Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Venance Methusalah Mwamoto

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:- Kwa nini Serikali isifute michezo Tanzania?

Supplementary Question 1

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.
Kwa kuwa sasa hivi suala la michezo Tanzania ni sawasawa na mgonjwa na unapokuwa na mgonjwa aidha umpeleke kwenye maombi, hospitali au kwa mganga wa kienyeji.
Sasa kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amekiri na anajua tatizo hilo na tatizo kubwa limekuwa ni kwamba Serikali imeshindwa kuwekeza kutoka chini kwa maana ya kwenye shule za msingi, UMISHUMTA, UMISETA na michezo mingine na kuifuta, sasa Serikali inasemaje kuhusu kufufua michezo hiyo kwa nguvu zote na kupanga bajeti ya kutosha? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa michezo ni ajira na Serikali ilikiri yenyewe kwamba itahakikisha inapeleka ajira kwa vijana kupitia michezo; na michezo inaleta pato la Taifa kwa mfano nchi kama Nigeria, Cameroon na Ghana imekuwa ni pato, sasa Serikali kwa nini imesahau kwamba hiyo itakuwa ni pato kubwa kwa nchi yetu na kuitelekeza michezo? Naomba jibu. (Makofi)

Name

Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Answer

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, la kwanza Serikali haijafuta michezo ya UMISHUMTA, UMISETA kama ambavyo imekuwa ikikaririwa, isipokuwa mwaka huu kilichotokea ni kwamba michezo hii iliahirishwa kwa muda, kwa sababu ya kuwa na maandalizi ambayo hayakuwa yanaridhisha na hivyo tukasema ni vizuri tujipange upya ili michezo hii iwe na maana.Kwa muda mrefu sasa michezo ya UMISHUMTA, UMISETA imekuwa ikifanyikakama matamasha ikifikia kilele mwishoni hakuna matokeo yanayoendelezwa baada ya michezo ile.
Mheshimiwa Spika, Serikali inajipanga kuhakikisha kwamba, michezo hii sasa inapofikia kilele chake wale wanaofanya vizuri wanapelekwa kwenye shule maalum zitakozotengwa kwenye Mikoa na Wilaya kwa ajili ya kuendeleza vipaji vyao badala ya kutokea kama ambavyo imekuwa ikitokea, michezo ile ikimalizika watoto wanarudi kwenye shule zao na vile vipaji vinapotea.
Mheshimiwa Spika, lakini la pili kwamba suala la uwekezaji kwenye michezo. Ni kweli michezo inahitaji uwekezaji mkubwa, kwa uwekezaji mdogo hatutapata matokeo ya kutosha. Serikali haijatelekeza michezo kama ambavyo nimejibu katika jibu la msingi kwamba Serikali itaendelea kutenga fedha kwenye bajeti zake, lakini na kuangalia vyanzo vingine ambavyo hata wenzetu wamekuwa wakivitumia kuendeleza michezo. Vyanzo vingine ni pamoja na pesa zinazotokana na Bahati Nasibu za Taifa. Duniani kote Michezo ya Bahati Nasibu ya Taifa ndio ambayo imekuwa ikifadhili michezo badala ya kutegemea hii bajeti ndogo.
Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa wito kwa sekta binafsi kushirikiana na Serikali kusaidiana katika kuwekeza katika michezo, tumeona sasa tunakoelekea michezo itakuwa ni biashara kubwa, italipa na hivyo natoa wito kwa wadau mbalimbali kuwekeza katika michezo wakishirikiana na Serikali na tukifanya hivyo tunaamini tutapata matokeo mazuri.