Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa fursa hii. Kwanza niunge mkono hoja iliyo Mezani kwetu tunayoijadili lakini nitumie fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watendaji wote katika Wizara hii. Kimsingi mnafanya kazi kubwa sana ingawa hamjafikia asilimia 100 kulingana na matarajio yetu, lakini niwapongeze mnafanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii vilevile kumpongeza sana Eng. Sanga, amekuwa msaada mkubwa sana kwa watu wa Kanda yetu na hasa kwenye eneo letu la Visiwa vya Ukerewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utakuwa katika maeneo kama matatu kama muda utaniruhusu. La kwanza, nianze na eneo la Ukerewe. Ukerewe tuna miradi takribani mitano, inakwenda vizuri tunashukuru sana lakini nimepitia hotuba, ukurasa wa 64 unaongelea mradi wa vijiji 301 vitakavyofaidika na mradi ule wa maji kutoka Ziwa Victoria. Ni mradi mzuri, kwenye Jimbo la Ukerewe kama utakamilika utatusaidia vijiji takribani 33 na kwa ujumla wake utakuwa umesaidia tatizo la maji mpaka kufikia zaidi ya asilimia 80. Rai yangu tu ni kuomba utekelezwe mapema ili uweze kutusaidia hasa kwenye eneo la Visiwa vya Ukerewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, Ukerewe pale tuna mradi mkubwa sana wa maji, ulizinduliwa na Mheshimwa Rais mwaka jana; Mradi wa Maji wa Nansio. Ni mradi mkubwa sana lakini kwa mazingira yalivyo mpaka sasa kimsingi uko under-utilized. Una wateja kama 2,900 pekee na una uwezo mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa ni kwamba Mamlaka ya Maji Nansio haina uwezo wa ku-extend ile distribution network matokeo yake Serikali sasa kupitia Wizara mmekuwa mna-support Mamlaka ile ili iweze kujiendesha. Ushauri wangu ili kuondokana na kila wakati kuisaidia Mamlaka kujiendesha mnge-inject fedha kwenye mradi huu ili Mamlaka ya Maji Nansio pale iweze ku-extend hii network ya usambazaji wa maji kwa vile ikiwa na wateja wengi inaweza ikajiendesha kwa kukusanya makusanyo makubwa badala ya kuwa mnai-support kila wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana Wizara ifanye jambo hili, kwa sababu sioni kama ni tija sana kila wakati kuendelea kuiwezesha Mamlaka hii iweze kujiendesha kuliko kama mnge-inject tu kiasi fulani cha fedha ili mamlaka hii ikaweza ku-extend usambazaji wa maji; mtakuwa mmetusaidia sana. Pamoja na changamoto nyingine ndogo lakini mambo yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, kuna watu wana eneo wanahitaji maji pale Ukerewe. Mheshimiwa Waziri ulipokuja Ukerewe nilishauri jambo hili. Inawezekana uwezo wa ku-apply kupata maji ni mdogo; mngeandaa programu fulani ili ikiwezekana wananchi hawa wakafungiwa maji na baada ya kufungiwa maji, hata kama ni kwa madeni ili kwamba maji watakapoanza kulipa zile bills za maji watakatwa pamoja na kile kiwango cha pesa ambacho Wizara ime-subsidize wakati wa kuwaunganishia maji. Inawezekana miradi hii ikawa na wateja wengi na hatimaye mamlaka hizi ziweze kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, hili nilitaka kushauri. Kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge, miradi mingi ya maji inasuasua sana, kuna matatizo mengi makubwa. Hata hivyo kwa mtazamo wangu tuna tatizo kubwa sana la wataalam wa maji kwenye halmashauri zetu na maeneo yetu. Ukichunguza matokeo makubwa yanaanzia hata kwenye usanifu wa miradi, matokeo yake tunakuwa na miradi ambayo inakuwa haina tija. Kwa hiyo tuhakikishe kwamba tunaajiri watu wa kutosha, hususan wenye kada hii ya maji ili angalau miradi yetu iweze kukamilika na iwe na tija kuweza kutoa manufaa tunayoyatarajia kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati fulani nilikuwa kwenye kamati ya LAAC tulitembelea miradi mingi sana. kwenye maeneo ya vijijini miradi hii ikishakamilika uankuta wananchi hawana uwezo wa kuiendesha miradi hii kwa sababu gharama za uzalishaji zinakuwa kubwa kwa sababu chanzo cha maji ama kinatumia mafuta au kinatumia umeme. Tunaweza tukaepuka hili kama tutaondoa kodi kwenye mashine zile zinazoingia kwa ajili ya kuzalisha maji. Vile vile kama tutatumia solar systems kwenye uzalishaji wa maji inawezekana production cost itakuwa ndogo na kwa maana hiyo wananchi wa kawaida hawa wanaweza wakamudu gharama hizi za kuendesha miradi hii ya maji na ikaweza kufanya kazi vizuri wananchi wakafaidika na miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kama mapendekezo yalivyoletwa na Kamati husika, sina shaka, ninaomba tuungane na mapendekezo ya Kamati hii kama ambavyo tumekuwa tukijadili kwa miaka mitatu. Kwa sababu matatizo mengi makubwa tuliyo nayo kwenye maji ni kwa sababu hatuna pesa za kutosha. Kama tukiongeza pesa kwenye mfuko wa maji inawezekana tukaondokana na tatizo hili kwa sehemu kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kunakuwa na kigugumizi, kwamba ama kutoa kwenye mafuta au namna gani, lakini kama Serikali ridhieni pendekezo hili, kwa namna yoyote itakayoonekana kwamba inawezekana, ama kutoa kwenye mawasiliano. For instance tukichukua labda kwa gigabyte moja tukitoa shilingi mia moja ninaamini tunaweza kuwa na makusanyo makubwa sana ambayo yanaweza kutunisha mfuko huu wa maji kuliko hiki cha maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano tukiangali kwa bajeti ya mwaka huu inatolewa asilimia 51 ambayo ni ndogo sana kuweza kukabiliana na tatizo la maji tulilo nalo kwenye nchi hii. kwa hiyo ninaungana kabisa na mapendekezo ya Kamati, kwamba ni muhimu tukaboresha mfuko wa maji ili hatimaye usambazaji wa maji hususan kwa wananchi wa vijijini ukawa kwenye kiwango kikubwa ili tuweze kutimiza azma ya kumtua mama ndoo kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchache nashukuru sana kwa nafasi hii uliyonipa. (Makofi)

MWENYEKITI: Unga mkono hoja.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitangulia mkono hoja; kwa mara nyingine ninaunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)