Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii kuchangia katika hotuba hii nzuri ya Mheshimiwa Waziri. Nitaenda moja kwa moja katika hoja ya Bandari ya Bagamoyo.

Mheshimiwa Spika, mradi huu wa uwekezaji umeorodheshwa na Serikali katika bajeti ya mwaka huu ambayo inamalizika 2018/2019 ikiwa ni mradi mkuu wa kielelezo ambao Serikali mlitaka kuutekeleza kwa ajili ya maendeleo ya nchi hii. Mradi huu unajumuisha ujenzi wa bandari, lakini pia unajumuisha ujenzi wa viwanda. Eneo hili maalum la uwekezaji ni kichocheo kikubwa sana cha maendeleo ya nchi yetu, maendeleo ya viwanda na maendeleo ya uchumi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa yale ambayo umeyasema kwa maana kwamba, umeendana kabisa na mawazo ambayo nilikuwanayo mimi kama Mbunge wa Bagamoyo. Imekuwa faraja sana kupata hao wawekezaji; China na Serikali ya Oman, marafiki zetu kama Waheshimiwa Wabunge walivyosema. Lazima tutumie fursa hizi za marafiki ambao tumehangaika nao sana kwa miaka mingi ambapo sasa fursa hizi wanatumia watu wengine sisi hatuzitumii, ni muhimu sana tutumie fursa hizi.

Mheshimiwa Spika, China na Oman wamekubali kuwekeza jumla ya dola bilioni 10 ama takribani trilioni 23 za Kitanzania kwa ajili ya ujenzi wa bandari na ujenzi wa viwanda. Mwanzoni wamekubali kwamba watajenga viwanda vikubwa 190 vya kuanzia. Maana yake kwa ajili ya ujenzi huu, vitatoa fursa za ajira takribani 270,000.

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa imefanyika na viongozi wetu na wataalam katika nchi hii, kwa miaka mingi iliyopita, tumeanza na mwaka 2012 ambapo MOU ilisainiwa, Machi, 2013 Framework Agreement imesainiwa; Desemba, 2013 Implementation Agreement imesainiwa; Oktoba, 2015 Tripartite MOU imesainiwa; na Septemba, 2015 jiwe la msingi la ujenzi wa bandari limewekwa na Rais Mstaafu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Pande na Mlingotini wamejitolea ardhi yao kwa ajili ya maendeleo haya ya ujenzi wa bandari pamoja na viwanda katika hali ngumu sana, lakini wakasema potelea mbali acha tutoe maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, nasikitika sana kwamba inavyoelekea sasa juhudi hizi zote hazikuzaa matunda. Nimesoma ukurasa wa 99, aya ya 136 ya Hotuba ya Waziri, inaelekea kwamba bandari hii sasa haipo.

Mheshimiwa Spika, China Merchant wakati tunasaini MoU ya 2012 wamesaini pia MoU na nchi ya Djibout kwa ajili ya ujenzi wa bandari. Hivi sasa wameshajenga multipurpose port inayoitwa Doraleh kule Djibout. Bandari hii sasa inafanya kazi. Kama vile haitoshi mwezi Machi mwaka huu wamesaini tena na China Merchant ujenzi wa Special Economic Zone Djibout kwa mtaji wa dola bilioni tatu na nusu, takribani shilingi za Tanzania trilioni nane; kwamba, 2012 wamesaini kama sisi na wameongeza tena sasa hivi wanajenga Special Economic Zone.

Mheshimiwa Spika, kama vile haitoshi, katika kipindi hiki sisi tunaongea tangu 2012, China Merchant weamesaini na kujenga bandari Nigeria, Tin Can Ireland; wamejenga Lome, Togo; wamejenga Abidjan, Ivory Coast, wamejenga Colombo – Sri-Lanka.

Mheshimiwa Spika, kipindi hiki cha miaka hii karibu saba sisi tunafanya maongezi, nchi tano nilizozitaja zimekamilisha maongezi. Djibout imekamilisha maongezi na wamejenga bandari, Nigeria wamekamilisha maongezi na wamejenga bandari, Togo wamekamilisha maongezi, Ivory Coast wamekamilisha maongezi, Sri-Lanka wamekamilisha maongezi na wamejenga bandari isipokuwa Tanzania tumeshindwa kwa muda wote huu kukamilisha maongezi. Tuna tatizo gani? Tuna shida gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wataalam wa nchi hizi tano nilizotolea mfano ni bora zaidi wanaweza wakakamilisha maongezi isipokuwa sisi nchi yetu ya Tanzania haina wataalam wa kuweza kukamilisha maongezi.

Mheshimiwa Spika, haiwezekani 2025 nchi hii kuwa nchi ya uchumi wa kati ni miaka sita ijayo. Hatuna muda tena hata kidogo wa kusubiri katika jambo hili. Mtaji wenyewe una wakati, kwa sababu sasa hivi China wanatekeleza mradi wao wa Belt and Road Initiative nao uko time bound, tukiuacha huo maana yake watakwenda kuwekeza mahali pengine. Huwezi kupata mtaji mkubwa kama huu unasubiri nchi moja tu ifanye maongezi miaka saba haikamiliki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, atakapokuja Mheshimiwa Waziri, kama ulivyoweka msisitizo, atuambie kwa kina. Tanzania tuna wataalam, Watanzania ni mahodari, Watanzania hatuna fani ambayo iko nyuma. Haiwezekani nchi hizi zikaweza kukamilisha, bandari zikajengwa, sisi tunaendelea kuzungumza kila siku. China wana usemi wao, maneno matupu ni hatari kwa Taifa. Na sisi tunataka kukumbatia kuzungumza tu na kuzungumza tu na kuzungumza tu kila siku, tutaliangamiza Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)