Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga soko la kisasa la mazao yatokanayo na uvuvi Wilayani Nkasi?

Supplementary Question 1

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Waziri mwaka 2016 Serikali iliwekeza fedha kwenye mwalo wa Kirando wenye thamani ya shilingi bilioni 1.1. Lakini mwaka 2019 mwalo huo ulizama ikiwepo Kasanga pamoja na maeneo mengine yote ya Ziwa Tanganyika. Nataka kujua Serikali ina mkakati gani wa ziada wa kujengwa mwalo mwingine na kuupandisha hadhi kama ulivyosema kwenye Kata ya Kirando?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ili kunufaika na mazao yatokanayo na uvuvi kwenye ushindani wa soko ni lazima Serikali iwekeze kwenye kulinda mazalia ya samaki. Napenda kujua Serikali ina mkakati gani wa ziada wa kulinda mazalia ya samaki bila kuathiri wavuvi wetu? (Makofi)

Name

Abdallah Hamis Ulega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkuranga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza Serikali imeshatoa maelekezo kwa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kupendekeza maeneo wanayodhani kuwa yanaweza kufaa sasa mara baada ya maji kuingia katika mwalo ule wa mwanzo, na mara baada ya kupendekeza tutakuja kufanya tathmini ili tujiridhishe na mchakato sasa wa ujenzi uweze kuanza.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili juu ya mazalia; mazalia ya samaki nini mkakati wetu ni kwamba Serikali la kwanza kwa kushirikiana na jamii tuko tayari na tunajipanga katika kuyatambua, kuyaainisha na kuyatangaza kwa mujibu wa sheria ili baadae tuweze kuyalinda na naomba niihase jamii ya wavuvi maeneo yote nchini ya kwamba kazi ya kulinda rasilimali hizi hususan maeneo ya mazalia ni kazi ya jamii nzima, Serikali za Vijiji, Serikali za Kata, Serikali mpaka Wilaya na Mikoa ni kazi yetu sote Watanzania.

Mheshimiwa Spika, bila ya kulinda mazalia samaki wetu watakwisha na hatua kali tutaichukua kwa yeyote anayefanya maingilio ya kwenda katika kufanya kazi ya uvuvi kwenye eneo la mazalia. Huo ni uhalifu na hatutamvumilia yeyote ambaye atakwenda kuharibu rasilimali hii ya Watanzania.