Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii ambayo ni muhimu sana katika ustawi wa taifa letu kwa sababu tukiwa na tukiweza kufanya biashara vizuri, tunaweza tukafanya mambo mengine mengi ya kijamii na tukaweza kwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze alikoishia ndugu yangu Mheshimiwa Mashimba Ndaki, ambaye tumesoma darasa moja kwamba ili tulinde viwanda vyetu, ni lazima tuwe na mazingira yanayotabirika. Katika nchi yetu, tuna tatizo kubwa sana la mazingira ya biashara yasiyotabirika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi huu uliopita tu, TRA walitoa tangazo la kupiga marufuku vinywaji vyote ambavyo havina stika ya kieletroniki kwamba ikifika tarehe 30 ya mwezi uliopita, hivyo vinywaji vyote vitakuwa vimekoma na havitakuwa na thamani tena. Hiyo marufuku inavyofanyika sijui walizingatia nini kwa sababu hivyo vinywaji vilinunuliwa katika utaratibu wa kisheria na vina stika ambazo zinatambulika na vimeshasambazwa katika nchi nzima. Maana yake vinywaji hivi vinapatikana Dar es Salaam, vinakwenda kwenye jimbo fulani, labda la ndugu yangu Mlimba kule Ifakara, sasa unavyowaambia unawapa siku chini ya 30 kwamba wavirejeshe vyote viweze kupata stika nyingine na wasipofanya hivyo, hiyo biashara itakuwa imekoma, kwa kweli ni kitu cha ajabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Naibu Waziri nilimweleza na amelifanyia kazi. Katika hali ya namna hiyo, inatupa shida na ndiyo maana biashara inasinyaa kila kukicha katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kuna masuala haya ya kurejesha VAT. Tumeambiwa hapa kuna burden ya zaidi ya shilingi bilioni 45, sasa ni nani anakuja kuwekeza hapa wakati hana uhakika wa kuridishiwa kile ambacho kiko kwenye mkataba? Kwa hiyo, katika hali kama hii, inatupa shida sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mazingira ya kufanya biashara ni magumu sana. Ndugu yangu Mheshimiwa Bashe alisema jana kuhusu habari ya kuanzisha kiwanda cha kusindika maziwa. Leo tunavyozungumza, nchi yetu inazalisha maziwa lita bilioni 2.4 kwa mwaka lakini maziwa tunayosindika ni lita kama milioni 37 tu. Hii ni kwa sababu ya mlolongo wa kodi ambazo zipo, jana Mheshimiwa Bashe alisema ni 26, mimi ninalo andishi hapa, ni tozo na kodi 28. Taasisi au mamlaka ambazo zinakwenda kushughulika na wewe siku ukiamua kuanzisha kiwanda cha kusindika maziwa ni 11 na taasisi moja inaweza ikarudi hata mara nne kwenye hiyo biashara yako.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu wa Kenya, leo wanazalisha maziwa lita bilioni tano kwa mwaka, wanasindika zaidi ya lita bilioni tano kwa mwaka. Leo Uganda wanazalisha lita bilioni 2.4, wanasindika zaidi ya lita laki tano kwa siku, sisi tuko kwenye laki moja na elfu hamsini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ndugu zangu ili uanzishe kiwanda cha kusindika hapa Tanzania, unapashwa ulipe zaidi ya shilingi milioni 33 ndiyo kiwanda kianze kuzalisha. Sasa tunang’ang’ania milioni 33 lakini tunapoteza ajira na kodi ambazo tunaweza tukazipata kwa kuwepo na viwanda vingi, tunapoteza mapato ambayo yanatokana na bidhaa zinazotokana na maziwa ambazo ziko zaidi ya 20. Sasa jamani, hii ni akili gani? Tumelogwa na nani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo hatutumii fursa ambazo tunazo ambazo tumepewa na Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye hoja ya tatu, nayo ni sakata la korosho. Nasi kwenye ukurasa wa 42 kwenye kitabu chetu cha Maoni ya Kambi ya Upinzani Rasmi Bungeni, tumesema watu wawajibike. Hapa nataka niwe very specific; na niliombe sana Bunge hili linisikilize na lichukue hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliingia mkataba na kampuni inaitwa INDO Power ya Kenya. Siku tulivyoenda kuingia mkataba Serikali ilikwenda pale, Mawaziri kadhaa walikwenda pale akiwepo Waziri wa wakati huo wa Katiba na Sheria, Profesa Palamagamba Kabudi na Gavana wa Benki Kuu alikuwepo pale. Katika watu waliozungumza, Kabudi alizungumza, akasema Kampuni hii ina weledi, ina uzoefu, ina uwezo wa kifedha na hata huyo mmiliki wa kampuni hiyo alikuja kwa ndege binafsi ya kukodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Gavana wa Benki Kuu akasema alifanya due diligence kuona kwamba kampuni hiyo ina weledi wa kutosha na uwezo wa kutosha wa kufanya hiyo biashara. Baada ya miezi minne, ile biashara, kama Watanzania walivyosema na Mheshimiwa Rais alisema, Watanzania siyo wajinga. Walisema hii kampuni ni ya kitapeli, haina uwezo huo. Waliandika kwenye mitandao. Baada ya miezi minne imeonekana kampuni ile haina uwezo, imeshindikana na ile biashara imekufa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi kweli Bunge hili linakubali Mheshimiwa Kabudi aendelee kubaki na Uwaziri wake, mtu ambaye kila kukicha anamdanganya na kumfanya Mheshimiwa Rais aendelee kupotoka hivi! Hapa duniani Rais wa nchi akilalamika, Rais wa nchi akilia, kinachoweza kumsaidia ni Bunge la nchi. Kama Bunge la nchi likishindwa, basi tunamuachia Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri tusifike hapo ndugu zangu, Bunge lako Tukufu lichukue hatua ili hawa watu wawajibike. Kabudi; na ningefurahi sana angekuwepo hapa; Kabudi, mnakumbuka masuala…(Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Komu, ni Mheshimiwa.

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Profesa Kabudi, nafurahi kama angekuwepo hapa, kwa sababu mnakumbuka issue ya makinikia, mnakumbuka issue ya Sheria ya PPP, mnakumbuka issue ya sheria ya kulinda rasilimali za nchi hii, mnakumbuka issue ya Sheria ya Takwimu; haya mambo yana utata. Kwa hiyo, naliomba Bunge hili lichukue hatua dhidi ya Kabudi, awajibike. Hawa wengine ndugu zangu hapa akina Kakunda, Mheshimiwa Japhet Hasunga, hawa ni watu ambao wako kwenye basi tu, lakini anayeendesha hili basi, ni Kabudi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana, tusije tukamfanya Rais wetu aonekane kwamba ni mtu tu ambaye analialia jambo ambalo siyo heshima kwa Bunge hili na siyo heshima kwa Watanzania walio...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)