Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Felista Deogratius Njau

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FELISTA D. NJAU aliuliza: - Je, ni lini Serikali itaajiri Maafisa Habari katika Balozi zetu ili kuutangaza nchi na vivutio mbalimbali?

Supplementary Question 1

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Balozi nyingi nje ya nchi hazifanyi vizuri kwa ufanisi katika kutangaza fursa za nchi yetu vivutio pamoja na utalii. Nini mkakati madhubuti wa Serikali kuhakikisha Balozi hizi zinafanya vizuri?

Swali la pili, kwa kuwa balozi zetu nyingi nje ya nchi hazina watumishi wa kutosha hasa balozi za kimkakati kama Congo na kwingineko, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi? (Makofi)

Name

Amber. Mbarouk Nassor Mbarouk

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Felista Deogratius Njau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kama nilivyoelezea katika swali la msingi, kwamba utekelezaji wa diplomasia ya uchumi ni kipaumbele muhimu cha Wizara ya Mambo ya Nje na Wizara imekuwa ikifanya juhudi mbalimbali ili kuhakikisha kwamba sera hiyo inatekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati ambayo inafanya kwanza ni Wizara ni kukiimarisha Kitengo chetu cha Mawasiliano ya Serikali ili kuhakikisha kwamba kinatoa taarifa zote muhimu kwa wadau kuhusu fursa zinazopatikana nje ya nchi na pia fursa ambazo zipo katika nchi yetu na hiyo imefanyika kwa ufanisi sana kwa sababu mfano Ubalozi wetu wa China ni ushahidi kwamba kitengo chetu kinafanya kazi vizuri kwa sababu ni taarifa nyingi ambazo Ubalozi wetu wa China zinapatikana kule na pia Serikali hapa na wananchi kwa ujumla wanapata taarifa nyingi za Ubalozi wetu na China na Balozi nyingine pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la watumishi, ni kweli kwamba ninaungana na Mheshimiwa Mbunge kwamba hapo nyuma kidogo hilo tatizo la ukosefu wa wafanyakazi lilikuwepo na lilikuwa ni kubwa, hata hivyo kwa hivi sasa tayari Serikali imechukua juhudi maalum za kuhakikisha kwamba suala hili halipo. Mfano, katika mwaka uliosha wa 2021/2022 jumla ya wafanyakazi 140 walipelekwa kwenye Balozi zetu mbalimbali nje ya nchi na suala hili ni endelevu, na tayari hivi sasa Wizara yetu imepata kibali cha kuajiri Maafisa wengi tu ambao watakuwepo Makao Makuu kwa ajili baadaye miaka ya mbele huko waweze kwenda kutumikia katika Balozi zetu.