Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Primary Question

MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: - Je, lini Serikali itafufua kilimo cha pamba katika Wilaya ya Kilwa?

Supplementary Question 1

MHE. FRANSIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naona majibu ya Mheshimiwa Waziri yamekuwa mepesi sana. Hii changamoto ya funza mwekundu iligundulika kwenye miaka ya 1940, sasa ni miaka zaidi ya 80 imepita bado hatujapata solution kuhusiana na changamoto hii. Je, Serikali ina mikakati gani madhubuti, ningeomba tuelezwe kwa kutumia teknolojia ya kisasa kuweza kutatua changamoto hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; ningependa kujua, kuna mazao mengina ya michungwa, ufuta na minazi ambayo yanalimwa sana katika Wilaya ya Kilwa, ningependa kutaka kujua, je, Serikali imeishirikisha vipi taasisi TARI katika kutatua matatizo ya magonjwa ya mazao haya?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mdudu huyu alitambulika muda mrefu na kama Serikali tumeendelea kuwekeza katika kufanya utafiti kushirikiana na wadau wengi wa kimataifa. Lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunamtokomeza mdudu huyu ambaye kila muda anaendelea kujipa maumbo tofauti tofauti lakini wataalam wetu wa TARI pamoja na wataalam wengine tunaendelea kuifanya kazi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo kubwa ni kuhakikisha tunamtokomeza mdudu huyu ambaye ana athari kubwa katika uzalishaji wa zao la pamba. Hivyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu hivi sasa Mheshimiwa Rais ametoa fedha nyingi kwenye utafiti, tunaamini kupitia fedha hizi wenzetu wa TARI pamoja na mashirika mengine tutafanya kazi hii kwa uaminifu mkubwa kabisa ili mwisho wa siku tupate suluhisho la mdudu huyu na wakulima hao kama ambavyo dhamira yao ya kulima basi tuwe tumemtokomeza mdudu huyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, bajeti yetu ya eneo ya utafiti miaka miwili iliyopita ilikuwa ni shilingi bilioni 11.6. Hivi sasa bajeti yetu ni shilingi bilioni 43 kwenye utafiti. Moja ya maeneo makubwa ambayo tumeyapa kipaumbele ni kuhakikisha pia tunakuja na namna bora ya udhibiti wa magonjwa na wadudu wasumbufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mbunge kwamba, TARI imewezeshwa na hivi sasa inaendelea kufanya tafiti ili kuja na suluhisho la kudumu la magonjwa ambayo yamekuwa yakitatiza sana michungwa na minazi. (Makofi)