Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2018

MHE. ANTHONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nianze na mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazingira ni kitu cha muhimu sana na ni kitu ambacho ni cha kufa na kupona, kwa sababu bila mazingira binadamu anaweza kuwa hatarini kutoweka kama viumbe vingine ambavyo vinatishika sasa hivi kutoweka. Uwekezaji unaofanywa katika mazingira hauakisi hali hiyo. Kwa hiyo, niungane na Kamati kwamba iko haja ya Bunge kuisukuma zaidi Serikali kuona umuhimu wa mazingira na kuwekeza inavyotakiwa katika mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hii kauli ya Mheshimiwa Rais ya juzi kwamba watu sasa wanaruhusiwa kufanya shughuli za kibinadamu kwenye maeneo yale ambayo ni tengefu na maeneo ya vyanzo vya maji. Sisi hatuna ugomvi na hilo, lakini tunasema kama kweli tunataka kufanya kazi kwa misingi ya kisheria na ili isiwe hii ni kugawa peremende kwa sababu za kiuchaguzi, halafu baada ya uchaguzi wananchi waje wapate taabu kama wanavyopata kwenye maeneo mengine, Serikali ilete sheria, ilete mapendekezo ya marekebisho ya sheria, tuijadili hapa Bungeni, tuipitishe, ili watakaokwenda kufanya shughuli za kibinadamu kwenye maeneo hayo ambayo Mheshimiwa Rais ameyasema, yaweze kuwa salama hata baada ya uchaguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hivyo, niende sasa kwenye Kamati ya Viwanda na Biashara. Kumekuwepo na kutokutekeleza mikakati mbalimbali ambayo tunaiweka. Hii mimi nasema kinachofanyika kwa kweli ni matamko tu, siyo mkakati. Ukiangalia, kuna mambo mengi ambayo yametajwa katika mpango wetu wa miaka mitano wa maendeleo. Leo ukiangalia ni kwa kiasi gani tunatekeleza yale ambayo tumeyaazimia, utashangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwepo na miradi ya kimkakati, mfano ujenzi wa viwanda ambavyo vinaweza vikachochea mageuzi ya viwanda katika nchi hii. Hivyo viwanda viko vingi. Kuna Kiwanda cha General Tyre, Mheshimiwa Lema amesema sana hapa, hakuna chochote pamoja na uwekezaji mkubwa ambao unazidi zaidi ya shilingi bilioni 20 ambao umekwenda kule. Pesa zile zimetupwa tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi wa Mchuchuma na Liganga, kuna zaidi ya shilingi bilioni 20 nazo zimetupwa tu. Kuna Mradi wa Magadi Soda Engaruka, kuna zaidi ya shilingi bilioni sita zimekwenda kule, hakuna chochote kinachoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika hali kama hiyo, nafikiri ipo haja ya kuangalia upya; na ili Bunge liweze kufika mahali pa kutoa maelekezo kwa Serikali, ili tuwe na vipaumbele ambavyo tunavifanyia kazi na tusiwe na haya matamko ambayo kwa namna moja ama nyingine yanaendelea kutumika kama vichochoro kwa ajili ya kutengea fedha na kupiga fedha. Kwa sababu ukiangalia Kamati inavyosema, Kiwanda cha General Tyre ni kama hakipo tena na hakitawezekana, lakini utashangaa mapendekezo ya bajeti yatakapokuja hapa, wanasema tunahitaji shilingi fulani kwa ajili ya kwenda kufanya utafiti, na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipo Kiwanda cha Urafiki ambapo sisi Tanzania ni wabia kwa asilimia 49, lakini kwenye Hotuba ya Kamati hapa wamesema kuna fedha zilikopwa na wabia wenzao wale wa China, wameandika pale Yu 217,000 lakini Kamati inasema haifahamu hizo fedha zilikwenda wapi na zilifanyia nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Kamati inasema hivyo, mwakilishi wetu pale ambaye ni Serikali, hajui kwamba hizo fedha zilizokopwa zilikweda kufanya nini na ziko wapi? Sasa katika hali ya namna hiyo ni kitu ambacho kwa kweli, kinaleta kichefuchefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hiyo miradi, kuna mtu alizungumza hapa akasema tunawasifia Serikali ya Awamu ya Tano kwa kufanya radical change. Sasa radical change kwenye kitu gani? Ingekuwa radical change mngetuambia leo mnajenga Mchuchuma na Liganga. Ingekuwa ni radical change mngesema mnajenga Engaruka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nim-quote Mheshimiwa Waziri Stephen Wassira. Wakati fulani akiwa anawasilisha Mpango wa Mapendekezo ya Mpango wa Taifa wa mwaka 2014/2015 alisema hivi: “Kwa upande wa Mradi wa Magadi Soda Bonde la Engaruka, Arusha, kazi ya kuchonga mashimo 12 kwa ajili ya uhakiki wingi na ubora na magadi umekamilika, ambapo imebainika kuwa eneo la Engaruka lina magadi yenye mita za ujazo bilioni 4.68 kiasi ambacho ni kikubwa kutosheleza uchimbaji wa magadi soda kwa zaidi ya miaka 400. Upatikanaji wa magadi soda utasaidia katika viwanda vya madawa, sabuni, nguo, rangi na viwanda vya kuchakata chuma.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilivyosoma hii, nikajua kumbe ndiyo maana Mheshimiwa Stephen Wassira anataka kurudi tena agombee Urais. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, liko Bwawa la Kidunda ambapo tungelijenga, linahitaji uwekezaji wa shilingi bilioni 251, leo tusingekuwa tunaenda kwenye Stiegler’s Gorge kwa sababu tungepata umeme, tungepeta maji ya kumwagilia, tungepata uchumi mkubwa wa miwa, utalii na uvuvi. Sijui tumelogwa na nani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna uchumi wa gesi ambao ulihubiriwa sana, lakini leo tumeshafika 7% tu ya utilization, mbali na uwekezaji mkubwa tuliouweka pale kujenga bomba kutoka kule Mtwara mpaka Dar es Salaam kwa pesa ya mkopo ambayo tunapaswa tulipe miaka na miaka na hakuna chochote ambacho mnasema. Leo mnasema mnafanya radical change, mnafanya radical change kwenye kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya biashara; na hapa nataka nimrejee ndugu yangu Mwalimu wangu Mheshimiwa Dkt. Mpango. Katika hali ya biashara, wakati wanawasilisha mapendekezo ya hali ya uchumi alisema watahakikisha kunakuwepo na kufungamanisha uchumi na maendeleo ya watu. Wakasema watajenga mazingira wezeshi kwa ajili ya uwekezaji, na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hawa Waheshimiwa walivyoingia madarakani, kwa mujibu wa Benki yetu Kuu ya Tanzania, ile economic monthly review, deni la ndani, ambapo walisema vilevile watalipunguza, Novemba, 2015, lilikuwa shilingi trilioni 7.9. Leo, yaani mwaka 2018 kwa takwimu za Benki Kuu ya Tanzania, deni la ndani ni shilingi trilioni 14. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hiyo radical change iko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Tanzania World Bank Economic Update, Report Number 11, utakuta umasikini katika nchi hii kwa kipindi hiki cha Serikali ya Awamu ya Tano, wamezalisha watu masikini kwa miaka hii mitatu, milioni mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye urahisi wa kufanya biashara, hali imeendelea kuwa mbaya. Kuanzisha biashara tulikuwa wa 129 mwaka 2015, leo ni wa 162. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vibali vya ujenzi tulikuwa wa 126, leo ni 156. Kusajili mali (property) tulikuwa wa 133, leo ni 142. Kupata umeme tulikuwa wa 83, hapo tumepiga hatua kidogo kwa moja, tuko 82 sasa hivi. Biashara mpakani tulikuwa wa 180, leo wa 182.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii ni kwa sababu ya sera mbaya, ni kwa sababu ya misururu ya kodi, ni kwa sababu ya taasisi nyingi za udhibiti, ni kwa sababu ya kukosekana one stop window; ni kwa sababu ya Sheria za Kodi zisizokuwa rafiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Serikali imeamua kufanya biashara na kuacha jukumu lake la msingi la kisera la kuwa facilitator, kuwa mwezeshaji; imeamua kuwa mshindani. Mifano ipo. Leo tunafanya biashara ya kwenye ATCL kwa asilimia 100, that is very wrong.

Sasa leo tunaenda kununua korosho.

MBUNGE FULANI: Wamelipa mikopo ya benki.

MHE. ANTHONY C. KOMU: Leo tunaenda kuingia kwenye biashara ya korosho kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, akili ya kawaida, sisi tulipaswa tufanye subsidy, tulipaswa tu subsidize. Kama walikuwepo wafanyabiashara waliotaka kununua ile korosho kwa shilingi 2,700/=, sisi tungewaongezea hiyo shilingi 600/= tukawakopesha. Leo tungekuwa tunahitaji shilingi bilioni 200 tumalize biashara ya korosho. Leo tunataka shilingi bilioni 900, tumechukua Jeshi letu la Wananchi wako kule wanapigana vikumbo na wananchi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeua kabisa mfumo wa korosho. Baada ya mwaka huu kwisha, nani atanunua tena korosho? Mwaka kesho tena Serikali wataenda kununua korosho? Mmeua Bodi ya Korosho, mmeshindwa kui-replace? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hili tatizo la korosho, kwa mujibu wa hii economic review, maana sijui Economic Review ya Benki yetu ya Tanzania, kwenye balance payment tume-experience deficit ya dola milioni 500. Halafu mnasema mnafanya radical change. Ipi? (Makofi)

MBUNGE FULANI: Wapi?

MHE. ANTHONY C. KOMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninawaomba sana; wafanyabiashara waliokuwa wanafanya biashara za ku--supply stationaries sijui kwenye Jeshi la Polisi, waliokuwa wanafanya biashara ya kuchapa vitu mbalimbali, leo wanaofanya ni TISS, Usalama wa Taifa. Wanaenda kufanya… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)