Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2018 Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Usimamizi wa Matumizi ya Fedha za Umma katika Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2017

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kwa kuwa ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC mchango wangu utajikita katika taarifa iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati yetu ya LAAC. Kwanza nianze kuipongeza TAMISEMI kwa hatua ambazo zinachukuliwa kwa sababu ukisoma hikhi kitabu cha taarifa ya CAG inaonekana kuna maboresha katika hati zinazopatikana. Hati za kuridhisha kwa councils ambazo zilikaguliwa mwaka jana 185, kuna ongezeko la halmashauri ambazo zimepata hati ambayo inaridhisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia takwimu utaona kwamba kwa taarifa ya mwaka 2015/2016 tulikuwa na councils 135 kati ya 171 ndio zilipata hati ya kuridhisha, lakini taarifa hii tunayoijadili kuna ongezeko, mwaka huu kuna halmashauri 165 zimepata hati ya kuridhisha kati ya halmashauri 185 ambazo ni sawa na 90%. Kwa hiyo, niwapongeze sana TAMISEMI kwa shughuli za ufuatiliaji ambazo zinafanywa na matokeo yake tunaanza kuyaona sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu halmashauri ambazo zinapata hati za mashaka nazo zinaanza kupungua, ukiacha halmashauri za Kigoma Ujiji ambayo imepata hati mbaya kwa miaka mitatu mfululizo, lakini katika maeneo mengine kuna maboresho ambayo yanaonekana. Kwa hiyo kwa sababu Waheshimiwa Wabunge ni Madiwani, nimshauri kaka yangu Mheshimiwa Zitto kwamba naye awe anahudhuria vikao vya Kamati ya Fedha ili inapojadiliwa ripoti ya CAG na yeye aweke inputs zake kwa sababu kupata hati isiyoridhisha kwa miaka mitatu mfululizo ni kitu kisicho cha kawaida na kinahitaji intervention za haraka ili Kigoma Ujiji iweze kupata hati safi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizi sasa nichukue nafasi hii kuishauri TAMISEMI, kama walivyosema wenzangu kwenye taarifa yetu tumesema matatizo yote ambayo yanatokea katika halmashauri zetu sababu kubwa ambayo inasabisha ni mifumo yetu ya ndani kutokuwa imara. Kwa hiyo mifumo wa udhibiti wa ndani inabidi iimarishwe. Tunapozungumzia mifumo ya udhibiti wa ndani tunaangalia Kitengo cha Ukaguzi, Kamati za Ukaguzi za Wilaya, matumizi ya TEHAMA katika ukaguaji au ufungaji wa hesabu, kuwepo kwa sera ya viashiria hatarishi na vilevile kuwa na fraud assessment. Kwa hiyo hayo yakizingatiwa, tutapunguza sana ubadhirifu ambao unatokea katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma agizo la 12, Local Authority Financial Memorandum kuna agizo kabisa limetolewa pale kwamba, kila halmashauri lazima kuwe na Kitengo cha Ndani. Changamoto iliyopo kwenye Kitengo chetu cha Ukaguzi wa ndani ni kukosekana kwa rasilimali fedha na rasilimali watu. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kama walivyopendekeza kwenye Kamati yetu, TAMISEMI na kwa kushirikiana na Mkaguzi Mkuu ambaye yupo Wizara ya Fedha Internal Auditor General, basi waimarishe kitengo hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma kulikuwa na jitihada za makusudi TAMISEMI walikuwa wanahangaika na vitendea kazi, lakini na Interanal Auditor General ambaye yupo Wizara ya Fedha na Mipango ambaye alikuwa anatoa mafunzo kwa Wakaguzi wa Ndani. Kwa hiyo tunaiomba Serikali sasa kurejesha yale mafunzo ili Wakaguzi wetu waweze kuwa na ujuzi wa kuweza kufanya kazi yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, ripoti hii inaonesha wazi kwamba kuna uchache, ikama inasema kila halmashauri kuwe na Wakaguzi wasiopungua wane, lakini halmashauri nyingi ambazo zilikuja ndani ya Kamati zina Mkaguzi wa Ndani mmoja au wawili. Kwa hiyo wanashindwa kutekeleza majukumu yao. Kama tulivyopendekeza kwenye ripoti yetu kwamba, Serikali ichukue jitihada za makusudi kuomba kibali cha jumla ili Wakaguzi wa Ndani waweze kuajiriwa na wasambazwe kwenye halmashauri kwa ajili ya kuimarisha Kitengo hiki cha Ukaguzi wa Ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la Kamati za Ukaguzi, ukisoma agizo la 13 la Local Authority Financial Memorandum, zinazitaka halmashauri kuwa na Kamati za Ukaguzi na Mwenyekiti atoke nje ya ile taasisi, lakini hapa kinachoendelea ni tofauti, halmashauri nyingi ambazo zimekuja kwenye mahojiano, Wakuu wa Idara au watendaji wa halmashauri ndio walikuwa Wenyeviti wa hizo Kamati, kinyume na mwongozo ambao umetolewa na Wizara na kinyume na agizo hili hapa. Kwa hiyo naomba TAMISEMI kusimamia kwa karibu ili halmashauri zote zipate Wenyeviti wa Kamati za Ukaguzi ambao wanatoka nje ya taasisi ili kuimarisha kamati kwa ajili ya kuweza kutimiza majukumu yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye udhibiti wa ndani kuna suala la TEHAMA; kumekuwa na mtindo sasa hivi mwezi wa Saba, mwezi wa Nane halmashauri zinasimama kila kitu, ukiuliza wanasema mfumo, Madiwani hawalipwi, vikao haviendelei, hakuna malipo yanayoendelea. Tulipofanya mahojiano na TAMISEMI, walisema hakuna kitu kama hicho, tatizo ni changamoto ya utalaam. Kwa hiyo naiomba Serikali kutoa mafunzo, kama tulivyopendekeza kwenye taarifa yetu, kwa wataalam ili kusiwe na kisingizio kwamba mwezi wa Saba na wa Nane hakuna kinachoendelea halmashauri kwa sababu ya kusingizia hiyo mifumo iliyopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni mafunzo kwa hawa Wakaguzi; inachekesha sana kwamba kuna mifumo mingi ambayo Serikali imeanzisha tuna EPICOR, Lawson kwa ajili ya mishahara, tuna ile ya kukusanya mapato (LGRCIS), lakini Mkaguzi wa Ndani hajapata mafunzo jinsi ya kuingia kwenye mifumo hii. Kwa hiyo, Mkaguzi wa Ndani anapokwenda kukagua anakumbana na changamoto ya matumizi ya mifumo hii. Hivyo, kama tulivyoshauri kwenye Kamati yetu Internal Auditor General ambaye ipo Wizara ya Fedha na Mipango na TAMISEMI wahakikishe kwamba Wakaguzi wetu wa Ndani wanapata mafunzo ya kutosha ili waweze ku-assess hii mifumo ambayo imeanzishwa kwenye halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze TAMISEMi kwa kuanzisha kitengo cha ukaguzi na ufuatiliaji wa fedha katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Hiki ni kitengo muhimu sana na kitengo hiki kikiimarishwa kitasaidia sana kupunguza ubadhirifu au utekelezaji wa miradi usioridhisha katika halmashauri zetu. Tulipowahoji maafisa ambao wapo kwenye kitengo hiki kuna changamoto kubwa sana, kitengo kimeanzishwa lakini ni ombaomba, tunaomba Wizara ya Fedha na TAMISEMI ihakikishe kwenye bajeti inatenga fedha za kutosha ili kitengo hiki kiwezi kutekeleza majukumu yake. Ni kitengo kizuri ambacho kikiimarishwa kitazuia ubadhirifu ambao unatokea kwenye halmashauri zetu kabla CAG hajaingia.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kitengo hiki kina watumishi wachache lazima kiongezewe watumishi kitengo hiki ili kiweze kutekeleza majukumu yake na kitengo hiki pia kiwezeshwe kutumia mifumo iliyopo ya TAMISEMI iliyopo sasa hivi ili waweze ku-assess ku-information, sio lazima wakimbie kwenye halmashauri, wanaweza kuitisha taarifa zilizopo kwenye mifumo na wakajua kwamba kwenye halmashauri X kuna changamoto hii na baadaye wakaenda kufuatilia kule kule kwenye halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kitengo hiki kikiimarishwa kitasaidia na kitapunguza wazo ambalo watu wanalo, kuna watu wana wazo kwamba Internal Audit asiwe sehemu ya Mkurugenzi, sasa Internal Auditor akiwa nje ya Mkurugenzi inavuruga maana ya kuwepo Internal Auditor, Internal Auditor kile kitengo kimeungwa ili liwe jicho la Mkurugenzi au Afisa Masuuli. Internal Auditor akitolewa nje ya ofisi huyu atakuwa External Auditor mwingine, kwa hiyo tukiimarisha kitengo hiki itasaidia kutoa ishara kwa Mkurugenzi kwamba idara yako X kuna hali mbaya, kwa hiyo chukua hatua haraka. Kwa hiyo, napendekeza kitengo kiimarishwe na sio kuondolewa kwenye Ofisi ya Afisa Masuuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie mchango wangu kuhusu utekelezaji wa miradi kwenye Halmashauri zetu. Kuna changamoto nyingi sana katika kutekeleza miradi kwenye Halmashauri yetu. Changamoto ya kwanza, ni fedha kupelekwa pungufu. Fedha zinatengwa kwenye bajeti lakini hazipelekwi na hivyo mipango ya Halmashauri kushindwa kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba TAMISEMI kila wanapopata fedha wahakikishe kwamba wanapeleka kwenye mamlaka ya Serikali za Mitaa ili waweze kutekeleza miradi kwa wakati. Kuna wakati mwingine tunaambiwa Halmashauri hazina uwezo, kumbe tunapeleka fedha Mei, 30 halafu tunawaambia watekeleze mradi. Mradi huu hauwezi kutekelezeka kwa sababu procurement process yenyewe inachukua siku nyingi. Kwa hiyo, mpaka kumaliza mchakato wa manunuzi fedha zile zitakuwa bakaa kwenye mwaka unaofuata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ni gharama za mradi kama ilivyoelezwa kwenye taarifa yetu pale Morogoro Manispaa tuliona mradi wa lami ambao ni wa kilomita 4.6 lakini unagharimu takribani shilingi bilioni 12. Sisi kwa hesabu zetu za haraka fedha zile zingeweza kujenga zaidi ya kilomita 10. Tulipouliza kwenye Halmashauri zingine viwango vinakuwa tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Kitengo cha Usimamizi wa Miradi kwenye Halmashauri kilichopo TAMISEMI lazima tuweke standard za miradi yetu, standard za utekelezaji katika mamlaka ya Serikali za Mitaa ili kutotoa mwanya kwa wale ambao wana nia mbaya ya kupiga fedha za Halmashauri wasiweze kufanya hivyo. Tunapokuwa na viwango tofauti na Halmashauri inajiamulia kwamba nitajenga barabara kilomita 1 kwa shilingi bilioni 3, mwingine anajenga kilomita 1 kwa shilingi bilioni 2, hapo lazima upotevu wa fedha utajitokeza. Kwa hiyo, naomba Kitengo cha Usimamizi wa Fedha TAMISEMI, Kitengo kinachosimamia miradi kihakikishe kinatoa standard ili miradi yetu tuweze kutekeleza kwa kile kiwango ambacho tumekikusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema mimi ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC, naunga mkono taarifa ya Kamati yetu kwa asilimia 100 na nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)