Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nashukuru kwa michango yote na ningeomba tu usikivu kwamba sijaja hapa kujibizana na mtu. Mimi sifanani kabisa na yule jamaa aliyekuwa anaoga, kichaa akaja akachukua nguo zake akaanza kumfukuza, kwa hiyo, mimi nabakia kwenye maji. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee namshukuru sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mheshimiwa George Masaju kwa kuungana na mimi katika kujibu baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Vilevile na kwa namna ya pekee kabisa niishukuru sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa maoni na ushauri wao kwa kweli uliokwenda shule. Maoni yote ya Waheshimiwa Wabunge na ya Kamati ya Kudumu ya Bunge tumeyachukua kama Wizara na tunaahidi kuyafanyia kazi na kuyatolea majibu kwa maandishi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa wengi wameongea na wengi wametuletea kwa maandishi hivyo nashindwa kupata idadi maana zinakuja karatasi mpaka sasa lakini kama nilivyosema majibu tutaleta kwa maandishi na muda nilionao ni mfupi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya hoja zimeletwa hapa chache nitazijibu kwa haraka haraka. Hoja ya kwanza ya Kamati ni kuhusu deni la mkataba wa ubia wa jengo la RITA. Naomba kusema kwamba mazungumzo tayari yanaendelea kati ya taasisi zinazohusika na ubia huu wa jengo la RITA. Lengo kuu ni kuhakikisha kwamba tunaishauri Serikali kulitwaa deni hilo na kupunguza ongezeko la deni linaloendelea katika mradi huu wa ujenzi huu wa jengo la RITA.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja ya Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kifuate sheria za NACTE na walimu wawe na sifa za shahada na uzamifu za kufundishia vyuo vikuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto tukumbuke wote kilianzishwa mwaka 1988 kwa ajili ya kutoa mafunzo endelevu kwa Majaji, Mahakimu na watumishi wa Mahakama. Kwa kweli chuo hiki kimefuata miundo kabisa ya vyuo vingine vilivyopo Kenya, Afrika Kusini na Canada vinavyotoa ujuzi wa kuboresha utendaji wa Mahakama.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba tunaweza kufika huko lakini kwa sasa tumejikita na lengo la awali la kutoa mafunzo endelevu kwa Majaji na Mahakimu na watumishi wa Mahakama lakini baadaye kama hali kwa kweli ita-demand tuanze kutoa mpaka degrees tutafanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja ya kufanya mapitio ya kisheria kuhusu adhabu ya kifo ili tuifute hapa Tanzania. Naomba tu niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba utafiti uliofanyika mwaka 2009 na Tume ya Kurekebisha Sheria ulionyesha kuwa Watanzania wengi bado wanataka adhabu ya kifo iendelee. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wanasema hivi kutokana na vitendo vya kikatili na vya kutisha kama vile kuwakata viungo wenzao hasa kwa mfano ndugu zetu wenye ualibino, kuua vikongwe, kuua watoto wachanga na huko nyuma kulikuwepo na mchezo wa kuchunana ngozi. Kutokana na hayo, Watanzania wengi wanaamini kwamba kuendelea na adhabu hii ni tishio zuri, it is a deterrent ambayo hatuwezi kuachana nayo haraka haraka hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja kwamba Mahakama ihakikishe ufanisi na ufasaha katika umaliziaji wa mashauri kwa kuzingatia kuwa justice delayed, is justice denied na kwamba justice hurried is justice buried. Nakubaliana kabisa na Kamati kwamba katika kuharakisha sana kumaliza hizi kesi tunaweza kujikuta kweli tunakanyaga baadhi ya haki za watu. Naomba tu Waheshimiwa Wabunge tukubaliane kwamba tulikuwa na mzigo mkubwa sana wa kesi (backlog). Mimi naipongeza sana timu ya uongozi wa Mahakama ya sasa kwa kuhakikisha kwamba tunaondokana na huu mzigo wa kesi na baada ya mwaka mmoja au miwili tutarudi sasa kukazania kuhusu substance na quality ya judgements hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, niende haraka kuzungumzia kuhusu mchakato wa Mahakama ya Kadhi. Mheshimiwa Ahmed Juma Ngwali anasema mchakato wa kuanzisha Mahakama ya Kadhi umeishia wapi?
Mimi niombe tu kusisitiza kwa Mheshimiwa Ngwali kwamba kimsingi Mahakama ya Kadhi ipo na inafanya kazi. Serikali ilichotaka kukifanya katika Bunge la Kumi kwa wale tuliokuwepo hapa ni kuyapa nguvu ya kisheria maamuzi yanayotokana na Mahakama hiyo kupitia sheria ya Bunge. Mliokuwepo mnakumbuka kwamba katika Bunge la Kumi Serikali ilipowasilisha Muswada huo wa Mabadiliko ya Sheria ulikabiliwa na upinzani mkubwa siyo tu ndani hata nje ya Bunge.
Mheshimiwa Naibu Spika, madai mengi yalikuwa kwamba hatukulifanyia hili suala kazi ya kutosha kuwahoji Watanzania wengi inavyostahili. Vilevile nje ya Bunge kulikuwa na mhemko mkubwa wa mawazo kiasi cha wananchi wawili kumfungulia Mwanasheria Mkuu wa Serikali kesi mbili. Alikuwepo, wote mnamkumbuka, Marehemu Mchungaji Christopher Mtikila alimfungulia kesi Mwanasheria Mkuu Mkuu wa Serikali kuhusu hili hili suala, kesi namba 7 ya mwaka 2015. Vilevile alikuwepo Shehe Rajabu Katimba na wenzake nao wakamfungulia kesi Mwanasheria Mkuu wa Serikali, tukalazimika kuliondoa suala hili Bungeni kwa lengo la kulifanyia kazi zaidi na suala hilo tayari tumelipokea rasmi kutoka Serikali ya Awamu ya Nne na sasa tunalifanyia kazi. Si suala jepesi maana lengo ni kupata muafaka wa Watanzania tuweze kuishi vizuri katika nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ngwali vilevile naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana kwa kunikumbusha kuhusu The Waqf Commission na vilevile Dkt. Suleiman naye alituongezea elimu yake kuhusu suala hili na sheria yenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa taarifa ni kwamba sheria hiyo haipo ila vipengele vyake vimekuwa incorporated kwenye Probate and Administration of Estate Act, Sura ya 352 na ukiangalia kifungu cha 142 kinaongelea kuhusu hiyo Waqf Commission. Namuomba Mheshimiwa Ngwali aniamini, nitalifuatilia. Nimekushukuru to bring it to my attention. Tuna sehemu ya kujifunza, wenzetu Zanzibar Sheria yao ya Waqf and Trust Commission inaweza kutoa mafunzo mazuri kwetu lakini kama nilivyosema nimelichukua hilo, nakushukuru sana kwa kunikumbusha.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Profesa Anna Tibaijuka amelalamika sana kuhusu Mahakama Wilaya ya Muleba hasa za Mwanzo, zinajisahau kama ni Mahakama. Anasema Mahakimu wamekuwa kama machifu wadogo wadogo kule. Vilevile Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu amelalamikia Mahakama za Mwanzo Wilayani Igunga kufikia mpaka kuwabambikizia wananchi kesi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme mawili, unapofikia mahali ambapo hujaridhika na uamuzi wa mahakama hizo za chini na ili tusiingilie uhuru wa mahakama, tafadhali Waheshimiwa Wabunge tuwatie moyo wale ambao wamesikitishwa wakate rufani. Siyo hivyo tu, nawaomba Waheshimiwa Wabunge tusiwe sehemu ya watu wanaolalamika, tuwe sehemu ya watu ambao wanasaidia kui-operationalise, kuitekeleza Sheria ya mwaka 2011 ambayo inaunda District Ethics Committees za watumishi wa mahakama. Kila Wilaya inatakiwa iwe na Kamati ya Wilaya ya Maadili ya Watumishi wa Mahakama. Sasa Wabunge tuhakikishe tunapofika Wilayani kwetu tumuulize Mkuu wa Wilaya kama tayari ameunda Kamati hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati hii itatusaidia sana kwa sababu Wajumbe wake ni Mkuu wa Wilaya ambaye anakuwa Mwenyekiti lakini wapo walioonesha kwamba ni tatizo kubwa hilo kwa Wakuu wa Wilaya kuwemo humo. Tulilijadili vizuri hapa, litakwenda vizuri kama Waheshimiwa Wabunge mtasaidia katika kuhamasisha hizi Kamati ziundwe haraka na tuweze kurejesha nidhamu hasa kwenye Mahakama zetu za chini. Mbali na Mkuu wa Wilaya tunaye DAS pale ndiye anakuwa Katibu. Mkuu wa Wilaya anateua Wajumbe wawili mmoja kiongozi wa dini anayeheshimika anaweza kuwa muislamu au mkristo na mtu wa pili atakuwa ni mzee mwenye heshima katika jamii ambaye kila mtu ukisema ameteuliwa wanasema sawa kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Jaji Mfawidhi katika eneo husika atateua wajumbe wawili ambao ni Wanasheria, wanaweza kuwa Mahakimu na Hakimu wa Wilaya vilevile anakuwa ni sehemu ya hiyo Kamati. Kwa hiyo, madudududu kama hayo yapelekwe moja kwa moja kwenye hiyo Kamati. Hiyo Kamati haina mamlaka ya mwisho itapeleka mapendekezo yake kwenye Judicial Service Commission ambacho ni chombo cha kikatiba. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge tukifanya vizuri hapa, tunaweze tukaleta mabadiliko makubwa sana badala ya sisi kuwa tunalalamika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa George Lubeleje ameongelea uhitaji wa miundombinu ya Mahakama katika Wilaya ya Mpwapwa. Mheshimiwa Omary ameongelea Wilaya ya Kilindi, nafikiri wengi wameongelea suala hili.
Waheshimiwa Wabunge, katika hotuba yangu nimeeleza kuwa tuna tatizo kubwa la miundombinu ya mahakama. Kama nilivyosema, the ideal situation tulitakiwa tuwe na mahakama zinazofanana angalau na kata tulizonazo maana tunaamini kuwa proper access to justice nchini kwetu inahitaji mahakama moja katika kila kata. Tuna kata 3,957 lakini tuna Mahakama za Mwanzo 976 tu!
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi naupongeza sana uongozi wa Mahakama chini ya Jaji Mkuu Othman Chande na Mtendaji Mkuu Katanga kwa kazi nzuri ambayo wameifanya katika kipindi kifupi sana kwa kuanza kampeni ya ujenzi wa Mahakama za Mwanzo za Wilaya na kwa kweli hata Mahakama Kuu, hata jengo la Mahakama ya Rufani hatuna. Kwa hiyo, tulikuwa tumelala kidogo kipindi kirefu sasa hivi ndiyo tumeamka na hawa watu wanahitaji kutiwa moyo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameliezea vizuri sana suala alilokuwa analalamikia mdogo wangu Mheshimiwa Tundu Lissu hapa kuhusu instrument ya mpangilio wa kazi za Mawaziri. Kaeleza vizuri kwamba mbona instrument ilishatoka? Tt the same time, it is not such a big deal mpaka Mheshimiwa Tundu Lissu unasahau kwamba sisi ni kaka zako, tumekusomesha sisi mpaka unaongea maneno mazito kutuita wajinga lakini sasa walimu wako wakiwa wajinga wewe unafikiri utakuwa nani? You could even be worse than that. Kwa sababu sisi kwenye Wizara bahati mbaya ni kaka zako. Niko na Profesa Mchome pale, ni mwalimu wako. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Rais anapoteua Mawaziri anatumia Katiba, Ibara ya 55. Akishamteua Waziri kuna condition moja tu inakuwa imebaki ili Waziri aweze kufanya kazi siyo lazima iwepo instrument! Ibara ya 56 inasema; ―Waziri au Naibu Waziri hatashika madaraka yake ila mpaka awe ameapa kwanza mbele ya Rais Kiapo cha Uaminifu na pia kiapo kingine chochote kinachohusika na utendaji wa kazi yake kinachowekwa kwa mujibu wa sheria inayotungwa na Bunge.‖
Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna instrument hapa ili uwe Waziri! Rais anaweza akaacha hata akakaa miaka mitatu bila instrument lakini Serikali ikaenda. Maana tumefika mahali pa kuona kuwa hata Waziri Mkuu alikuwa anafanya kazi bila uhalalai, hapana! Tusome vizuri Katiba Ibara ya 52 imempa kazi ya kufanya Waziri Mkuu. Inasema; ―Waziri Mkuu atakuwa na madaraka juu ya udhibiti, usimamiaji, utekelezaji wa siku hata siku wa kazi na shughuli za Serikali ya Jamhuri ya Muungano.‖
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kusema tu kwamba tusilitie chumvi sana hoja hii, tukafika mahali kusema kwamba tulikuwa tumepotea, hapana! Hii ni Serikali ya Awamu ya Tano, Rais anafanya mabadiliko makubwa katika mfumo wa Serikali ilibidi tumpe muda kuweza ku-come-up na hiyo instrument ambayo tayari alishaitoa. Watanzania bahati nzuri mimi nafurahi kwamba wame-appreciate kazi anayoifanya ni kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kakunda yeye anadai ameachia Ofisi ya Mbunge Sikonge ili iwe ya Mahakama. Dah! Sasa hapa ni kazi kwa sababu siyo kila ofisi inaweza ikatosha kuwa Mahakama na Ofisi ya Mahakimu. Mimi nashukuru tu kwamba umetupa hiyo ofisi, kwa heshima na taadhima tutafika kuiangalia. Nitaongea na Mtendaji Mkuu wa Mahakama aangalie kama miundombinu ya kuweza kufanya hiyo kazi ipo. Cha msingi ni kwamba Sikonge tumeiweka kwenye orodha ya Wilaya ambazo tutazijengea Mahakama, uwe na subira tu, usiende haraka sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Sheria ya Manunuzi, Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali nakushukuru sana umelijibu, umelimaliza suala hili. Haikuwa kazi rahisi Waheshimiwa Wabunge kuipitia sheria hii. Wengi wanaisema tu hawajawahi kuiona wala kuosoma. Mimi ningesema nipitishe mtihani hapa, sitaki kusema! Maana hii sheria ina vifungu 108, ina majedwali makubwa matatu na ina Kanuni zake 380 na majedwali ya Kanuni 19.
Watanzania hatupendi kusoma tunakimbilia tu magazeti ya Tanzania Daima na kadhalika, lakini hii document iko hivyo. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, muda wangu ni mfupi sana, Mheshimiwa Koshuma naye ameongelea kuhusu Sheria ya Ndoa. Tulishasema hili suala Serikali imelipa kipaumbele sana. Katika Mkutano huu huu nilishasema, hata hivi juzi nilisema tutaleta mapendekezo ya kubadilisha Sheria ya Elimu ili mtoto yeyote ambaye yuko shule ya msingi na sekondari ni marufuku kuoa au kuolewa na ni marufuku kupata mimba! Sasa hiyo marufuku tutaisimamia namna ya kuifanya, tutaileta hapa ninyi wenyewe ndiyo wazazi mtaona hiyo marufuku ya kupata mimba tutaifanyafanyaje. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa anasema kwamba eti Serikali inashindwa kesi nyingi sana! Unachosema una uhakika nacho? Unajua hili Bunge linahitaji facts. Mimi sasa nafikiri nitakuja hapa niwaeleze jinsi ambavyo vijana wetu wanavyofanya kazi nzuri na ya ajabu sana katika mazingira magumu sana. Tuna Ofisi ya Mwendesha Mashtaka, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, wanafanya kazi kubwa sana under extremely difficult conditions lakini wanashinda kesi dhidi ya matajiri, watu wenye kesi kubwa na Mawakili wanaolipwa sana, vijana wetu hata nyumba za kukaa hawana. Kwa hiyo, tusiwakatishe tamaa vijana wetu, kazi wanayoifanya ni kubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu haraka haraka mambo mawili, matatu. La kwanza, Mheshimiwa Tundu Lissu alikuwa anauliza hivi Jaji Mkuu atastaafu lini? Mimi namwomba mdogo wangu awe anasomasoma hii Katiba kwani Ibara ya 120 ina majibu, sikutegemea wewe uulize swali hilo.
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Ana umri gani? Jibu lipo hapa kwenye Ibara ya 120(2) ambayo inasema kwamba; ―Jaji yeyote wa Rufani aweza kustaafu Ujaji wa Rufani wakati wowote baada ya kutimiza umri wa miaka sitini, isipokuwa kama Rais ataagiza kwamba asistaafu, na iwapo Rais ataagiza hivyo basi, huyo Jaji wa Rufani atakayehusika na maagizo hayo ya Rais hatakuwa na haki ya kustaafu mpaka upite kwanza muda wowote utakaotajwa na Rais kwa ajili hiyo.‖ (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 120(3) inaendelea kusema kwamba; ―Iwapo Rais ataona kuwa kwa ajili ya manufaa ya umma inafaa Jaji wa Rufani aliyetimiza umri wa miaka sitini na tano aendelee kufanya kazi, na Jaji huyo wa Rufani anakubali kwa maandishi kuendelea kufanya kazi, basi Rais aweza kuagiza kwamba...
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unaweza ukafika miaka sabini na zaidi, yote iko ndani ya Katiba. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo mengi mazito yameongelewa hapa. Mheshimiwa Maige anasema Jimboni kwake kuna majengo mazuri ya mahakama lakini hakuna Hakimu. Hili nalisikia na Ndugu yangu Katanga akisikia hivyo atashtuka sana kwamba kuna majengo mazuri Jimboni kwa Maige lakini hakuna Hakimu, tutalifuatilia hili kwa karibu sana tena sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mbunge wa Ulanga, Bwana Mdogo Mheshimiwa Goodluck Mlinga anasema kwake hakuna miundombinu ya Mahakama. Umenishtua sana, sisi hatupendi kusikia kitu kama hicho kwamba Wilaya ipo lakini hakuna kabisa miundombinu. Nitakaa na ndugu zangu upande wa Mahakama tuweze kutembelea Jimbo lako na mimi nakuhakikishia kuwa kama hali ni mbaya kiasi hicho hatuwezi kuliacha Jimbo lako la Ulanga kwenye mpango wa miaka mitano wa ujenzi wa Mahakama za Wilaya na Mahakama za Mwanzo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli nimeelewa masuala aliyoyalalamikia Mheshimiwa Augustine Holle ya sheria za kazi na hali ya migodini. Wakati wataalam wa Tume ya Kurekebisha Sheria bado wako hapa, hata kesho tunaweza tukapata muda kukusikiliza ulete yote unayofikiria ni muhimu tuyaangalie.
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mengi hapa yameongelewa, pengine niongelee la mwisho la Mheshimiwa Tindu Lissu kuhusu kuanzishwa Mahakama ya Mafisadi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuwa na Mahakama ya Wahujumu Uchumi, ni kweli. Tulivyoanza, pengine huwezi kukumbuka ulikuwa bado mdogo pengine shule ya msingi, tulipoanza na hiyo Mahakama it was a non-starter kwa sababu it was a tribunal nje ya mfumo rasmi wa Mahakama. Kwa hiyo, hiyo tribunal sisi tukiwa university tuliipinga sana na ilibidi sasa ibadilishwe tena ikawa appeal zinakwenda kwa Rais. Sasa hiyo ndiyo ikawa mbaya zaidi na ikashindikana, ndipo marekebisho yakaja kwamba High Court yenyewe inaweza ikasikiliza hizo economic crimes cases. Kwa taarifa tu ni kwamba kuanzia mwaka 2011 mpaka leo mimi sijaona kesi pale, wewe mwenyewe ni Wakili hujaona Mahakama Kuu ikisikiliza kesi za namna hiyo kama Mahakama ya Uhujumu Uchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, lengo kubwa hapa ni kurekebisha hitilafu tulizokuwanazo katika msururu wa sheria zetu hizi tuje na kitu kizuri zaidi, tutakileta mbele yenu hapa si muda mrefu. Atakayeileta hapa ni yule yule Mwanasheria wetu Mkuu mahiri George Masaju ambaye mimi nimekaa naye muda mrefu na mimi nawaambia hii ndiyo kamusi ya weledi upande wa sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja ya Rais kuonekana ni dikteta! Mimi imenishangaza sana! Maneno yanayoongelewa hayafai, eti Mawaziri wanaogopa, Rais hashauriwi! Jamani!
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu dakika mbili hizi nimalizie, unajua hii mimi inanikumbusha kuhusu mchezo wa mpira. Ukienda kuangalia watu wanaangalia screen inacheza timu nzito kama Barcelona na Manchester, utaona sasa pale wanaoangalia wanajua zaidi mpira kuliko wanaocheza! Unamsikia mtu anasema aah Messi angedokoa tu pale kidogo kwa kisigino, wewe! Ukimwangalia mtu mwenyewe pengine ana miguu yote ya kushoto utadokoa vipi mpira pale? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna hilo tatizo hapa! Tunajua zaidi kupita watu ambao wako jikoni! Sisi tuna uzoefu wa kuendesha Serikali. Unapomwona Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ametoa directive, hiyo directive imetolewa na presidency! Sisi kama Mawaziri, we are part of that presidency. Haiwezekani leo Rais amesema twende kushoto unafikiri ameamua mwenyewe? Ana cabinet yake ni sisi tuko sehemu yake. Kwa hiyo, siyo uwoga ndiyo utaratibu wa kuendesha Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Ndugu zangu mnajua mambo yalikuwa hayaendi vizuri sana, Rais amejitahidi kwa kweli kurekebisha mambo mengi sana. Amejitoa sana kiongozi wetu, kafanya mambo mengi ambayo hayajapata kutokea na dunia nzima inamuimba leo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kuondoa pesa za sherehe akanunulia vitanda Muhimbili ni udikteta? Kuondoa fedha za sherehe akajenga barabara ni udikteta? Ndugu zangu itakuwa tunayoongea hapa ni tofauti kabisa na thinking ya public huko nje. Hicho kitu kinampa Mheshimiwa Rais comfort kubwa ndani ya moyo kwa sababu wananchi wanachokisema kinamtia moyo sana. Sisi wenyewe hapa tulikuwa tunalalamika ooh, uongozi huu legelege, dhaifu, limekuja tingatinga, malalamiko tena eee, nini tena? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia kengele ikilia, kwa mara nyingine tena mimi nakushukuru wewe binafsi kwa kutuongoza vyema katika mjadala wa bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria. Nawashukuru pia Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika mjadala huu…
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunaongea halafu kuna vichaa humu ndani wanaongeaongea...
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunaongea halafu kuna vichaa humu ndani wanaongeaongea...
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Halima Mdee, tafadhali.
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mimi nashindwa kuelewa sijui wanakula yale majani yale, sielewi?
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi napenda tu kurudia kuahidi kwamba maoni na ushauri ambao Waheshimiwa Wabunge mmeutoa tuta-compile na tutawaletea majibu yake yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.