Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ally Juma Makoa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Primary Question

MHE. ALLY J. MAKOA aliuliza: - Je, ni Wananchi wangapi Kondoa Mjini walioharibiwa mazao yao na tembo wamehakikiwa na lini watalipwa?

Supplementary Question 1

MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Moja; kwa kuwa kiwango wanacholipwa wakulima walioharibiwa mazao na wanyama ni kidogo sana.

Je, Serikali ina mpango gani wa kubadili sheria, ili kuweza kuwalipa wananchi kulingana na thamani ya mali zao zinazoharibiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa, pamekuwa pakitokea matukio haya ya tembo mara kwa mara katika maeneo hayo hususan Kijiji cha Chemchem, ni lini Serikali sasa itatujengea kituo cha Askari wa Hifadhi, ili kuweza kuzuia athari zaidi katika mzao ya wananchi? Ahsante. (Makofi)

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza mawili, ya Mheshimiwa Ally Makoa, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wananchi wamekuwa wakilipwa kiwango kidogo. Na kiwango hiki cha kifuta machozi ama kifuta jasho ni ile tu kutoa pole kwa wananchi na kuweka mazingira ya ushirikiano baina ya uhifadhi na wananchi, lakini tulipata maelekezo katika Bunge lako hili Tukufu wakati wa bajeti kwamba, tupitie kanuni za sheria hizi na tayari Wizara imeshaanza kuzipitia kwa ajili ya kurejea upya kanuni hizi, ili kifutajasho basi kiweze kuongezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ninamuahidi Mheshimiwa Mbunge wa Kondoa Mjini, Mheshimiwa Ally Makoa kwamba, katika bajeti hii ya 2022/2023 tumeoanga kujenga vituo 13, vituo hivi vitapelekwa katika Jimbo lake ili tuweze kupeleka Askari waweze kuendelea na zoezi la kuzuia wanyamapori wakali na waharibifu.

Name

Anne Kilango Malecela

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Same Mashariki

Primary Question

MHE. ALLY J. MAKOA aliuliza: - Je, ni Wananchi wangapi Kondoa Mjini walioharibiwa mazao yao na tembo wamehakikiwa na lini watalipwa?

Supplementary Question 2

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Waziri umeshafika kwenye Jimbo langu ndani ya Kata ya Maore, umeona ni kiasi gani wananchi wangu wanauawa na kuharibiwa mazao yao. Je, huoni umuhimu sasa kujenga kituo pale ndani ya Kata ya Maore ili uepushe maisha ya wananchi wangu na hatari? Ahsante.

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mama Anne Kilango, Mbunge wa Same, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nilifika katika eneo hilo la Maore na kuna changamoto kubwa sana ya wanyama wakali na waharibifu. Tuliahidi kujenga bwawa lakini pia tutapeleka kituo ambacho kitasaidia hawa wananchi kupunguza adha hii ya wanyama wakali na waharibifu. (Makofi)