Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:- Kwa miaka ya hivi karibuni vifo vya Watanzania kutokana na ajali za barabarani vimekuwa vingi na kuleta hisia kwamba hali hii sasa ni janga la Kitaifa, ni muhimu Watanzania wakafahamu kwa takwimu kuhusu ukubwa wa tatizo la vifo na majeruhi kutokana na ajali za barabarani badala ya kusikia taarifa ya tukio moja moja:- (a) Je, takwimu ni zipi na mchanganuo wa matukio kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 Kitaifa na Mikoa miwili inayoongoza na yenye ajali chache? (b) Je, mfumo gani endelevu kama upo, wa wazi ambao Serikali inatumia kutoa takwimu hizi kwa Watanzania badala ya taarifa moja moja pindi inapotokea?

Supplementary Question 1

MHE. OSCAR R. MUKASA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa idadi ya karibu vifo 12,000 vilivyosababishwa na ajali za barabarani kwa miaka hiyo mitatu vinaweza kulinganishwa na mauaji ya kimbari, mauaji ya halaiki, na majeruhi 44,444 ni sawa na kiwanda cha kutengeneza Watanzania kupata ulemavu wa viungo mbalimbali. Je, Serikali inatueleza nini kuhusu kuja na suluhisho lenye mashiko na kutatua tatizo hili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa ajali za barabarani hasa za mabasi ya abiria zinashiriki sana kwenye kutengeneza vifo na majeruhi, tena kwa kiwango kikubwa kwa mara moja, Je, Serikali ina mkakati gani pia kudhibiti ajali za barabarani zinazohusisha mabasi ya abiria?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa na mipango na mikakati mbalimbali ya muda mrefu na muda mfupi. Miongoni mwa mikakati hiyo ni kama ifuatavyo:-
Kwanza, tunajaribu kutoa elimu kwa umma kupitia vyombo mbalimbali vya habari. Pia Jeshi la Polisi kupitia Askari wa Usalama Barabarani wamekuwa wakifanya doria za mara kwa mara na ukaguzi ili kuweza kuwabaini na kuwakamata wale ambao wanavunja sheria. Pia kumekuwa na utaratibu wa kutumia zile kamera za tochi ambazo zinabaini wale ambao wanakiuka taratibu za usalama barabarani ikiwemo kuongeza kiwango cha speed zaidi ya kilichowekwa kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa pia tukiangalia mchakato wa kuangalia utaratibu wa utoaji leseni vile vile ili kudhihirisha kwamba kwa kushirikiana na mamlaka nyingine watu wote ambao wanaendesha vyombo vya moto barabarani basi wawe ni ambao wana leseni zilizopo kisheria na isiwe kuzipata kinyemela. Pia kuna utaratibu wa kuchukua hatua stahiki kwa wanaovunja sheria siyo tu wale ambao wanaendesha vyombo hivi, hata wasimamizi wa sheria hizi mara moja inapotokea kutaka kulitia madoa Jeshi la Polisi basi hatua zimekuwa zikichukuliwa dhidi yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na mifumo ambayo tumejaribu kuanza nayo sasa hivi, mifumo ya matumizi ya point ambayo bado haijaanza ipo katika utaratibu mzuri, nadhani muda siyo mrefu sana tutaweza kutumia ili kuwafanya sasa watu wawe na hofu zaidi ya kuvunja sheria hizo za barabarani. Pia kuna utaratibu wa tozo za papo kwa papo na hii imesaidia sana kiasi fulani kudhibiti ajali hizo. Tuna utaratibu wa kutumia TEHAMA kwa ajili ya kudhibiti ajali za barabarani. Pia tuna mipango, maana alitaka mipango ya sasa hivi na baadaye, tunayo mipango ya matumizi ya kamera ambayo nayo vile vile ipo katika michakato na ukaguzi wa lazima kwa magari yote. Kwa hiyo, hizo ni baadhi ya hatua ambazo Serikali imekuwa ikichukua katika Jeshi la Polisi kupitia kitengo cha Polisi cha Usalama Barabarani kudhibiti hali ya ajali nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kiasi fulani imepungua, na ndiyo maana ukiangalia kwenye takwimu nilizozisoma kwenye swali la msingi utakuta ajali za barabarani zimekuwa zikipungua mwaka hadi mwaka.

Name

Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:- Kwa miaka ya hivi karibuni vifo vya Watanzania kutokana na ajali za barabarani vimekuwa vingi na kuleta hisia kwamba hali hii sasa ni janga la Kitaifa, ni muhimu Watanzania wakafahamu kwa takwimu kuhusu ukubwa wa tatizo la vifo na majeruhi kutokana na ajali za barabarani badala ya kusikia taarifa ya tukio moja moja:- (a) Je, takwimu ni zipi na mchanganuo wa matukio kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 Kitaifa na Mikoa miwili inayoongoza na yenye ajali chache? (b) Je, mfumo gani endelevu kama upo, wa wazi ambao Serikali inatumia kutoa takwimu hizi kwa Watanzania badala ya taarifa moja moja pindi inapotokea?

Supplementary Question 2

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na sababu ambazo Mheshimiwa Waziri amezizungumza, naamini kabisa baadhi ya ajali, tena ajali nyingi sana zinatokea kwa sababu ya kutokuwa na alama barabarani pamoja na matuta makubwa sana. Tulishasema hapa Bungeni matuta yawe na standards. Ni lini Serikali itafanya matuta nchi nzima yawe ya standard ili kuepusha ajali ambazo siyo za lazima?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kudhibiti ajali barabarani ni suala ambalo ni mtambuka linahusisha taasisi mbalimbali. Kwa mfano, suala ambalo Mheshimiwa Suzan Lyimo amelizungumza ni la msingi, ambalo kwa upande wa Serikali linahusisha Wizara ya Ujenzi na ndiyo maana tukawa na mkakati kabambe wa kushirikisha wadau wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muda muafaka utakapofika tunaweza tukauanika mpango huu, tupo katika hatua nzuri ambapo tuna ushirikiano mzuri na SUMATRA, Wizara ya Ujenzi kupitia TANROADS, TBS na shule za udereva pamoja na Polisi, tunakaa pamoja ili tuweze kuwa na utatuzi wa kudumu wa matatizo ya ajali kwa kuunganisha nguvu kwa pamoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimtoe tu wasiwasi kwamba mambo hayo tunayafanyia kazi na wakati muafaka utakapofika basi tutauweka hadharani.