya viwanda wameshapewa notisi ya kuhama ndani ya wiki mbili na huku bado hawajafidiwa. Nashauri wananchi wasibughudhiwe mpaka wafidiwe kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, faida za mradi kwa wananchi ama Wilaya husika. Kwa kuwa mradi huu wa magadi umetwaa vipande vya ardhi vilivyoko ndani ya Wilaya ya Monduli na Longido, ni vyema Wizara itambue hilo na ibainishe kuwa kiko katika wilaya zote mbili ili jamii zote wapate faida na kuepusha migogoro isiyo ya lazima ya kugombania rasilimali husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, miundombinu. Kwa kuwa eneo la mradi ni mbali (remote area) na lenye mazingira magumu na lisilo na barabara inayopitika, nashauri Serikali iwekeze kwanza katika kufungua barabara za kufikia eneo la mradi. Kuna njia mbili za kufika katika eneo la mradi: Barabara ya kutoka Mto wa Mbu (km 70); na barabara ya kuunga barabara ya moram inayotoka Longido – Oldonyo Lengai (km 14).

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, umuhimu wa kuanzisha kiwanda cha kuchakata nyama. Kwa kuwa eneo la Bonde la Engaruka na maeneo yote yanayopakana nalo ni ya wafugaji ikijumuisha Tarafa nzima ya Ketumbaine, Wilayani Longido, Engaresero, Wilayani Ngorongoro na Tarafa ya Ngorongoro, Wilayani Monduli. Napenda kuishauri Serikali kuwa kijengwe kiwanda katika eneo hili cha kuchakata nyama. Eneo hili ni tajiri kwa mifugo na lina nyanda pana za malisho kasoro maji safi na kwa kuwajengea wafugaji kiwanda cha kuchakata nyama na mazao mengine ya mifugo itakuwa ni faida ya ziada ya kufunguliwa uchumi wa viwanda katika Bonde la Engaruka.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache, naomba kuhitimisha kwa kutamka tena kuwa naunga mkono hoja.