Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. MWIGULU L. N. MADELU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia Wizara hii nyeti, Wizara iliyobeba msingi mkubwa kabisa wa Ilani ya Uchaguzi ya 2015/2020 chini ya Rais wetu na Mwenyekiti wetu wa CCM wa Tanzania ya viwanda ambao Mheshimiwa Rais ameusema na ameanza kuitekeleza kwa kiwango kikubwa tangu ameingia madarakani.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatofautina katika maeneo mengi sana tunapotazama jambo hili la viwanda, wapo wanaoona kazi haijafanyika, lakini na wapo wanaofanya uchunguzi wa kina kwenye mahitaji makubwa ya viwanda tunaoona kwamba kuna kazi kubwa sana imefanyika. Matatizo ya sekta hii ya viwanda na biashara yapo mengi lakini nitataja yaliyokuwepo kwenye ngazi nne.

Mheshimiwa Naibu Spika, ngazi ya kwanza ilikuwa katika mazingira ya uzalishaji na mazingira ya kufanya biashara. Katika mazingira ya kufanya biashara, Serikali ilishatambua jambo hili na kuna kazi kubwa ambayo imeshafanya na jambo hilo ni kuandaa dira (blue print) ambayo imebainisha matatizo na imeweka mapendekezo ya namna ya kutatua matatizo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maoni yangu kwa Wizara ni kwamba, kama ambavyo Serikali iliweza kuleta sheria tukarekebisha kwenye upande wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii, ilete sheria ambayo itafanya merging ya zile taasisi zote ambazo ndiyo zinaleta multiplicity ya duties pamoja tozo ambayo inaleta matatizo katika mazingira haya ya ufanyaji wa biashara katika nchi yetu. Hatutaweza kuondoa tu vile vitu ambavyo vinafanya wananchi wetu wananyanyasika na mazingira ya ufanyaji wa biashara yanakuwa mabaya kama hatutaanza kwanza kwa kuziunganisha taasisi hizo ambazo kuishi kwake zinategemea tozo zinazotolewa na wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, kwa sababu dira ile ilikuwa imebainisha maeneo ya taasisi ambazo majukumu yake yanafanana, iletwe sheria ile ambayo itaunganisha taasisi hizo zote na tukiunganisha taasisi hizo, zile tozo zinazoenda sambamba ambazo zinaleta matatizo kwa wananchi wetu, zitakuwa zimefutika. Hatutaweza kuzifuta tozo peke yake kwa sababu taasisi nyingi hizo zinaishi kwa kutegemea tozo hizo ambazo wananchi wetu wanatozwa na zinasababisha matatizo katika biashara za watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutakuwa tumeshatatua tatizo pia la muda mwingi kutumika kwa wananchi kusubiri vibali vya taasisi nyingi ambazo zina-justify kutoza tozo hizo kwa kujifanya kwamba zina majukumu japo majukumu yale yanafanana na yangeweza kufanywa na taasisi moja na ikaondoa gharama na muda ambao unatumika kwa watu wanaoshughulika na biashara kwenda katika madirisha mengi. Kwa hiyo, jambo hili kwa sababu Serikali tayari ilishatengeneza blue print ile, tunaweza kusema kwamba kuna hatua kubwa ambayo imeshafanyika sasa tufanye ile ya umaliziaji ili tatizo hilo liweze kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo lilikuwa tatizo na lilikuwa kigezo ambacho Serikali imeshalifanyia kazi kwa kiwango kikubwa na Waheshimiwa Wabunge wengine wameshaongelea ni suala la umeme. Suala hili la umeme ni jambo muhimu na kigezo muhimu sana kwenda kwenye viwanda serious katika nchi yoyote inayoenda kwenye viwanda vikubwa ambavyo vinaweza vikachukua vijana wengi wakapata ajira katika maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili wengi tunaweza tusitambue faida yake na kwa nini tunalisemea kwa kiwango kikubwa na kwa nini Rais aliamua kufanya uamuzi wa kijasiri kuweza kuhakikisha kwamba tunakuwa na uzalishaji mkubwa wa umeme ambao unaweza ukaendesha viwanda. Kwa umeme tuliokuwa nao, mtakumbuka hata matumizi ya majumbani tu tulikuwa na mgao wa umeme; tusingeweza kuwa na viwanda vingi serious kwa kiwango kile cha umeme tulichokuwa tunakuwa nacho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo limesalia ambapo Serikali na Wizara inatakiwa ilifanyie kazi ni kwenye ngazi ya uzalishaji. Kwa malighafi tulizonazo tukiweza kutengeneza viwanda vikubwa ambavyo vinatakiwa vitumie umeme mkubwa huu tunaotengeneza na picha kubwa aliyokuwa nayo Mheshimiwa Rais ya kutengeneza viwanda, tunahitaji tutengeneze zoning katika nchi yetu ili kuweza kutengeneza mazingira (mechanization) kwenye uzalishaji ili tuweze kuzalisha malighafi ambazo zinaweza zikatosha kuwa na viwanda vikubwa ambavyo vinaweza vikatufanya katika sekta ambazo tutakuwa tumezitaja tuweze kuwa wazalishaji wakubwa duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hiviā€¦

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ilishagonga Mheshimiwa Mwigulu, ahsante sana.

MHE. MWIGULU L. N. MADELU: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na kazi kubwa inayofanywa na Rais na Wizara hii. (Makofi)