Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 1 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 6 2016-09-06

Name

Venance Methusalah Mwamoto

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:-
Kwa nini Serikali isifute michezo Tanzania?

Name

Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Answer

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Methuselah Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza nimtambue Mheshimiwa Venance Mwamoto kama mwanamichezo ambaye amewahi kucheza mpira wa miguu katika timu ya ligi daraja la kwanza wakati huo, sawa na ligi kuu Tanzania kwa sasa, yaani timu ya Majimaji ya Songea na RTC ya Kagera lakini pia timu ya Taifa.
Mheshimiwa Spika, hapa Bungeni Mheshimiwa Venance Mwamoto ndiye Kocha Mkuu wa timu ya mpira wa miguu ya Bunge. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kufuatia sifa hizo za Mheshimiwa Venance Methuselah Mwamoto, binafsi naamini kuwa swali lake limelenga kupata maelezo ya kwa nini michezo haiendelei kwa kasi wanayotamani wapenda michezo wengi hapa Tanzania na wala siamini kuwa anayo nia ya kutaka Serikali ifute michezo kwa kuwa anafahamu fika umuhimu wa michezo kwa Taifa paoja na wananchi kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Tanzania haiwezi na wala haina nia ya kufuta michezo nchini kwa sababu yoyote ile, badala yake nia ya Serikali ni kuiendeleza sekta hiyo muhimu kwa maendeleo ya Taifa hili kwa kuwekeza katika miundombinu ya michezo, elimu ya michezo ya kushirikiana na wadau wengine kuhakikisha kuwa sekta ya michezo inaendelezwa ipasavyo.
Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge lako Tukufu kushirikiana na Serikali kuhimiza maendeleo ya michezo katika majimbo yetu. Aidha, tunashauri na kuhimiza wadau wote wa michezo ikiwemo Serikali za Mitaa, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Waheshimiwa Wabunge, sekta binafsi na wadau wengine kuibua vipaji vya michezo kwa watoto kuanzia umri mdogo na kuviendeleza.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara na Taasisi zake itaendelea kutenga fedha kupitia bajeti yake na vyanzo vingine kadri inavyowezekana kila wakati ili kuendeleza michezo katika ngazi mbalimbali.