Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 26 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 212 2016-05-23

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Kwa miaka ya hivi karibuni vifo vya Watanzania kutokana na ajali za barabarani vimekuwa vingi na kuleta hisia kwamba hali hii sasa ni janga la Kitaifa, ni muhimu Watanzania wakafahamu kwa takwimu kuhusu ukubwa wa tatizo la vifo na majeruhi kutokana na ajali za barabarani badala ya kusikia taarifa ya tukio moja moja:-
(a) Je, takwimu ni zipi na mchanganuo wa matukio kuanzia mwaka 2013 hadi 2015 Kitaifa na Mikoa miwili inayoongoza na yenye ajali chache?
(b) Je, mfumo gani endelevu kama upo, wa wazi ambao Serikali inatumia kutoa takwimu hizi kwa Watanzania badala ya taarifa moja moja pindi inapotokea?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013 zilitokea ajali 23,842 zilizosababisha vifo karibu 4,002 na majeruhi 20,689. Mwaka 2014 kulitokea ajali 14,260 zilizosababisha vifo 3,760 na majeruhi 14,530 na mwaka 2015 zilitokea ajali 8,337 zilizosababisha vifo 3,464 na majeruhi 9,383.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mikoa ambayo imeongoza kwa ajali kwa mwaka 2013 ni Mikoa ya Kipolisi ya Kinondoni, ambao ulikuwa na ajali 6,589 na Mkoa wa Kipolisi wa Ilala ambao ulikuwa na ajali 3,464 na mkoa ambao ulikuwa na ajali chache ilikuwa ni Simiyu ambao ulikuwa na ajali 67 na Tanga ajali 96. Mwaka 2014 mikoa iliyoongoza kwa ajali ni Mikoa ya Kipolisi Kinondoni ambapo ajali zilikuwa ni 3,086 na Mkoa wa Kipolisi wa Ilala ulifuata kwa kuwa na ajali 2,516. Mikoa ambayo ilikuwa na ajali chache kwa mwaka huo ilikuwa ni Kagera ambayo ilikuwa na ajali 29 na Simiyu ajali 55. Mwaka 2015 Mkoa wa Kipolisi ya Ilala ajali 1,431 na Temeke ajali 1,420 ambayo ndiyo iliyokuwa inaongoza kwa mwaka huo. Mikoa ambayo ilikuwa na ajali chache kwa mwaka 2015 ni Mkoa wa Rukwa ambao ulikuwa na ajali 53 pamoja na Mkoa wa Arusha ambao ulikuwa na ajali 53.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo endelevu wa wazi uliopo wa kutoa takwimu za kupitia taarifa za mwaka za Jeshi la Polisi (Police Annual Reports) ambapo kila Mtanzania anaweza kupata taarifa hizo za ajali.